Habari za Punde

Lowasa ajisogeza klabu za habari


Na Rose Chapewa, Morogoro
WAZIRI Mkuu (mstaafu), Edward Lowasa ataongoza shughuli za uzinduzi wa mfuko  wa jamii pamoja na tovuti ya chama cha waandishi wa habari mkoa wa Morogoro (MOROPC) wakati wa sherehe ya kuuaga mwaka 2012 na kuukaribisha 2013.

Hayo yalibainishwa na Mwenyekiti wa muda wa klabu hiyo,Boniventure Mtalimbo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za chama hicho, na kwamba uzinduzi huo utafanyika Januari 19 mwaka huu katika hoteli ya kitalii ya   Nashera mjini Morogoro.

Alisema  lengo la kuanzishwa mfuko wa jamii ni kuwawezesha waandishi wahabari kwenda vijijini kwa ajili ya kuandika habari kutokana na maeneo hayo kushindwa kufikika kwa urahisi kutokana na ukosefu wa fedha.


Mtalimbo alisema mbali na waandishi kwenda vijijini pia utakuwa ukisaidia mambo mbalimbali ikiwemo maafa, kama vile vifo, magonjwa na kuwawezesha kujiendeleza kielimu.

Akizungumzia uzinduzi wa tovuti, alisema waandishi wa habari mkoani Morogoro watakuwa wakiandika makala mbalimbali zikiwemo za kuelimisha jamii,na kuandaa vipindi vya televisheni na redio na kuingiza kwenye tovuti hiyo.

 Aidha Mwenyekiti huyo aliwaomba wadau mbalimbali ndani na nje ya mkoa wa Morogoro, kujitokeza kuchangia kwa hali na mali mfuko huo ili kuwawezesha waandishi hao kufanya kazi kwa ufanisi zaidi pamoja na kuibua mambo mbalimbali yaliyojificha hususani vijijini.

Aliwataja wadhamini waliojitokeza hadi sasa kuwa ni Hoteli ya Nashera, Benki ya CRDB, Mamlaka ya Mapato Tanzania,Kampuni ya Umeme ya Mac Dolnad Live line, Kampuni ya Abood, Mbunge wa Jimbo la Morogoro mjini, Mamlaka ya Maji safi na taka mkoa wa Morogoro (MORUWASA).

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.