Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk Hussein Ali Mwinyi afanya ziara ya kushtukiza Hospitali ya Rufaa Mnazimmoja atoa miezi mitatu kuhakikisha utendaji kazi unabadilika

                                                         

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Hussein Ali Mwinyi  akizungumza na Wananchi na Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja leo baada ya kumaliza zuiara yake ya kustukiza Mchana huu na kujionea  utendaji Kazi wa Wafanyakazi wa Hospitali hiyo na kutoa miezi mitatu kukamilisha kasoro zote katika Hospitali hiyo. 

RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ametoa muda wa miezi mitatu kwa uongozi wa Wizara ya Afya kurekebisha kasoro za kiutendaji zinazosababisha kutokuwepo  ufanisi katika utoaji wa huduma bora kwa wagonjwa.

Dk. Mwinyi ametoa kauli hiyo  wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mnazi mmoja, alipofika kuangalia utoaji wa huduma kwa wagonjwa katika maeneo na vitengo  tofauti  vya Hospitali hiyo.

Alisema kwa kiwango kikubwa mambo mengi yanahitaji kufanyiwa marekebisho, akibainisha kuwepo changamoto mbali mbali za kiutendaji na hivyo kuzorotesha uapatikanaji wa huduma bora kwa wagonjwa.

Alisema analenga kuchukua hatua za kiutawala dhidi ya watendaji wasiowajibika kazini na kusababisha wananchi kulalamika kutokana na ukosefu wa huduma, pamoja na kupewa lugha zisizordhisha kutoka kwa wauguzi na watendaji wengine  wa Hospitali hiyo.

Aidha, Dk. Mwinyi alisema pamoja na Serikali kuipatia fedha za kutosha Hospitali hiyo kila mwezi, kumekuwepo changamoto za ukosefu wa vifaa muhimu kwa wagonjwa ikiwemo magodoro, dawa na vifaa vya maabara, hivyo akautaka Uongozi wa Hospitali hiyo kubadilika na kuondokana na utendaji wa mazowea.

Alisema pale Serikali inapotoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa na hatimae wagonjwa wakakosa dawa hizo, ni dhahiri kuwa kuna tatizo mahala hapo.

Alieleza kuwa kumekuwepo matatizo madogo madogo katika uendeshaji wa Hospitali hiyo na kubainisha  kuwa; kama yangelishuhulikiwa ipasavyo , ni wazi kuwa huduma bora zingepatikana.

Aidha Rais Dk. Mwinyi , aliahidi kufanya ziara nyingine katika siku zijazo na kuzungumza na wafanyakazi kwa lengo la kuimarisha utendaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Alisema wafanyakazi wana wajibu wa kuwatumikia wagonjwa kikamilifu sambamba na kupata haki wanazostahili.

Aliwataka madaktari na wauguzi kuvaa vitambulisho ili kuondokana na urasimu kwa wagonjwa ambao hatimae huzaa rushwa.

Katika ziara hiyo Dk. Mwinyi alipata fursa ya kutembelea maeneo mbali mbali ya Hospitali, ikiwemo OPD  , MRI, Jengo la kuhifadhia Dawa, Kitengo cha Macho pamoja  na kusikiliza changamoto mbali mbali zinazokwamisha na kuzorotesha  utendaji kazi, sambamba na kuwajuilia hali wagonjwa, ikiwemo wale waliopata ajali.

Mapema, Mkurugenzi Uuguzi wa Hospitali ya rufaa ya Mnazi mmoja Dk. Haji Nyonje alisema Uongozi wa Hospitali hiyo ulilazimika kujenga Bohari mpya ya kuhifadhia dawa  kutokana na ongezeko la upatikanaji  wa Dawa hospitalini hapo.

Alisema changamoto kubwa llinaloikabili hospitali hiyo hivi sasa ni kuwa mashine za kufulia ambazo baadhi ya nyakati hushindwa kufanya kazi.

Dk. Nyonje aliahidi kuyafanyia kazi malalamiko ya wagonjwa wanaolazwa na kulazimika kwenda na mashuka yao wenyewe, mbali na Uongozi wa Hospitali hiyoo kununua mashuka ya kutosha katika kipindi cha hivi karibuni.

Nae, Daktari Mkuu Kitengo cha Macho, Dk. Slim Mgeni alisema pamoja na juhudi za Serikali kuimarisha upatikanaji wa vifaa, bado kunahitaji vifaa zaidi hususan katika suala zima la  kufanyia Operesheni.

Alisema katika kitengo hicho  kuna changamoto ya upungufu wa vitanda vya kulazia wagonjwa na hivyo kulazimika baadhi ya wagonjwa waliopata nafuu kuwapa ruhusa ya kwenda nyumbani baada ya kufanyiwa Operesheni.

Aidha, alisema kuna changamoto ya dawa , sambamba na ‘theatre’ mpya iliojengwa kutokukamilika, mbali na Mkandarasi aliepewa zabuni kukamilishiwa fedha zote za ujenzi.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 

 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.