Habari za Punde

Madrasa zote zikaguliwe – Asasi za kijamii


Na.Mwandishi Wetu.
Asasi za Kiraia zinazopambana na ukatili wa kinjisia kwa wanawake na watoto Zanzibar, zimetiwa moyo na hatua zilizochukuliwa na Afisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kuifungia Madrasa ya Ridhwaa Al Rasuul iliyopo Jangombe Jijini Zanzibar, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, baada ya kutuhumiwa  kuwafanyia udhalilishaji wanafunzi wa Madrasa hiyo.

Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kupitia kwa Katibu wake Sheikh. Khalid Ali Mfaume pia imepiga marufuku walimu wa Madrasa hiyo kusomesha katika madrasa nyengine yeyote ile.

Asasi za Kiraia zimekuwa zikifuatilia kwa makini mwenendo wa makosa ya udhalilishaji nchini ikiwemo kutoa elimu na kusaidia hatua za kisheria wahanga ambapo kwa muda mrefu imegundua baadhi ya walimu wa madrasa kuhusika kwa namna moja ama nyengine.
 
Asasi za Kiraia zinaamini kuwa walimu wa madrasa ni watu wazuri sana na wenye maadili mazuri na wanaoamrisha matendo mema kwa watoto na jamii kwa ujumla lakini bahati mbaya kuna walimu ambao wanatumia vibaya nafasi zao, hivyo ni muhimu kuwafungia na kuwapeleka katika vyombo husika ili kuendeleza mustakbali mwema wa taifa letu.

Hivyo, Asasi zinaomba Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kuendelea kuzipitia na kuzikagua Madrasa nyengine ambazo bado zinaendelea kufanya vitendo vya udhalilishaji Unguja na Pemba.

Pia zinaiomba Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kuweka mikakati maalum kuhakikisha kuwa walimu hao hawaajiriwi katika madrasa nyengine zozote na jamii pia inakuwa na uelewa wa walimu hao.

Zinaomba pia tuhuma hizo zifikishwe katika vyombo husika ili sheria iweze kuchukua mkondo wake na kukomesha vitendo hivyo ya udhalilishaji dhidi ya watoto wadogo ambavyo huathiri mpangilio mzima  wa maisha yao. 

Zaidi ya watoto 20 wameripotiwa katika matukio mbali mbali kuwa walifanyiwa vitendo vya udhalilishaji na walimu wa madrasa wa vyuo mbali mbali vya Unguja na Pemba katika kipindi cha miaka miwili

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa katika kipindi maalum cha redio Jamii ya Micheweni Kisiwani Pemba na Mkuu wa Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba hivi karibuni Bi Salama Mbarouk Khatib ni kwamba katika shehia ya Chimba kisiwani Pemba watoto 15 wameharibiwa na walimu wa Madrasa mbali mbali ziliyopo katika Kisiwa hicho.

Mkuu wa Wilaya ya Micheweni.Bi.Salma Mbarouk Khatib amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Walimu wa Madrasa ya Konde,Matangatuani,Viamboni,Kiwandani na Kijiji cha Chanjani Konde.

Kwa upande wa Unguja, Asasi za Kiraia zimerikodi matokeo zaidi ya matano ya udhalilishaji ambayo walimu wa madrasa wamehusishwa katika maeneo tofauti ikiwemo eneo la Kisauni, Magogoni na Kitope.

Hivi karibuni kesi mbili za udhalilishaji zimetolewa hukumu zilizokuwa zikiwakabili walimu wa madrasa. Mahakama ya Mkoa Vuga, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja imetoa adhabu kwa Mwalimu Abdulkadir Rajab Miraji (19) aliyehukumiwa kwenda jela kwa kipindi cha miezi sita.

Pia Mahakama ya Mkoa Chakechake, Mkoa wa Kusini Pemba, imemhukumu Mwalimu wa Madrasa Abubakar Juma Kombo (18) kwenda jela miaka 12.

Asasi za Kiraia zinaunga mkono jitihada za taasisi na watu binafsi waliohusika kufuatilia udhalilishaji huu na kuomba taasisi nyengine kuchukua mfano wake.

Tamko hili limetolewa na Chama cha wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), Jumuia ya Wanawake Wenye Ulemavu (JUWAUZA), Mtandao wa Jinsia Zanzibar (ZGC), na Chama cha Waandishi wa habari Wanawake Tanzania, (TAMWA, ZNZ.
Mkurugenzi wa ZAFELA, Jamila Mahmoud
Mwenyekiti wa JUWAUZA, Salma Saadat
Mwenyekiti ZGC, Asha Aboud
Mkurugenzi TAMWA, ZNZ, Dkt Mzuri Issa

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.