Habari za Punde

Dk.Hussein Amesifu Mafanikio Makubwa ya Hati Safi Zilizowasilishwa kwa Serikali, Kufuatia Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar, (CAG)

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia katika viwanja vya Ikulu Jijini Zanzibar ,baada ya kukabidhiwa Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (CAG), hafla hiyo iliyofanyika katika leo 13-5-2024
 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesifu mafanikio makubwa ya hati safi zilizowasilishwa kwa serikali, kufuatia taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar, (CAG) na kuzitaka taasisi na Mashirika ya Umma zenye hati zzilizo na dosari kujitathmini na kuzifanyia kazi ili mapungufu yasiendelee kujirejea.

Rais Dk. Mwinyi ameyaeleza hayo alipozungumza kwenye viwanja vya Ikulu, Zanzibar baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar, (CAG), Dk. Othman Abbas Ali.

Alisema, pamoja na mapungufu na changamoto zinazohitaji kushughulikiwa kwa kuchukuliwa hatua mbalimbali ili kufaya vizuri zaidi siku za usoni, alisifu hati za ukaguzi safi kwa serikali, kwa kufikia kiwango cha asilimia 95.4 na kueleza kuwa ni mafanikio makubwa kwa Serikali.

Akizungumzia mapungufu yaliyojitokeza kwenye ripoti hiyo, Rais Dk. Mwinyi alieleza baadhi yao ni ya kiutawala na mengine ya kiutendaji yanayohitaji ufumbuzi wa kiutawala.

Hivyo, amemuagiza Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi, Mhandisi Zena Ahmeid Said kuunda Kamati maalumu itakayoshughulikia kasoro hizo ili kuzifanyia kazi.

Alisema, sio kila kasoro zilizomo kwenye Ripoti ya CAG ni za kijinai, nyengine zipo za Kiutendaji zinahitaji ufumbuzi wa Serikali na zile za kijinai zitakabidhiwa kwa Mamlaka ya Kudhibiti na Kuhujumu Uchumi, Zanzibar (ZAECA) kwa hatua za kisheria.

Dk. Mwinyi, alizionya baadhi ya taasisi za Serikali kuingia kwenye mikataba ya utekelezaji wa miradi ya Serikali bila kuishirikisha Ofisi ya Mwanashiria Mkuu wa Serikali jambo alilolieleza kuwa ni kosa kisheria.

Hata hivyo, aliwataka viongozi wa Serikali wa ngazi zote, kuendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Zanzibar panapokua na wajibu wa kufanya hiyo.

Mapema, akiwasilisha ripoti yake, CAG Dk. Othman Abbas Ali, aliishauri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa na mifumo michache itakayodhibiti siri za serikali pamoja na mapato ya serikali yasipotee.

Akizungumzia kasoro za baadfhi ya Mashirika ya Umma na kampuni zinazoendelea kujiendesha kwa hasara kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo, Dk. Abass alisema mashirika hayo huathiri mitaji ya Serikali iliyoekezwa pamoja na kuwa na mitaji hasi hali inayosababisha taasisi hizo kutegemea mikopo na ruzuku kutoka serikalini kwajili ya kujiendesha na kushindwa kulipa gawio kwa serikali.

Dk. Abass, pia alieleza ukaguzi huo ulibaini kasoro kwa mashirika na kampuni hizo kutokuwa na ufanisi wa utoa huduma na hayaendani na malengo na mkakkati yaliyojiwekea kwa ushindani na taasisi nyengine binafsi.

Akiyataja Mashirika na kampuni hizo Dk. Abass alisema ni pamoja na Shirika la Magazeti ya Serikali ya Zanzibar (SMS), Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC), Kampuni ya Maendeleo ya Uvuvi, Kampuni ya mafuta na Kampuni ya ujenzi Zanzibar.

Aidha, aliishauri Serikali kuwa na mashirika machache yenye uwezo wa kujiendesha wenyewe na kutoa gawio kwa Serikali.

Akizungumzia ukaguzi wa awali wa mafao ya kiinua mgongo na pesheni, Dk. Abass alieleza ripoti hiyo ilibaini asilimia 28 ya upotevu wa fedha za Umma zilizokokotolewa kwa mafao ya mishahara ya watumishi waliokwishastaafu.

Alisema kasoro hizo zilijitokea baada ya mfumo wa “Payroll” kushindwa kuzuia utaratibu wa ugawaji wa mishahara hiyo na kuendelea kuitia hasara Serikali kwa upotevu wa fedha za Umma kwa baadhi ya watumishi hao kushindwa kuwekewa kizuizi cha mishahara na kuendelea kupokea mishahara wakati tayari walishahtaafu, miongoni mwa dosari hizo Dk. Abbasi alisema zilitokea kwa Wizara ya Afya, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Chuo cha Mafunzo, Kikosi cha cha Kuzuia Magendo KMKM, Kikosi cha Zimamoto na uokozi pamoja na Wizara Nchi Tawala za Mikoa na Vikosi Maalum vya SMZ..

Hivyo, CAG, aliishauri serikali kuwana mifumo michache itakayokuwa na tija kwao kuliko kuwa na mifumo mengi inayoitia hasara serikali sambamba na kuacha kubuni mifumo mipya isiyokuwa na uwezo wa utatuzi wa changamoto za kimifumo juu ya changamoto za serikali.

Jumla ya ripoti nane zilikabidhiwa Serikali ikiwemo ya Serikali Kuu (Mawizara na taasisi zote).

Kifungu cha 112 (5) kinamtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali CAG, awasilishe taarifa yote aliyoikagua na aikabidhi kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa hatua nyengine na baadae Rais Dk. Mwinyi alimkabidhi Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora, Haroun Ali Suleiman ambae nae ataikabidhi kwa Baraza la Wawakilishi kwa mujibu wa takwa la kikatiba kwaajili ya kujadiliwa.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.