Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi Amewaapisha Viongozi Aliowateua Hivi Karibuni.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akimuapisha Mhe. Muumin Khamis Kombo kuwa Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, hafla hiyo ya uapisho imefanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 30-10-2021, na (kushoto kwa Rais) Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said.(Picha na Ikulu)

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi leo amewaapisha  watendaji mbali mbali aliowateuwa Oktoba 29, mwaka huu kushika nyadhifa zao  katika sekta ya Sheria.

Katika hafla hiyo ya kiapo  imefanyika Ikulu Jijini Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi amemuapisha Muumin Khamis Kombo kuwa Jaji wa Mahakama Kuu Zanzibar pamoja na Salma Ali Hassan kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar (DPP).

Aidha, amemuapisha Mwanamkaa Abdulrahman Mohammed kuwa Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar.

Katika hafla hiyo Viongozi mbali mbali wa Kitaifa walihudhuria, akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdalla, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dk. Talib Mwinyi Haji, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said, Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kaab pamoja na Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Wengine ni  Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Idrissa Kitwana Mustafa, Wakuu wa Vikosi vya  Ulinzi na Usalama, Watendaji wa Mahakama, Viongozi wa Kisiasa pamoja na wana familia.

Wakizungumza baada ya ya hafla hiyo,  watendaji hao wameahidi kushirikiana na watendaji wengine  wa Mahakama katika kuharakisha usikilizaji wa kesi ili wananchi waweze kupata haki zao kwa mujibu wa sheria.

Aidha, wamesema watashirikiana na jamii, Asasi zisizo za Kiserikali na zile  za Kiserikali ili kuhakikisha kunakuwepo mikakati na mifumo bora katika mapambano dhidi ya vitendo vya Udhalilishaji wa wanawake na watoto.   

Kitengo cha habari,

Ikulu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.