Habari za Punde

Kauli Mbiu ya Mbio za Mwenge Mwaka Huu. “Tehama ni msingi wa Taifa Endelevu ,itumie kwa usahihi na Uwajibikaji”

Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Maswala ya Ulemavu, Vijana, Sera na Uratibu wa Shughuli za Bunge Jenista Mhagama (kulia) akimkabidhi Kaimu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Lela Muhamed Mussa vitabu maalum vya mbio za Mwenge wa uhuru 2021 aweze kukata utepe ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa vitabu hivyo vitakavyomfikia kila mtu kupitia Ofisi za Wilaya hafla iliyofanyika Ukumbi wa Wizara ya Utalii na Mambo ya kale Kikwajuni Zanzibar.
Kaimu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Lela Muhamed Mussa akisoma taarifa maalum kwa vyombo vya habari juu ya suala zima la Uzinduzi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru unaotarajiwa kufanyika katika Uwanja wa Mwehe Makunduchui Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 17 Mei 2021 ambapo kauli mbiu ni “Tehama ni msingi wa Taifa Endelevu, itumie kwa usahihi na Uwajibikaji” hafla iliyofanyika Ukumbi wa Wizara ya Utalii na Mambo ya kale Kikwajuni Zanzibar.

Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Maswala ya Ulemavu Vijana, Sera na Uratibu wa Shughuli za Bunge Jenista Mhagama akitoa historia ya mwenge wa uhuru na kutolea ufafanuzi faida zinazopatikana katika mbio za Mwenge huko Ukumbi wa Wizara ya Utalii na Mambo ya kale Kikwajuni Zanzibar.

Viongozi mbalimbali wakiwa katika picha ya pamoja wakionyesha kitabu maalum chenye ratiba ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2021 ambazo zitazinduliwa Mkoa wa kusini Unguja Mwehe  tarehe 17 Mei 2021 na kilele cha mbio hizo kufanyika mkoani Geita tarehe 14 oktoba 2021,kauli mbiu kwa mwaka huu ni “Tehama ni msingi wa Taifa Endelevu ,itumie kwa usahihi na Uwajibikaji”
 

Na Khadija Khamis –Maelezo Zanzibar.

Mkuu wa Wilaya ya Kusini Unguja, Rashid Makame Shamsi, amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi kesho siku ya Jumatatu Mei 17 katika Uwanja wa Mwehe Makunduchi, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja.


Hayo aliyasema katika Uwanja huo wakati wa harakati za ukamilishaji wa Maandalizi ya upokeaji wa Mwenge wa Uhuru ambao unatarajiwa kuzinduliwa rasmin katika wilaya hiyo.  

 

Alisema katika ukimbizwaji wa Mwenge huo utazindua miradi mitatu ya maendeleo katika mkoa wa Kusini  Unguja ikiwemo mradi wa maji safi na Salama ambao utazinduliwa katika  shehia ya Mtende, uwekaji wa jiwe la msingi Ukumbi wa mitihani katika Skuli ya Jambiani, na kuweka jiwe la msingi katika mradi wa kijamii pamoja na  nyumba maalum inayohusiana na masuala ya maadili.

 

Hata hivyo alisema Uzinduzi wa Mwenge wa Uhuru utaufanya Mkoa wa Kusini kutambulika kimataifa na kupatikana fursa za uwekezaji kwa wageni ambao watafika hapo na kuvutika na hali halisi ya mazingira jambo ambalo litasaidia kukuza uchumi wa nchi

 

Kwa upande wa Mkuu wa Itifaki Fakih Kombo Faki amesema taratibu zote zimeshaandaliwa ikiwemo utaratibu wa usafiri ambao utawachukua wananchi wote wanatarajiwa kufika katika uwanja huo.

 

"Tumeweka gari katika vituo vyote ambavyo wananchi watakuwepo, pia kwa watu wenye mahitaji maalum nao wamezingatiwa kwa sababu hii ni tunu ya watu wote"alisema.

 

Nae Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kasini Abdul Aziz Hamad Ibrahim, wanafurahia Mwenge huo kuzinduliwa katika Mkoa wa Kusini kwa sababu ndiko alikotoka Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

 

Alisema wanatarajia wananchi wengi watahudhuria katika sherehe hizo wakiwemo wanachama wa vyama vyote vilivyopo nchini ,

 

Nao Wananchi wa Mkoa huo baadhi yao wamesema wamefarajika sana kupata tunu hiyo ambayo wamezowea kila mwaka kufanyika Dare es salam.

 

Walisema watahakikisha wanatoa ushirikiano kwa wageni na wenyeji wote ambao watafika wilaya ya Kusini.

 

Nae Kijana Asha Makame Ali alisema Mwenge huo umekuwa ukiwafungulia fursa mbali mbali ambapo mwaka 2001 walipata kufunguliwa soko kubwa la biashara maeneo ya Kitogani.

 

Mwenge wa Uhuru ni Chombo kilichoasisiwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1961, ikiwa ni tunu na ishara ya kuwepo kwa Taifa huru la Tanganyika ,

 

Kauli Mbiu ya mwaka huu ni “TEHAMA ni  msingi wa Taifa endelevu; itumie kwa usahihi na uwajibikaji ”

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.