Habari za Punde

Maonesho ya Kimataifa ya Utalii Kufanyika Zanzibar Mwezi wa Febuari.2023

Na Khadija Khamis –Maelezo, Zanzibar.11/01/2023.

Maonyesho ya Kitaifa  ya Utalii na Uwekezaji , (Zanzibar  Tourism Investment and  Travel Exhibition –ZTITE ) yanatarajiwa  kuanza  - Tarehe  9 Hadi 11 Februari  katika Makumbusho ya Amani na ya Viumbe  hai  hapo Mnazimmoja 

 

Hayo yameelezwa na Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Utalii Hafsa Mbamba wakati akizungumza na waandishi wa habari huko katika Hoteli ya Emerson in Space Mji Mkongwe.

 

Amesema maonyesho hayo ni ya mara ya mwanzo kufanyika hapa Zanzibar ambayo yanatarajiwa kupokea wageni 200 kutoka nchi  mbali mbali .

 

Amesema lengo la kufanyika maonyesho hayo  katika eneo la makumbusho ni kuifanya  Sekta ya Utalii kwenda sambamba  na Mambo ya Kale kwa kuleta  maendeleo ya taifa na urithi wa vizazi vinavyo.

 

Aidha amesema kufanyika kwa Tamasha hilo  ambalo litasimamiwa na kamisheni ya utalii kutasaidia kutangaza maeneo ya kihistoria kitaifa na kimataifa ili wageni  wengi wapate  fursa ya  kutembelea maeneo hayo pamoja na kukuza mapato ya Taasisi na Serikali kiujumla.

 

Alifahamisha kuwa Zanzibar ina maeneo zaidi ya 86 ambayo yameainishwa na  kutangazwa kupitia gazeti la Serikali hivyo ni  fursa  pekee ya kutangazwa maeneo hayo kupitia maonyesho.

 

Katibu huyo alisema  kuwa kufanyika kwa maonyesho hayo yatasaidia kutangaza fursa za uwekezaji zinazopatikana Zanzibar jambo ambalo litaimarisha sekta ya utalii na sekta mbali mbali.

 

Alieleza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea kuwakaribisha wawekezaji katika sekta mbali mbali ikiwemo Utalii,Kilimo,Makaazi Afya na nyenginezo kwa ajili ya kuimarisha maendeleo ya Zanzibar.

 

Hata hivyo amesema Serikali imekusudia kuongeza idadi ya Matamasha  au maonyesho jambo ambalo litasaidia kuitangaza Zanzibar kuifanya kuwa maarufu zaidi kitaifa na kimataifa na kueweka vyema kiutalii katika ramani ya dunia hasa katika nchi za Falme za Kiarabu na Asia .

 

Nae Mkurugenzi wa Idara ya Makumbusho na  Mambo ya Kale Mariamu  Mohamed  Mansab amesema maonyesho hayo yanayotarajiwa kufanyika katika makumbusho yatakuwa  ya kimataifa na kibiashara zaidi tofauti na maonyesho mengine hayo yatakuwa na utaratibu maalum ya kuingia ili kutoa fursa nzuri kwa washiriki wa ndani na nje ya nchi .

 

Amesema kutakuwa na kujisajili kwa washiriki wa maonyesho hayo ambao washiriki watajisajili  kwa njia ya mtandao na kutakuwepo na viingilio katika maonyesho hayo  .

 

Alieleza kuwa kuwapatia wageni fursa ya kutembelea katika sehemu za vivutio kutasaidia kujitangaza  wakati watakaporudi katika nchi zao watakuwa mabalozi wa kuitangaza Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.