Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Husssein Ali Mwinyi Aongoza Wananchi Katika Dua Maalum ya Kumuombea Rais wa Kwanza wa Zanzibar Marehemu Abeid Amani Karume Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk. Hussein Ali Mwinyi akiongoza kisoma cha Dua na Hitma ya kumuombea Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Marehemu Abeid Amani Karume, iliofanyika katika ukumbi wa Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Jijini Zanzibar na (kulia kwa Rais) Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi na Waziri Mkuu wa Tanzania Alhajj Kassim Majaliwa na (kushoto kwa Rais) Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Othman Ngwali Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman na Rais Mstaaf wa Tanzania Alhajj Ali Hassan Mwinyi.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhadj Dk. Hussein Ali Mwinyi leo amejumuika na wananchi,  viongozi  wa Serikali pamoja na viongozi wa madhehebu mbali mbali ya Dini katika dua ya kumbukumbu ya muasisi wa Zanzibar, marehemu mzee Abeid Amani Karume.

Katika hafla hiyo iliyofanyika  Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui, pia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alihudhuria, ambapo viongozi na wananchi hao walishiriki katika kisomo maalum  na hatimae viongozi wakuu wakapata fursa ya  kuzuru kaburi la marehemu na kumuombea dua.

Katika Hitma hiyo iliyoongozwa na Sheikh Mohamed Abass,  Mufti wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kaab aliomba dua na kusema wakati wa uhai wake marehemu alileta neema kubwa kupitia Nyanja tofauti ikiwemo ujenzi wa majengo ya kisasa katika maeneo mbali mbali nchini, akilenga kuboresha maisha ya wananchi.

Alisema Marehemu mzee Abeid Amani Karume alisisitiza umoja na mshikamano miongoni mwa Wazanzibari pamoja na kuhakikisha kila mwananchi anaishi maisha mazuri katika Nyanja zote, ikiwemo upatikanaji wa chakula, malazi na makaazi.

Aidha, Sheikh Kaab alimuombea dua Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi  kwa kumuomba Mwenyezi Mungu aithibitishe azma yake inayolenga kuwepo umoja na mshikamano miongoni mwa Wazanzibari wote.

Mapema, Mjumbe wa Baraza la Maulamaa Zanzibar Sheikh Salum Batashi alimsifia Marehemu Karume kuwa ni kiongozi alieifanyia mambo mengi mazuri Zanzibar, jambo linaloendelezwa na viongozi wanaomfuatia.

Aliwataka waumini na wananchi kwa ujumla kumkumbuka na kumuombea dua marehemu Karume, kuyaenzi yale aliyoyaanzisha pamoja na kuwatakia rehema viongozi waliotangulia mbele ya haki , sambamba na kuwapa pole viongozi waliopo kwa misiba mbali mbali iliolikumba Taifa.

Katika hatua nyengine, Viongozi wa serikali, viongozi wa dini kutoka madhehebu mbali mbali nchini pamoja Mwakilishi wa Vyombo vya ulinzi na Usalama  walipata fursa ya kuweka mashada ya maua juu ya kaburi la Marehemu pamoja na kumuombea dua..

Dua ya kumbukumbu ya Marehemu Abeid Amani Karume, ambayo   hufanyika kila ifikapo April 7 ya kila mwaka, ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali, akiwemo Rais wa Jamuhuri ha Muuungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassimu Majaliwa pamoja na Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania  Ali Hassan Mwinyi.

Wengine, ni Rais mstaafu wa Zanzibar Abeid Amani Karume,  Makamo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Othman Masoud Othman, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdalla,Mawaziri wa SMZ na SMT pamoja na Mabalozi wadogo wanaoziwakilisha nchi zao waliopo  Zanzibar.

Aidha, wengine ni  Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Dk. Mwinyi Talib Haji,  Mwakilishi wa Familia ya Marehemu Balozi Ali Karume, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Sadalla ‘Mabodi’.

Vile vile hafla hiyo  Viongozi mbali mbali wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama nchini walihudhuria.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 

 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.