Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Akabidhiwa Ripoti ya Sensa ya Watu na Makaazi ya Mwaka 2022 Ikulu Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akipokea Ripoti ya Sensa ya watu na Makaazi ya mwaka 2022 kutoka kwa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo.05/05 2023.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Mipango Zanzibar Mhe.Dkt.Saada Mkuya Salum (kushoto kwa Rais) akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Sensa ya watu na Makaazi mbele ya  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (katikati) wa kukabidhi Taarifa hiyo leo katika Ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar (kushoto)  Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (kulia) aliokuwa akizungumza na Ujumbe wa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman wa Pili kulia) mara baada ya kupokea Ripoti ya Sensa ya watu na Makaazi ya mwaka 2022  katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo. 05/05 2023. 

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema inajukumu kubwa la kuzifanyia kazi takwimu za Sensa ya watu na makaazi ya mwaka 2022, ili kujipanga na utekelezaji wa mipango ya maendeleo, kiuchumi na kijamii.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipopokea ripoti ya Kamati ya Sensa ya watu na makaazi iliyofanyika mwaka jana.

Rais Dk. Mwinyi alisema sensa hiyo imetoa mambo mengi ambayo lazima yafanyiwe kazi kabla ya kukamilika kwa mpango wa Maendeleo 2025 - 2050 kuelekea mwisho wa Dira ya Maendeleo ambako mwaka 2030 alieleza Zanzibar itakadiriwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya watu.

Alisema ripoti hiyo na nyengine zitakazofuata lazima zitafutiwe namna nzuri ya kufanyiwa kazi kwa undani ili serikali ijipange katika masuala mazima ya maendeleo ya nchi.

“Ripoti kama hii na nyengine zitakazokuja lazima tutafute namna nzuri ya kujipanga jinsi ya kuzifanyia kazi kwa undani ili serikali iweze kujipanga sasa kwa masuala mazima ya maendeleo ya nchi kwa kipindi cha muda mfupi, muda wakati na mrefu” alifafanua Rais, Dk. Mwinyi.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi aliipongeza Kamati ya ushauri wa sensa Kitaifa kwa kazi nzuri waliyoikamilisha.

“Tulidhani tukishapata idadi ya watu na makazi basi kazi imekwisha, kumbe bado kuna kazi kubwa yakufanya, kwa kweli mnaendelea kuifanya kwa ufanisi mkubwa” Rais Dk. Mwinyi aliipongeza kamati hiyo.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdullah aliwaahidi Rais Dk. Mwinyi na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan kwamba kamati yao ya ushauri wa sensa Kitaifa, itajitahidi kuendeleza sehemu ndogo iliyobaki ili kulikamilkisha kwa vitendo zoezi hilo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambae pia ni Mwenyekiti Mwenza wa Kamati hiyo, aliwashuruku Rais Dk. Mwinyi na Rais Samia kwa kuiamini kamati hiyo katika kukamilisha zoezi zima la sensa kitaifa.

Naye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Mipango, Dk. Saada Mkuya Salum, alisema matokeo ya sensa yanadhihirisha wazi kwamba ifikapo mwaka 2025 wakati wa kuhitimisha Dira ya Maendeleo ya Tanzania, Zanzibar pekee itakua na idadi ya watu wapatao milioni mbili na elfu nane na dunia itakapohitimisha maendeleo endelevu mwaka 2030, Zanzibar inakadiriwa kuwa na idadi ya watu wasiopungua 2,440,000 na mwaka 2050 Zanzibar inakisiwa kuwa na idadi ya watu wasiopungua 4,630,000.

Dk. Mkuya alieleza kwa mujibu wa viashiria hivyo vya idadi kubwa ya watu wa Zanzibar kwa wakati huo, Serikali haina budi kuangalia upya sera ya idadi ya watu nchini pamoja na kuzifanyia mabadiliko sera nyengine ili ziendane na mabadiliko ya kiuchumi na jamii kwa wakati husika.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.