Habari za Punde

SMZ Haijahusisha Mfadhili Katika Bajeti ya Uchaguzi Mkuu 2020

Na. Jaala Makame Haji- ZEC                                                              

Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), itaendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na wadau wa Uchaguzi ili kuhakikisha Uchaguzi Mkuu utakaofanyika tarehe 27 na 28 Octoba mwaka huu unafanyika kwa salama na Amani.

Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mkuu Mstaafu Hamid Mahmoud Hamid wakati akizungumza na Viongozi wa Dini mbali mbali kisiwani Pemba katika Ukumbi wa kiwanda cha mafuta ya Makonyo Wawi Pemba

Mwenye Hamid Mahmoud alisema, tokea kuanza kwa zoezi la matayarisho ya  hatua mbali mbali za Uchaguzi ZEC, imekuwa karibu na wadau wake kwa kufanya mikutano mbali mbali inayohusiana na suala hilo ikiwa na dhamira hiyo ya kuwepo amani na utulivu .

Aliwataka viongozi wa dini waendelee katika kuhamasisha kampeni na hatua nyengine za uchaguzi kwa utulivu na amani ili nchi iendelee kutajika kuwa visiwa vya amani.

Alifahamisha kuwa, katika kuzingatia nafasi ya viongozi hao katika jamii iliyowazunguuka Tume imeona kuwa wao ni wadau muhimu wa Uchaguzi na inatambua umuhimu wao kwa vile wanaongoza kundi kubwa katika jamii.

Jaji Mahamoud, aliwaomba Viongozi hao kuendelea kuhubiri amani kwa wananchi wote wakati,  kabla na baada ya Uchaguzi pia kuendelea kuhamasisha na kutoa elimu kwa jamii ili iweze kushiriki kikamilifu katika masuala ya Uchaguzi.

Mwenyekiti huyo alifahamisha kuwa, utunzaji wa amani ni wajibu wa kila mwananchi katika Taifa hili, hivyo kila mmoja wetu atumie muda wake kuitunza amani iliopo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uchaguzi (ZEC) Thabit Idarous Faina, akiwasilisha mada juu ya matayarisho ya Uchaguzi Mkuu 2020, alieleza kwamba Tume hiyo tayari imeshafanya mambo mengi na kuchukuwa hatuwa mbali mbali juu ya mchakato wa uchaguzi ambazo zitawezesha kukamilisha uchaguzi huo kwa mafanikio makubwa.

Alifahamisha kuwa, miongoni mwa mambo hayo ambayo tayari yamekamilika ni uandikishaji wa wapiga Kura Wapya na uhakiki wa taarifa za wapiga kura ambapo jumla ya wapiga kura 566,352 waliandikishwa na wanatarajiwa kuwa Wapiga Kura  katika uchaguzi mkuu wa 2020.

Aliendelea kueleza kuwa, Tume ya Uchaguzi imefanya uteuzi wa Wagombea 17 wa ngazi ya Uraisi wa Zanzibar, Wagombea 252 Ujumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa majimbo mbali mbali ya Uchaguzi na Wagombea wa Udiwani 360 kwa Wadi zote.

Aidha, akizungumzia kuhusu Waangalizi wa Uchaguzi Mkurugenzi Faina alifafanua kuwa, Tume imeruhusu kuwepo kwa waangalizi wa Uchaguzi katika Uchaguzi Mkuu 2020 na jumla ya taasisi 61 za ndani ziliomba kupatiwa vibali na zilizokidhi vigezo ni 35.

Alifahamisha kuwa jumla ya taasisi 15 za kimataifa ambazo zimepatiwa vibali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi NEC zimeomba pia kupatiwa kibali kuangalia Uchaguz wa Zanzibar.

Sambamba na hayo, pia Mkurugenzi alibainisha kuwa kwa mara ya Kwanza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetumia bajeti yote ya Uchaguzi kwa ukamilifu bila hata kutumia pesa za wafadhili.

Alisema Tume ili kuhakikisha inaendesha uchaguzi huo bila ya kuwepo malalamiko , ilipitia upya matakwa ya sheria mpya ya Uchaguzi , maelekezo ya miongozo juu ya majukumu kwa Wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi na vituo pamoja na majukumu yao.

Hata hivyo wadau wa Uchaguzi wanalojukumu la kuhakikisha uchaguzi na harakati zake unakamilika kwa amani na Tume itakuwa karibu kufanya kazi nao kwa mashirikiano  makubwa ili kukamilisha kazi ya uendeshaji wa uchaguzi kwa salama na amani.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.