Habari za Punde

Zanzibar yazindua sera ya utawala bora


Na Hafsa Golo 
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Haji Omar Kheri, amesema sera mpya ya Utawala Bora ni miongoni mwa mchakato utakaohakikisha shughuli za serikali zinafuata misingi ya katiba, utawala wa sheria na kuimarisha maadili.

Waziri huyo alieleza hayo jana katika ukumbi wa hoteli ya Bwawani mjini hapa, kwenye hafla fupi ya uzinduzi wa sera ya utawala bora, ambayo ilihudhuriwa na watendaji wa ngazi mbali mbali serikalini na asasi za kiraia.


Waziri huyo alisema moja ya faida ya kuwepo kwa sera hiyo ni kutoa muongozo juu ya mgawanyo wa madaraka katika utekelezaji wa majukumu ya serikali, kufuatwa kwa maadili pamoja na utamaduni wa utayarishwaji wa watendaji na viongozi wa kuchaguliwa.

Alisema awali misingi ya utawala bora ilikuwa haijumuishwi katika sera za kitaifa, hivyo kuzinduliwa kwa sera hiyo ni miongoni mwa mikakati ya kuifuata misingi hiyo kivitendo.

Alifahamisha kuwa miongoni mwa malengo ya kuwepo sera hiyo kutaisaidia jamii kutekeleza majukumu kwa kufuata misingi ya utawala bora, hali itakayosukuma mipango ya kufikiwa kwa maendeleo.

"Wizara yangu itahakikisha inafuatilia tathmini ya utekelezaji wa sera hiyo, na kutoa taarifa kila mwaka ya utawala bora, taarifa hiyo itakuwa ya wazi na itaonesha maeneo yaliyofanya vizuri pamoja na kuonesha changamoto zilizopo ili tuweze kutafuta njia za kuzishughulikia changamoto hizo", alisema.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa wizara hiyo Joseph Meza, alisema kuwa itaimarishwa mikakati ya utekelezaji wa sera hiyo na kwamba misingi ya sheria zilizowekwa nchini inafuatwa.

Meza alisema sera hiyo mpya itakuwa dira na chombo muhimu cha kufanyia tathmini na kutoa muelekezo juu ya namna utawala bora unavyotekelezwa nchini.

Alisema wakati wa utayarishwaji wa sera hiyo, juhudi zilichukuliwa katika kuwashirikisha wadau ili kuhakikisha michango yao inapatikana, ambapo michango hiyo ilikuwa chachu ya kukamilika kwa sera hiyo.

Katibu huyo alisema imerahisishwa kila madau kuisoma sera hiyo kwani imeandaliwa kwa lugha za kiingereza na Kiswahili pamoja na kuwepo kwa nukta nundu ambazo zinawawezesha watu wasioona kuweza kuisoma.

Kwa upande wa Mwakilishi wa watu wasioona Fatma Djaa Chesa, aliiomba serikali kutoa elimu kwa wizara husika ili iweze kuzingatia umuhimu wao wa kuelewa mambo muhimu yanafanyika katika serikali yao kwa kuwachapishia maandishi ya nukta nundu na kuwafikishia sehemu walipo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.