Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la mapinduzi Dk.Hussei Ali Mwinyi (katikati) akiwasikiliza Uongozi wa Jumuiya ya Jumuiya ya Maimamu (JUMAZA) wakati wa mazungumzo yao Ikulu Jijini Zanzibar leo waliofika kumpongeza kutokana na ushindi alioupata katika uchaguzi Mkuu uliopita Mwaka 2020.[Picha na Ikulu] 28/12/2020.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la mapinduzi Dk.Hussei Ali Mwinyi (katikati) akisitiza jambo wakati wa mazungumzo na Ujumbe wa Jumuiya ya Maimamu (JUMAZA) waliofika Ikulu Jijini Zanzibar leo kumpongeza kutokana na ushindi alioupata katika uchaguzi Mkuu uliopita Mwaka 2020.[Picha na Ikulu] 28/12/2020.
STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
28.12.2020
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali
Mwinyi amesema kuwa Serikali anayoiongoza itahakikisha inashirikiana vyema na
Jumuiya ya Maimamu Zanzibar (JUMAZA) katika kujenga misingi ya dini ya Kiislamu
hapa nchini.
Dk. Hussein Mwinyi aliyasema hayo leo wakati
alipofanya mazungumzo na Wajumbe wa Jumuiya Maimamu Zanzibar (JUMAZA)
wakiongozwa na Kaimu Katibu Sheikh Ali Abdalla Amour.
Wajumbe wengine kutoka (JUMAZA) waliofika
Ikulu kuzungumza na Rais ni Dk. Moh’d Hafidh Khalfan, Sheikh Masoud Hemed
Nassor, Sheikh Yussuf Khamis, Sheikh Abdalla
Issa Makame, Sheikh Muhiddin Zubeir Muhiddin na Ukhti Halima Qasim
Moh’d.
Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Hussein
mwinyi alisema kuwa miongoni mwa mambo makubwa ambayo yanapaswa kupewa
kipaumbele katika kujenga misingi ya dini ya Kiislamu ni umoja, amani na mshikamano.
Hivyo, alieleza kuwa kuwepo kwa
maridhiano ya kisiasa hapa Zanzibar kumetoa nafasi nzuri ya kuimarisha umoja,
amani na mshikamano miongoni mwa viongozi, wananchi pamoja na kuamsha ari ya
kushirikiana.
Alisema kuwa hatua hiyo, imesaidia kuweka
pembeni kasoro zilizokuwepo hapo siku za nyuma hali ambayo itapelekea kupata
maendeleo makubwa hivyo, ni jukumu la viongozi wa siasa, viongozi dini pamoja
na wananchi kuhakikisha hilo linafanikiwa.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi alieleza juhudi za
makusudi zinazokusudiwa kufanywa na Serikali katika kupambana na udhalilishaji
wa kijinsia ikiwa ni pamoja na kuwaita wadau na kukaa nao pamoja na kujadili
hatua za kuchukuliwa katika kupiga vita janga hilo wakiwemo viongozi hao wa
dini ambao wako katika jamii.
Rais Dk. Mwinyi alieleza jukumu kubwa la
viongozi wa dini katia kuielewesha jamii juu ya athari za janga hilo ambalo hivi
sasa limeshika kasi katika jamii.
Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi pia,
alieleza haja ya kutafutiwa ufumbuzi changamoto za Hijja huku akieleza umuhimu
wa kuwepo Mfuko wa Hijja ambao umeweza kuzinufaisha nchi nyingi duniani ambazo zimeuanzisha.
Rais Dk. Mwinyi alieleza haja ya kuwekwa
kwa utaratibu maalum kwa ajili ya walimu wa madrasa ikiwa ni pamoja na kuwepo
miongozo ya utoaji elimu wa madrasa kwa mashirikiano ya viongozi wa dini,
Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Ofisi ya Mufti pamoja na Wadau ambao ni
walimu hao wa Madrasa.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi
alieleza azma ya Serikali ya kuwaangalia kimaslahi walimu pamoja na madaktari
kutokana na kazi kubwa wanazozifanya katika kutoa huduma katika jamii.
Nao Wajumbe wa Jumuiya hiyo ya (JUMAZA)
walimpongeza Rais Dk. Hussein Mwinyi kwa kuchaguliwa na wananchi wa Zanzibar na
kuweza kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
Katika maelezo yao walimpongeza kwa kasi
yake aliyoanza nayo katika kuwaletea maendeleo wananchi ikiwa ni pamoja na
kuona umuhimu wa kuwepo amani, umoja na mshikamano katika jamii na kuamua
kusimamia maridhiano.
Walieleza kuwa hatua zake za kurudisha
mshikamano nchini na kuleta umoja ni jambo kubwa na la kuungwa mkono na
kupongezwa kwani bila ya kuwepo amani,
umoja na mshikamano maendeleo hayawezi kupatikana.
Aidha, viongozi hao wa (JUMAZA),
walieleza haja ya kutafatwa hatua za makusudi za kupambana na udhalilishaji
katika jamii kwani janga hilo limekuwa likipoteza haiba ya nchi.
No comments:
Post a Comment