Habari za Punde

Tamko la Shirika la Kazi Duniani Kanda ya Afrika Mashariki na Rwanda


TAMKO LA SHIRIKA LA KAZI DUNIANI KANDA YA AFRIKA MASHARIKI NA RWANDA ILIYOTOLEWA NA BI FATMA M. RASHID KWA NIABA YA
MKURUGENZI WA SHIRIKA LA KAZI DUNIANI
KANDA YA AFRIKA MASHARIKI NA RWANDA
BW. ALEXIO MUSINDO MEI DAY, 2012
BWAWANI HOTEL.

Leo, Shirika la Kazi Duniani linaungana na Serikali, waajiri na wafanyakazi na vyama vyao, kusherehekea Siku ya Wafanyakazi Duniani. Kwa niaba ya Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani Kanda ya Afrika Mashariki na Rwanda, bw. Alexio Musindo ninayo heshima kuwaletea salamu za Shirika kwa ajili ya siku hii muhimu – siku ya kutafakari kuhusu haki za msingi mahala pa kazi na majadiliano ya kijamii ambayo yanalenga kuhusu uhuru na utu wa binadamu; pia kama zana za kuzidisha uzalishaji na maendeleo linganifu.

Wafanyakazi ni kitovu cha ustawi wa Jamii. Wafanyakazi ni kichocheo muhimu cha mikakati ya  maendeleo na nafasi yao inahitaji kutambuliwa katika maeneo kama ujira, mazingira na masharti ya kazi. Hii husaidia sana katika kuhimiza maendeleo ya kijamii na kiuchumi, kuwaimarisha wafanyakazi wenyewe, familia zao na jamii kiujumla.


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kazi Duniani Ndugu. Juan Somavia katika salamu zake za Siku ya Mei Mosi mwaka huu ameeleza kuwa, “…Kufanya kazi kinadhifu na kwa bidii ndio chanzo cha heshima kwa binadamu, uimarishaji wa familia, kuleta amani katika jamii na pia ni chanzo cha kuaminika kwa uongozi wa kidemokrasia…Katika maeneo mengi ulimwenguni tumepoteza mtazamo wa msingi kuwa kazi sio bidhaa”.

Mgogoro wa kiuchumi na kifedha duniani umeathiri kwa haraka sana uchumi halisi duniani na kuzidisha tatizo la ukosefu wa ajira kwa kuwaacha watu zaidi ya milioni 200 bila ajira duniani, ikiwa ni pamoja na karibu vijana milioni 80, wengi wakiwa wanaishi kwa kiasi cha Dola za Kimarekani 1.25 tu kwa siku. 

Kama mchango wa kushughulikia changamoto hizi, Shirika la Kazi Duniani limeuteua ‘ Mwezi Machi 2012’, kama  ‘Mwezi wa Ajira kwa Vijana’ na limeamua kuwa mada ya  “Tatizo la Ajira kwa Vijana” kuwa moja ya ajenda kuu za Kikao cha 101 cha Mkutano Mkuu wa mwaka wa Shirika la Kazi Duniani mnamo Juni mwaka huu huko Geneva.

Kwa malengo hayohayo, mkutano wa kitaifa unaohusu ajira kwa vijana uliitishwa jijini Dar es Salaam hivi karibuni ili kujadili ajenda ya ajira za staha kwa vijana nchini na kubadilishana mawazo kuhusu yale mazuri yaliyokwishafanyika. Zanzibar nayo ilishiriki katika mkutano huo. Katika mkutano huo tumeshuhudia juhudi  mbalimbali zilizokwishachukuliwa kujumuisha masuala ya ajira katika mikakati ya maendeleo ya kitaifa, yaani (MKUKUTA) na (MKUZA).

Ili kusonga mbele, Shirika la Kazi Duniani linaonelea kuwa ulimwengu unahitaji kubadili muundo wa sasa wa ukuaji kiuchumi duniani kwani  muundo uliopo umejenga ukwasi mkubwa ulioenea katika mikono michache. Muundo huu umeshindwa kuandaa aina ya ukuaji jumuishi tuliotegemea.

Shirika linapendekeza aina nyingine ya ukuaji kiuchumi ambao unajali mazingira na kulenga mahitaji ya watu, yaani  muundo ambao lengo lake kuu ni kuongeza ustawi wa watu hivyo kupima mafanikio kutokana na idadi ya ajira na sio asilimia ya ukuaji wa jumla wa Pato la Taifa (GDP).

Hivyo tunahitaji kuchukua hatua kadhaa kuhakikisha kuwa tunaelekea katika enzi mpya ya haki ya kijamii (new era of social justice) kama namna ya kusonga mbele katika kushughulikia baadhi ya masuala niliyokwisha yaeleza kabla na baadhi yake ni:

·         Kuhakikisha kuwa malengo ya kuandaa nafasi za ajira yanakuwa kipengele muhimu cha sera ya uchumi mpana (Microeconomic policy) pamoja na kupunguza mfumuko wa bei, pia kuchochea uwekezaji na kuhimiza uwekezaji katika biashara ndogondogo, sekta zinazotoa nafasi nyingi za ajira, masoko jumuishi ya ajira na ukuzaji wa ujuzi wa aina mbalimbali.

·         Kutambua kuwa haki za msingi kazini na majadiliano ya kijamii ambayo ni sehemu ya uhuru na heshima ya kibinadamu pia ni kama zana ya kuzidisha uzalishaji, tija na maendeleo linganifu.

Ili haya yafanikiwe na kulenga kwenye kuwa na kazi zenye staha, ni muhimu kuimarisha suala la majadiliano ya kijamii na lile la utatu. Shirika la Kazi Duniani limeendelea kufanya kazi na asasi mbalimbali za masuala ya kazi kwa kipindi cha miezi 12 iliyopita kupitia mradi wake wa kuboresha uelewa na matumizi ya sheria za kazi ili kuongeza ufahamu kati ya waajiri na wafanyakazi kuhusu wajibu na haki zao za msingi kazini, kwa kuzingatia sheria za kazi nchini. Kazi iliyofanyika imepelekea kuongezeka kwa uwajibikaji katika mifumo ya uongozi kazini hasa katika utekelezaji wa sheria za kazi. Yafuatayo ni baadhi tu ya mafanikio:

·         Kusaidia kuchapishwa kwa vipeperushi vinavyohusu kitengo cha usuluhishi wa migogoro ya kazi
·         Kusaidia mafunzo ya darasani na kivitendo kwa wakaguzi kazi pamoja na kuifanyia majaribio tool, checklist iliyotengenezwa kutokana na mafunzo yaliyopita nyuma.
·         Kutoa mafunzo kwa maafisa kazi na bodi ya kazi ya ushauri juu ya sheria za kazi, mijadala ya pamoja, utatu na mikataba ya shirika la kazi duniani.
·         Mafunzo ya usuluhishi wa migogoro ya kazi kwa kitengo cha usuluhishi wa migogoro.
·         Kuanzishwa kwa database ya masjala ya kitengo cha usuluhishi wa migogoro ya kazi.
·         Kusaidia kitengo cha usuluhishi wa migogoro kuunganishwa na kitengo cha usuluhishi migogoro ya kazi cha huko bara na kupata mafunzo kivitendo kwa wiki mbili.
·         Kitengo cha usuluhishi wa migogoro na mahakama ya kazi kupatiwa vifaa vya ofisi kama komputa na saver kwa ajili ya kurahisinsha utekelezaji wa kazi za kila siku.
·         Kusaidia kuanzishwa kwa kitengo cha usuluhishi wa migogoro ya kikazi.
·         Kusaidia mahakama ya kazi kuhifadhi maamuzi ya kesi za kazi kwa njia ya kompyuta.
·         Kusaidia mkutano wa utatu wa viongozi na wadau wetu ambao unakutanisha viongozi wa Wizara ya Kazi, Jumuiya ya Waajiri na Wafanyakazi wa Zanzibar na wa Tanzania bara kuzungumzia juu ya masuala ya kazi.

Ni matumaini yetu makubwa kuwa shughuli hizi zitachangia katika kuimarisha majadiliano ya kijamii na kuboresha uhusiano na ushirikiano mahala pa kazi.

Kama wengi tunavyofahamu tayari, viwango vipya vya kazi vya kimataifa kwa moja ya vikundi vya wafanyakazi vilivyo katika mazingira hatarishi kwenye uchumi usio rasmi yaani – “kazi zenye staha kwa wafanyakazi wa ndani” vilipitishwa wakati wa Mkutano Mkuu wa Shirika la Kazi Duniani wa 100, yaani Mkataba Na. 189, na pendekezo Na. 201 (2011). Napenda kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali ya Tanzania hasa Zanzibar na washirika wetu ambao ni jumuiya ya wafanyakazi na waajiri kwa juhudi zao walizofanya kuhakikisha viwango hivyo vinapitishwa na kwa juhudi ambazo tayari zinaendelea kufanyika kama maandalizi ya kuridhia mkataba huo.

Kwa mara nyingine, napenda kukuhakikishia ndugu mgeni rasmi nia na  utayari wa Umoja wa Mataifa kwa ujumla, kupitia Mpango wake wa Msaada wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDAP), na Shirika la Kazi Duniani kusaidia shughuli zinazolenga kuimarisha majadiliano ya kijamii miongoni mwa wadau wote kama njia ya kukuza kazi zenye staha kwa wote.


Ahsanteni Sana!

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.