Habari za Punde

Mhe Hemed Ametoa Siku Kumi Kuangamizwa au Kurejeshwa Bidhaa Zilizopita Muda wa Matumizi Yake.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akiwa katika ziara yake ya kushtukiza katika bandari ya Zanzibar leo na kutembelea maeneo mbali mbali katika bandari ya Malindi.
Muonekano wa Mchele wa ASHA KUKU uliongizwa Nchini Julai 11 mwaka na ARY Company ambao umepitwa na wakati na haufai kwa Matumizi ya Binadamu.
Muonekano wa Mafuta Lainishi (Oil) zilizoingizwa Nchini Mwaka 2019  bidhaa ambayo ilikwishapitwa na wakati na kukataliwa ya TBS.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akimuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari kuchukua hatua za haraka ndani ya Kipindi cha wiki moja kufanya marekebisho ya Miundombinu katika maeneo mbali mbali ya Bandari ya Malindi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akimuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari kuchukua hatua za haraka ndani ya Kipindi cha wiki moja kufanya marekebisho ya Miundombinu katika maeneo mbali mbali ya Bandari ya Malindi.

Na.Kassim Abdi. OMPR. 

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ametoa muda wa siku Kumi (10) kuangamiza au kurejesha zilipotoka bidhaa  zilizopitwa na wakati.

Mhe. Hemed alitoa agizo hilo wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika Bandari ya Malindi Jijini Zanzibar.

Katika ziara hiyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitembelea ghala lililohifadhiwa mafuta lainishi (Oil) ambayo yaliingizwa nchini mwaka 2019 kutokea Dubai na kukosa kiwango Kwa matumizi ya Vyombo vya Moto.

Alisema ni vyema kwa wizara kuhakikisha Zanzibar haipokei bidhaa zilizopitwa na wakati kwa usalama wa wananchi wake, Pamoja na kuitaka wizara ya Biashara na maendeleo ya Viwanda kuchukua hatua kali kwa wafanyabiashara wanoingiza Bidha zilizopitwa na wakati ili iwe fundisho kwa wafanyabiashara wengine.

“ Zanzibar sio sehemu ya kuja kutupa bidhaa zisizo salama, Naitaka Wizara ya biashara na maendeleo ya viwanda kuhakikisha wanachukua hatua kali kwa wahusika wanaoleta  bidhaa hizo kwa kufuata sheria na taratibu”  Alisema Makamu wa Pilin wa Rais

Katika ziara hiyo Mhe. Hemed alikagua mchele aina ya Asha Kuku ulioletwa na kampuni ya A.R.Y  ulioingia Zanzibar  July 11, mwaka huu na na mchele ulioletwa na I.A SIWJE TRADERS ulioingia Zanzibar  June 30 mwaka huu, ukiwa ni jumla ya kontena 10 sawa na tani Mia mbili na Sitini (260).

Mhe. Hemed Alitaka  mamlaka ya kuzuwia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar (ZAECA) kumaliza kesi ya mchele wa I.A SIWJI TRADER ambapo kampuni hiyo imeashiria kutenda vitendo vya uhujumu uchumi kwa kutoa rushwa  ili kuhalalisha bidhaa yake ilikwisha pitwa na muda.

Akitoa taarifa kuhusu bidhaa ya mafuta lainishi Kaimu Mkurugenzi Mamlaka ya Viwango Zanzibar (ZBS) Ndugu Muhamed Mwalim Simai alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa bidhaa hiyo ilikaguliwa na TBS na kukataliwa na hatimae muhusika huyo kuhamishia Zanzibar Bidhaa hiyo ambapo ZBS imeizuiwia kuingia sokoni.

Kwa Upande wake Mkuu wa Usajili na Tathmini ya Chakula kutoka ZFDA Ndugu Khadija Ali Sheha alimueleza Makamu wa Pili wa Rais kuwa  mchele uliongizwa Zanzibar kutoka Kampuni hizo umeshafanyiwa vipimo na kuonekana kupitwa na wakati sambamba na kugundulika kuwa haufai kwa matumizi ya binadamu ambapo Mamlaka yao  imetoa maelekezo kwa wahusiku kuweza kuchukua hatua zaidi.

Wakati huo huo, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitembelea Gati kuu ya Malindi na kutoridhishwa na mandhari ya eneo hilo kutokana na uchakavu wa Miundombinu.

Katika kulipatia ufumbuzi tatizo hilo la miundombinu Makamu wa Pili wa Rais amempa  muda wa wiki moja kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari kuhakikisha maeneo yote yalio na hitilafu kwa usalama wa wananchi yanafanyiwa marekebisho.

“Naomba mufahamu kuwa Bandari hii ndio uso wa Zanzibar yetu haifurahishi bandari yetu kuwa katika mandhari kama hii isioridhisha”. Alieleza Mhe. Hemed

Katika ziara yake Makamu wa Pili wa Rais alikagua eneo la kumpunzikia abiria, Ofisi ya Uhamiaji, Ofisi ya wakaguzi wa Afya na kutoridhishwa na Mazingira ya maeneo hayo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.