Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Ahutubia Maadhimisho ya Miaka Mitano ya (Barefoot Cholllege Zanzibar ) Kinyasini Wilaya ya Kaskazini "A" Unguja leo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia katika hafla ya Maadhimisho ya Miaka Mitano ya Kituo cha Wanawake cha Utengenezaji Vifaa vya Nishati ya Umeme wa Jua Kinyasini Wilaya ya Kaskazini"A" Unguja leo 8/8/2020.                  


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema Wizara ya Kazi, Uewezeshaji, Wazee, wanawake na watoto ina jukumu la  kukaa pamoja na Uongozi wa Kituo cha Wanawake kinachotengeneza Vifaa vya Umeme wa Jua  “Barefoot Callege’ ili kuandaa mwelekeo wa kituo hicho baada ya kukamilika kipindi cha miaka mitano tangu kIfunguliwe.

Dk. Shein amesema hayo leo huko Kinyasini Mkoa wa Kaskazini Unguja katika sherehe za kutimiza miaka mitano tangu kuanzishwa kwa kituo hicho, hafla iliyokwenda sambamba na ufunguzi wa jengo jipya la dakhalia kwa ajili ya wanafunzi 

Alisema kwa kuzingatia sera na maelekezo ya Serikali,  Wizara hiyo inapaswa kukaa pamoja na Uongozi wa kituo hicho na kuanza kufikiria mahitaji ya baadae ya kituo, ikiwemo eneo la ardhi litakalotumika kwa ajili kuongeza majengo na baadhi ya nyenzo muhimu zitakazohitajika.

Alisema kuwepo kwa changamoto mbali mbali, ikiwemo uhaba wa madarasa na mabara ya kufundishia, ukosefu wa mahala pa kusalia kwa ajili ya washiriki wengi wa mafunzo pamoja na ukosefu wa lami katika eneo dogo la barabra inayoingia kituoni hapo ni mambo yanayohitaji kutafutiwa ufumbuzi na Wizara hiyo.

“Nauagiza Uongozi wa Wizara uchukue hatua ya kuzitatua changamoto hizo, zile ziliomo ndani ya uwezo wao moja kwa moja na zile zinazohitaji mashirikiano na taasisi nyeingine wazishughulikie”, alisema.

Alisema kuna umuhimu wa kukiendeleza kituo hicho kwa kuzingatia hali halisi ya mazingira ya Zanzibar na mabadiliko ya dunia.

Aidha, Dk. Shein aliuagiza uongozi wa kituo hicho kuunda jumuiya ya Wanafunzi wanaomaliza mafunzo kituoni hapo pamoja na kutoa mialiko ya kufika kituoni ili kueleza namna walivyofaidika na mafunzo, jinsi wanavyoitumia taaluma waliyoipata na mafanikio yao.

Alieleza kuwa kuna mafanikio makubwa yaliopatikana na kituo hicho ndani ya kipindi cha miaka mitano na kuwashukuru wale wote waliochangia katika kufanikisha uendeshaji mzuri wa kituo hicho.

Alisistiza umuhimu wa viongozi wa kituo hicho kuwa na utaratibu mzuri wa kutunza na kuweka kumbu kumbu za historia ya kituo hicho.

Alisema ni jambo la kujivunia kuona kituo hicho kinapokea wanafunzi kutoka Tanzania Bara na nchi za jirani, na kubainisha kuwa hilo ndio lengo la serikali tangu kituo hicho kilipoanzishwa.

“Hili lilikuwa ndio lengo la serikali tangu mwanzo kituo hiki kiwe kwa ajili ya nchi za Afrika Mashariki na kati, sina shaka washirki kutoka nchi mbali mbali watakuja miaka ijayo na kituo hiki kuwa na hadhi ya Kimataifa”, alisema.

Alieleza ni vyema kituo kikawa na uatartibu wa kutunza vyema takwimu na kumbukumbu za usajili wa wanafunzi wapya na taarifa zao muhimu zinazohusiana na usajili huo ikiwemo mahali wanapotoka na kuzihifadhiwa vizuri.

Aidha, Dk. Shein aliutaka Uongozi wa kituo hicho  kufuatilia kwa karibu maendeleo ya wahitimu wote  baada ya kumaliza mafunzo yao pamoja na kuziwekea kumbukumbu taarifa zao.

“Mnahitajika kuwa na mawasiliano na wanafunzi wanaomaliza mafunzo na kuwaalika katika hafla zenu muhimu, wanafunzi hao ‘Alumn’ ni kiungo muhimu katika kukiendeleza na kukikuza kituo hiki kwa kukitangaza na kukipa msukumo”, alisema.

Alitumia fursa hiyo kuipongeza kwa dhati Serikali ya India kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukiendeleza kituo hicho na kusema ufunguzi wa jengo hilo ni uthibitisho wa ushirikiano mwema wa nchi mbili hizo na dhamira ya kukifanya kituo hicho kuwa maarufu  na chenye kupendwa katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Akigusia mipango na mikakati ya serikali katika kutafuta vianzio mabadala vya umeme, badala ya kutegemea kianzio kikuu kimoja, Dk. Shein alisema serikali imepata mafanikio makubwa katika kuiendeleza miundombinu  mikuu ya umeme na usambazaji wake kupitia nishati ya jua,

Alisema Serikali na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya zimeshrikiana kufanya tafiti  juu ya uwezekano wa kupata nishati hiyo, huku matokeo yakionyesha kuwepo uwezekano mkubwa wa kupata kiwango kikubwa cha umeme kupitia chanzo hicho.

“Benki ya Dunia imeonyesha nia ya kutuunga mkono kwa kuanza na Megawati 35, ambapo zaidi ya wawekezaji 30 wamevutwa na mipango yetu na kuonyesha dhamira njema ya kushirikiana nasi”, alisema.

Alieleza pale umeme wa uhakika utakapopatikana kazi ya kusambaza umeme huo kwa wananchi itakuwa rahisi, kwa kuzingatia miundombinu ya umeme ipo katika shehiya zote za Unguja na Pemba..

Vile vile, alisema kuna kila sababu ya kukiendeleza kituo hicho Barefoot College kwa kuzingatia hali ya hewa iliopo nchini inayotoa fursa nzuri ya kuendeleza umeme wa jua.

Aidha, Dk. Shein alibainisha juhudi mbali mbali zinazochukuliwa na serikali katika kuwawezesha na kuimarisha ustawi wa wanawake, kupitia Mfuko wa Uwezeshaji wananchi kiuchumi pamoja na ule wa Vijana unaotekelezwa na  Serikali kwa kushirikiana na Uongozi wa Mfuko wa Khalifa Fund.

“Teknolojia hii ya umeme wa jua inaendana vizuri na mazingira pamoja na Jiografia ya nchi yetu na ndio maana utafiti uliofanyika umependekeza kwanza tuendeleze umeme wa jua kuliko vianzio vyengine vya nishati ya umeme”, alisema.

Rais Dk.Shein aliwataka akinamama kuongeza ari katika kujifunza teknolojia hiyo ili iweze kuwanufaisha wao pamoja na watu mbali ,mbali wanaohitaji.

“Ni fahari kubwa kuona mama anaweza kutatua tatizo la umeme nyumbani yeye mwenyewe bila kumsubiri baba au kutafuta fundi kutoka nje”, alisema.

Dk. Shein alionyesha matumaini yake na kusema pale akinamama hao watakapoongeza ari na kujituma, kutafuta utaalamu zaidi na kubuni mbinu mbali mbali za kuendeleza ujuzi huo, kituo hicho kitaweza kuwa kituo kikubwa na maarifu sana katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Ulimwenguni.

Katika hafla hiyo Dk. Shein alipata fursa ya kutembelea na kuangalia kazi za ujasiriamali zinazoendeshwa na washriki wa mafunzo ya kituo hicho pamoja na kupokea zawadi mbali mbali kwa ajili yake na Mama Mwanamwema Shein.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein alipongeza uongozi wa kituo hicho kwa kubuni nyanja mpya za mafunzo yahusuyo ujasiriamali, ukiwemo ufugaji  wa nyuki na  ufumaji , hatua aliyosema itakuza uchumi wa familia na nchi kwa ujumla.

Aidha, alibainisha juhudi mbali mbali  zinazochukuliwa na Serikali za kuwawezesha na kuimarisha ustawi wa wanawake, kupitia Mfuko wa Uwezeshaji wananchi Kiuchumi pamoja na ule wa Vijana unaotekelezwa na Serikali kwa mashirikianao na Uongozi wa Khalifa Fund.

Mapema, Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na watoto, Moudline Castico, alisema Wizara hiyo itaendelea na juhudi za kukiendeleza kituo hicho ili kufanikisha dhamira ya kuanzishwa kwake.

Nae, Balozi Mdogo wa India nchini, Bhagwant Singh alisema Serikali ya India itaendelea kuunga mkono juhudi za kukiimarisha kituo hicho ili kuweza kupata mafanikio makubwa.

Alisema ana matumaini makubwa kuwa ushirikiano uliopo kati ya India na na Zanzibar na Tanzania  kwa ujumla utaendelea kuimarika kwa maslahi ya watu wa nchi mbili hizo.

Katibu Mkuu Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, wanawake na watoto Fatma Gharib Bilali alisema jumla ya akinamama 45 wameweza kunufaika na kutokana na mafunzo ya utengenezaji wa vifaa vya umeme wa jua, ikiwemo 13 waliopata mafunzo hayo nchini India, ambapo sasa ni wakufunzi wa kituo hicho.

Alisema jumla ya nyumba 958 kutoka shehiya mbali mbali za Unguja na Pemba  tayari zimeunganishwa umeme wa jua kupitia washiriki wa mafunzo ya kituo hicho.

Aidha, alisema kituo hicho kimekuwa kikiendesha mafunzo ya ujasiriamali, ikiwemo ushoni wa nguo na ufugaji nyuki, ambapo katika kipindi cha maradhi ya COVID 19 kiliweza kushona Barakoo 30,000 na kusambazwa katika maeneo mbali mbali ya nchi, ikiwemo Wizarani, Manispaa, Wilaya za Mkoa Kusini Unguja na baadhi ya taasisi za Serikali.  

Mkuu wa kituo cha Barefoot College, Pendo alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliopatikana katika uendeshaji wa kituo hcho, kuchelewa kupatikana vifaa vya umeme wa jua ni miongoni mwa changamoto zinazokikabili kituo hicho.

Kituo cha Barefoot College, kilizinduliwa rasmi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein mnamo Augosti 6, 2015.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.