Na
Abdi Shamnah
SERIKALI
ya Oman imesema iko tayari kutekeleza makubaliano yote yaliofikiwa kati ya nchi
hiyo na Zanzibar katika nyanja mbali mbali, zikiwemo za habari,
utamaduni,utalii na michezo, kama hatua ya kuendeleza uhusiano uliopo kati ya
nchi mbili hizo.
Hayo
yameelezwa na Balozi mdogo wa Oman aliopo Zanzibar, Mansour Al Busaid, wakati
alipokuwa na mazungumzo na Waziri wa Habari,Utamaduni,Utalii na Michezo, Said
Ali Mbarouk ofisini kwake Mnazi Mmoja.
Viongozi
hao walipata nafasi ya kuzipitia kumbu kumbu za makubaliano ‘memorundum of
understanding’ ziliosainiwa Augost, 17,2010 baina ya iliokuwa Wizara ya Elimu
na Mafunzo ya Amali Zanzibar na Wizara ya Urithi na Utamaduni ya Oman, pamoja
na kuangalia maeneo mengine ambapo zinaweza kushirikiana.
Balozi
Mansour alisema kuna mambo mengi ya kushirikiana katika nyanja za sanaa na
utamaduni kupitia katika maonyesho mbali mbali pamoja na ile ya kubadilishana
vitabu vitakavyoonyesha maingiliano yaliokuwepo kati ay watu wa nchi hizi.
Alisema
Oman inakususdia kuangalia ni aina gani ya vifaa vilivyo mashuhuri ambavyo
vilipata kutumika hapo zamani na sasa vimepotea katika makumbusho ili kuvileta
nchini na kusaidia katika juhudi za kukuza utalii.
Alishauri kuwepo utaratibu wa kushirikiana na
kubadilishana uzoefu kwa wasanii (wanamuziki) wa Zanzibar ili wapate fursa ya kwenda Oman sambamba na wale wa Oman
kuja nchini.
Balozi
huyo alimhakikishia Waziri Mbarouk kuwa nchi yake ina wataalamu wazuri katika
masuala ya uhifadhi wa nyaraka, hvyo iko tayari kuisaidia Zanzibar ili kuona
nyaraka zote muhimu zinatunzwa kwa faida ya baadae.
Mapema
Waziri Mbarouk alimweleza Balozi huyo kuwa Zanzibar imedhamiria kuendeleza ushirikiano wa
muda mrefu na wenzao wa Oman, na kuiomba
nchi hiyo kuangalia uwezekano wa kusaidia matengenezo katika majengo ya
Makumbusho ambayo yako katika hali mbaya, huku baadhi ya nyaraka zikiwa
zimeshaharibika.
Aidha
aliiomba Oman kusaidia matengenezo ya magofu mbali mbali ili kulinda historia
zake , kutoa nafasi za masomo kwa Wazanzibari pamoja na kupata fursa ya
kujifunza jinsi nchi hiyo ilivyopata maendeleo makubwa ya kiutalii bila kuathiri
utamaduni wake.
Vile
vile aliiomba nchi hiyo kusaidia upatikanaji wa mafunzo kwa mafundi wa Shirika
la Utangazaji (ZBC –TV) sambamba na haja yakubadilishana vipindi kati ya kituo
hicho cha Televisheni na ile ya Taifa nchini Oman.
Nae
Mkurugenzi wa Makumbusho na Mambo ya Kale, Dk. Amina Ameir, alitilia shime
matengenzo ya majengo ya Beit el Ajaib, Kasri la Mfalme pamoja na Kaburi na
kuelezea umuhimu mkubwa wa kuyanusuru kabla uharaibifu haijawa mkubwa zaidi.
Pia
aliiomba nchi hiyo kusaidia juhudi za Idara yake za kuanzisha kitengo cha
Marine Achiology Unit, kwa kukipatia vifaa vya kutendea kazi pamoja na taaluma
kwa wafanyakazi wake.
Dk.
Amina aliomba kupatiwa fursa za mafunzo kwa wafanyakazi wa Idara hiyo, ili
kufanikisha malengo ya kufungua
makumbusho zaidi katika Mikoa ya Unguja na Pemba, na kuweka bayana uhaba wa
wafanyakazi wenye taaluma ya kutosha unaoikabili Idara yake.
Akizungumza
katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Ali Saleh Mwinyikai,
alisema mambo yaliokubaliwa katika ‘Memorundum’ hiyo ni makubwa sana lakini
bado ukubwa wake haujaonekana na kushauri kuteremshwa katika ngazi za watendaji
kwa utekelezaji kutoka ngazi za Mawaziri ilipo sasa.
No comments:
Post a Comment