RAMBIRAMBI KUFUATIA KUZAMA KWA MELI YA MV SPICE ISLANDERS KUTOKA KWA WATANZANIA WANAOSOMA NA KUISHI WALES, UK
Sisi Watanzania tunaosoma na kuishi Wales, UK tumepokea kwa masikitiko makubwa habari za kuzama kwa meli ya MV Spice Islanders iliyokuwa safarini kuelekea kisiwani Pemba na kusababisha zaidi ya wananchi 200 kupoteza maisha na wengine zaidi ya 600 kujeruhiwa katika ajali hiyo mbaya na kubwa kutokea katika historia ya visiwa vya Zanzibar.
Tunaungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein na Watanzania wenzetu duniani kote katika kipindi hiki kigumu cha msiba na maombolezo.
Tunachukua nafasi hii kuwapa pole wafiwa na kuwaombea uvumilivu hasa kwa kuondokewa na wapenzi wao katika kipindi hiki kigumu ambacho walikuwa wakiwahitajia sana. Mwenyezi Mungu awape moyo wa subira.
Aidha, tunawaombea dua majeruhi na wote walionusurika katika ajali hiyo mbaya na kumuomba zaidi Mwenyezi Mungu awajaalie wapone haraka na waungane na familia zao katika ujenzi wa mustakbali bora wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
Tunatanguliza shukrani zetu za dhati kwa vyombo mbali mbali vilivyoshiriki kwa njia moja ama nyengine katika jitihada za kusaidia kuokoa maisha katika janga hili kubwa la Taifa.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu awalaze marehemu mahali pema peponi, AMIN
No comments:
Post a Comment