Habari za Punde

ULEGA ATAKA KUCHANGAMKIWA KWA SOKOLA KAA NA JONGOO BAHARI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (wa pili kutoka kulia) akiwa ameshikana mkono na Mwenyekiti wa kikundi cha Upendo Beach Bw. Mzee Makole, wakati Naibu Waziri Ulega akikabidhi msaada wa injini ya boti yenye thamani ya Shilingi Milioni 15 kwa ajili ya kukiimarisha kikundi hicho kwenye shughuli za uvuvi. Naibu Waziri Ulega amekabidhi msaada huo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi akiwa nje ya jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga wakati alipofika ziara ya kikazi ya siku moja mkoani humo. Wa kwanza kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Martine Shigella na kwanza kushoto ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini Mhe. Ummy Mwalimu
Katibu wa Kikundi Shirikishi cha Ulinzi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) katika Kijiji cha Tawalani, kilichopo Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga Bw. Salehe Ally Sua akifafanua jambo juu ya zao la mwani kwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Martine Shigella na Katibu Tawala wa mkoa huo Bi. Judica Omari, wakati Naibu Waziri Ulega alipofika katika kijiji hicho kuhamasisha kilimo cha zao la mwani na kutoa ahadi ya wizara ya kutoa msaada wa Shilingi Milioni Nne kwa ajili ya kununulia kamba maalumu ya kupandia zao hilo ambazo ameagiza zifike katika kikundi hicho ndani ya muda mfupi
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (wa kwanza kulia) akiwa kwenye mazungumzo na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Martine Shigella (aliyevaa kofia nyeusi) wakati Naibu Waziri Ulega alipotembelea shamba la wakulima wa mwani katika Kijiji cha Tawalani, kilichopo Wilaya ya Mkinga, Mkoani Tanga. Naibu Waziri Ulega amefanya ziara ya kikazi ya siku moja Mkoani Tanga na kuwataka wakulima wa mwani wazidi kuongeza uzalishaji na kujiunga kwenye vikundi vya ushirika na kuchangamkia fursa ya ukuzaji viumbe maji kwa kufuga kaa na jongoo bahari ambao wana soko kubwa nje ya nchi. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari – Wizara ya Mifugo na Uvuvi)

Na. Edward Kondela,MKINGA.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amewataka wananchi wanaofanya shughuli zao katika Ukanda wa Bahari ya Hindi kuchangamkia fursa ya ufugaji viumbe maji wakiwemo kaa na jongoo bahari ambao wamekuwa na soko kubwa nje ya nchi.

Akizungumza mwishoni mwa wiki (24.04.2021) katika Kijiji cha Tawalani kilichopo kata ya Manza iliyopo Wilaya ya Mkinga, Mkoani Tanga, wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja mkoani humo, Mhe. Ulega amesema Ukanda wa Bahari ya Hindi bado haujatumiwa vyema katika kuongeza pato la mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla, hivyo wananchi kujikita zaidi katika uvuvi na kutojishughulisha na ufugaji wa viumbe maji ambao wamekuwa wakitakiwa nchi mbalimbali.

Mhe. Ulega amebainisha kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amekuwa akizungumzia sana Sekta ya Uvuvi kuwekeza kwenye uchumi wa bluu, hivyo wananchi hususan wanaofanya shughuli za uvuvi wanatakiwa kuongeza wigo wa shughuli za kiuchumi katika Ukanda wa Bahari ya Hindi zikiwemo za ufugaji wa viumbe maji hususan kaa na jongoo bahari pamoja na kilimo cha zao la mwani.

“Shughuli za uchumi ziwe nyingi sana, rais anataka twende na uchumi wa bluu, anataka tufanye kazi twende baharini tufanye kazi lakini huku pwani tutengeneze vizimba kwa ajili ya shughuli mbalimbali mfano kunenepesha kaa na majongoo bahari na tufunge Kamba kwa ajili ya kulima mwani.” Amesema Mhe. Ulega

Ameongeza kuwa ni wakati sasa kwa wananchi wa ukanda huo kuondoa umasikini kwa kuendeleza shughuli za uvuvi, ufugaji wa viumbe maji pamoja na kilimo cha mwani ili waweze kuongeza mapato na kuwa na wigo mpana zaidi wa kuongeza kipato kwa mwaka.

Akisoma taarifa ya Kikundi Shirikishi cha Ulinzi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) mwishoni mwa wiki (24.04.2021) katika Kijiji cha Tawalani, katibu wa kikundi hicho Bw. Salehe Ally Sua amesema katika kipindi cha miezi kumi wamepata tani 52 za mwani na kuziuza kwa Shilingi Milioni 52 ambapo kwa sasa wamefanikiwa kupata soko la uhakika ambalo wanauza Shilingi 1,250 kwa kilogramu moja.

Aidha, amesema kupitia kilimo hicho kipato cha mtu mmoja mmoja kimeweza kuongezeka na kujikomboa kiuchumi hali ambayo imewasaidia kujipatia maendeleo na kumudu mahitaji mbalimbali ya kijamii.

Licha ya mafanikio hayo Bw. Sua amesema wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya mabadiliko ya hali ya hewa ambayo imekuwa ikiharibu zao hilo na kupanda na kushuka kwa bei ya zao mwani katika masoko mbalimbali hali ambayo inawafanya wakulima kushindwa kuweka mipango stahiki ya kilimo hicho pamoja na ukosefu wa vifaa kwa ajili ya kilimo hicho.

Katika ziara hiyo Naibu Waziri Ulega amesema wizara itatoa Shilingi Milioni Nne kwa ajili ya kununua kamba za kilimo cha mwani na kuelekeza fedha au kamba zenye thamani ya hiyo pesa ziwasilishwe haraka katika kikundi hicho.

Amesema fedha hizo ziwe chachu kwa ajili ya kukuza kilimo hicho na kwamba Wizara ya Mifugo na Uvuvi itazidi kutoa misaada mbalimbali kwa vikundi vinavyojishughilisha na kilimo cha zao la mwani kwa kutoa vifaa zikiwemo kamba ili kuongeza uzalishaji wa zao la mwani hali ambayo pia inaweza kuchochea uwepo wa viwanda vya kuzalisha bidhaa zitokanazo na mwani.

Akiwa katika ziara hiyo ya kikazi ya siku moja Mkoani Tanga, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ametoa msaada wa injini mbili za boti kwa ajili vikundi vya uvuvi vya Upendo Beach Group na Songambele.

Injini hizo zenye thamani ya shilingi Milioni 30 ambapo kila moja ina thamani ya Shilingi Milioni 15, Naibu Waziri Ulega amewataka wavuvi hao kutotumia vifaa hivyo kwa kujiingiza katika uvuvi haramu bali watumie kwa ajili ya uvuvi unaofuata sheria na kanuni na kwamba serikali bado inaendelea kuweka mazingira mazuri ya uvuvi kwa kuondoa tozo ambazo zimekuwa kero kwao.

Wakizungumza baada ya kukabidhiwa injini hizo, viongozi wa vikundi hivyo wamesema wamefurahishwa na msaada huo ambao utakuwa na tija kwao katika kuongeza kiwango cha uvuvi na kutumia muda mfupi baharini na kuwataka wavuvi wengine kujiunga katika ushirika ili waweze kupata misaada mbalimbali kutoka kwa wadau ikiwemo Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.