Habari za Punde

Ukaguzi wa Visima vya Maji ya Kuzimia Moto (FIRE HYDRANT)

 

Maji yakiwa yakititirika katika kisima kilichopo katika eneo la Nyerere Square katikati ya Jiji la Dodoma wakati wa ziara ya ukaguzi wa Visima vya maji ya kuzimia moto iliofanyika leo 16 Julai, 2021 Chini ya Uongozi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kushirikiana na Ofisi ya Kamanda wa Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Dodoma.

KAMISHNA WA USALAMA DHIDI YA MOTO JESUALD IKONKO AKIZUNGUMZA NA BAADHI YA WAFANYABIASHARA KATIKA ENEO MAARUFU JIJINI DODOMA NYERERE SQUARE JUU YA UMUHIMU WA KUTUNZA VISIMA VYA MAJI YA KUZIMA MOTO MAPEMA.

Askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ZM 2869 CPL Kabuche Tengwa akitoa uchafu katika moja ya visima vya vya kuzimia moto vilivyofukiwa katika ukaguzi uliofanyika leo Jijini Dodoma.

Dodoma 16 Julai, 2021.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limefanya ukaguzi wa visima vya maji ya kuzima moto (Fire Hydrants) katika Jiji la Dodoma leo 16 Julai, 2021. Waliombatana katika ukaguzi huo ni Kamishna wa Utawala na Fedha Mbaraka Semwanza, Kamishna wa Usalama dhidi ya Moto Jesuald Ikonko, Mwenyeji wa Msafara huo ambaye ni Kamanda wa Zimamoto na Uokoaji (M) Dodoma Kamishna Msaidizi Mwandamizi, SACF Julishael Mfinanga pamoja na Maafisa na Askari kutoka Makao Makuu ya Zimamoto na Ofisi ya Kamanda wa Mkoa.

Ukaguzi huu umefanyika ili kujiridhisha na hali ya visima hivyo ambavyo husaidia wakati wa shughuli za uzimaji moto. Katika ukaguzi huo Viongozi hao waligundua mapungufu mbalimbali ikiwa ni pamoja na baadhi ya visima hivyo kufukiwa na uchafu kutokana na shughuli mbalimbali zinazoendelea katika maeneo husika na watu kutokuwa na uelewa wa kutosha juu ya umuhimu wake, vingine kutokuwa na maji kabisa kutokana na miundombinu chakavu.

Viongozi hao walitumia nafasi hiyo kuzungumza na wananchi wanaofanya shughuli zao jirani na visima hivyo ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha umuhimu wa kutunza visima hivyo. Akizungumza na baadhi ya wafanyabiashara katika eneo maarufu lijulikanalo kama Nyerere Square, Kamishna Ikonko aliwataka wafanyabiashara kuvitunza visima hivyo ili kuweza kusaidia pale ambapo uhitaji wa maji utatokea wakati wa zoezi la kuzima moto katika maeneo mbalimbali katikati ya Jiji la Dodoma.

 “Niwaombe wafanyabiashara katika eneo hili kuendelea kuvitunza visima hivi maana ndio sehemu tunayoweza kukimbilia kuchukua maji linapotokea janga la moto katikati ya Jiji letu la Dodoma” alisema Kamishna Ikonko.

Naye Kamishna Semwanza aliagiza ofisi ya Kamanda wa Mkoa kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa visima hivyo kila wakati ili kuondokana na changamoto ya Maji wakati wa matukio ya moto.

Ukaguzi huo ulifanyika katika maeneo mbalimbali ikiwemo Nyerere Square, Hospitali Kuu ya Jiji la Dodoma “Dodoma General Hospital”, Chuo cha Mtakatifu John pamoja na Area D.

(Picha zote na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji)

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.