Na waandishi wetu
MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif
Sharif Hamad amelaani vikali kitendo cha kupigwa risasi na kuuliwa Padre Evaristus
Mushi wa kanisa katoliki Zanzibar.
Alisema
kitendo hicho kimevuruga sifa njema ya Zanzibar
ya kuwa kisiwa cha amani.
Maalim
Seif ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CUF ametoa kauli hiyo kisiwani Pemba wakati akifungua semina ya madiwani wa CUF
inayofanyika ukumbi wa kiwanda cha mafuta ya makonyo Wawi.
Alisema
kwa niaba yake binafsi, chama chake na serikali analaani vikali kitendo hicho
cha kinyama ambacho kimeitia doa kubwa Zanzibar.
Alisema
kitendo hicho ambacho hakikubaliki ni cha kusikitisha kwa vile Wazanzibari
wamekuwa wakiishi kwa kuvuliana kwa kipindi kirefu bila ya kutokea vitendo
hivyo.
Alisema
ni wajibu wa Wazanzibari kuendeleza sifa njema ya Zanzibar
kwa kuhakikisha wananchi wanaendelea kuishi kwa kuvumiliana na kuwapa matumaini
wageni wanaokuja kuitembelea Zanzibar
kwa shughuli mbali mbali ikiwemo ya utalii.
Ameviomba
vyombo vya dola kufanya kazi ya ziada kuwatafuta waliohusika na tukio hilo na kuchukuliwa hatua
za kisheria.
Hata
hivyo, alisema wakati uchunguzi huo ukiendelea kufanyika, ni vyema kwa vyombo
vya dola kufanya kazi kwa umakini mkubwa ili kuepuka kuwahusisha watu
wasiohusika na tukio hilo.
Amekiri
kuwa kitendo hicho ni kikubwa na kibaya, lakini hakijafikia hatua ya kuitangaza
Zanzibar kuwa nchi ya kigaidi, na kwamba kufanya hivyo ni kuijengea sifa mbaya Zanzibar na kuwafukuza watalii ambao ndio tegemeo la
uchumi wa Zanzibar.
Wakati
huo huo Maalim Seif amesema ni lazima maamuzi ya madiwani yaheshimiwe na
watendaji wengine katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu yao.
Alisema
madiwani ndio wafanya maamuzi katika serikali ya mitaa, hivyo maamuzi yao yaheshimiwe na
watendaji ili kujenga mustakbali mwema katika kuwatumikia wananchi.
Alifahamisha
kuwa tatizo lililopo sasa ni kuwa mfumo uliopo unatoa mamlaka makubwa kwa
watendaji, hasa makatibu wa Halmashauri na Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa.
Alisema
wakati serikali imo katika mchakato wa kuleta mageuzi katika serikali za Mitaa Zanzibar, ni vyema
mageuzi hayo yakarekebisha hali isiyoridhisha iliyopo sasa.
Alitoa
wito kwa Madiwani kuchapa kazi kwa bidii
na kuhakikisha wanayafahamu, kuyasimamia na kuyatekeleza ipasavyo majukumu
waliyokabidhiwa.
Aidha
Maalim Seif amewasihi Madiwani wa CUF kutokubali kuburuzwa na watendaji, na
kuhakikisha kuwa maamuzi yao
katika Mabaraza na Halmashauri yanaheshimiwa na kutekelezwa kwa ukamilifu.
“Endapo
Katibu au Mtendaji hafuati maagizo ya Madiwani na anafanya atakavyo, lazima
mumuarifu Waziri anayehusika, na kama Waziri atapuuza wasilisheni ripoti kwa
Makamu wa Pili wa Rais,” alisema.
Alifahamisha
kuwa ili malengo ya utekelezaji yaweze kufikiwa ni vyema kwa Madiwani kufanya
kazi bega kwa bega na watendaji wengine wakiwemo wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi, Wabunge na Masheha, kwa vile kazi na maeneo yao ya kazi yanalingana.
Jumla
ya madiwani 83 wa CUF kutoka Pemba na Unguja
wanashiriki semina hiyo ya siku 6 ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji
inayofadhiliwa na Taasisi ya Friedrich Naumann Foundation (FNF) ya Ujerumani.
Wakati
huo huo Marekani imelaani vikali mauaji ya Padrid Evaristus Mushi yaliyofanywa
na watu wasiojulikana juzi katika eneo la Beit el Ras mjini Zanzibar.
Taarifa
iliyotolewa na Balozi wa Marekani nchiNI Tanzania kwa vyombo vya habari
imesema mauaji hayo yanakwenda kinyume na utamaduni wa amani uliodumu katika
visiwa hivyo kwa muda mrefu.
Ubalozi
huo umesema Zanzibar
imekuwa makaazi ya makabila mengi
kutokana uvumilivu na kuheshimiana
walionao wananchi wake.
Taarifa
hiyo ilisema vurugu za kidini hazina nafasi nchini Tanzania na popote pale
duniani na kuwataka wananchi wa Zanzibar
na Tanzania kukataa vitendo vya chuki vinavyosambazwa na watu wachache ambao wana lengo la kuvuruga amani, usalama
na haiba ya Tanzania.
Marekani
imesema iko tayari kuusaidia mfumo wa sheria nchini Tanzania na kutoa wito
kwa wote waliohusika na mauaji ya Padri huyo kukamatwa, kushtakiwa na kuhukumiwa kutokana na uhalifu waliotenda
kwa viongozi wa dini.
Imewaomba
wananchi wa Zanzibar na Tanzania kujenga ustaarabu wa kuvumiliana, busara,
umoja na amani.
Kwa upande
wake Jumuiya ya Maimamu Zanzibar (JUMAZA) imelaani vikali kitendo cha mauaji ya
Padri Mushi wa Kanisa Katoliki na kusema kitendo hicho si cha kibinaadamu bali
ni cha kinyama.
Aidha
Jumuiya hiyo ilieleza kushitushwa na kusikitishwa kwake kwa tukio hilo la
kikatili na kusema kitendo hicho cha kiharamia kinaashiria kuitia doa Zanzibar
ambayo kwa muda mrefu watu wake wamekuwa
wakiishi kwa amani na ukarimu mkubwa.
Taarifa
kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na Katibu wa Jumuiya hiyo, Muhiddin Zubeir
Muhiddin ilisema kuwa Maimamu wanaungana na kauli ya Rais wa Jamuhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kwa maagizo yake kwa jeshi la
Polisi nchini kufanya uchunguzi wa haraka ili kubaini wahusika wa tukio hilo.
Aidha
imeliomba jeshi la polisi kufanya uchunguzi wa uadulifu usioambatana na
shindikizo la mtu ama kikundi chochote ili kutambua ukweli bila ya kuwadhuru
wasiohusika.
Hata
hivyo, JUMAZA iliwataka waumini wa madhehebu yote nchini kuendeleza amani na
utulivu na kuwataka kutotoa mwanya kwa watu ama vikundi ambavyo vina nia mbaya
ya kutaka kuleta vurugu na kutoelewana kwa wananchi kwa malengo yao binafsi.
Jumuiya
hiyo imevitahadharisha vyombo vya habari
vinavyohusisha tukio la kuuawa Padri Mushi na uislamu na kusema kitendo hicho kinaweza kupandikiza
chuki na uhasama katika jamii, hatimae kupandikiza mizizi ya fitna na
kulisababishia taifa kuingia kwenye machafuko.
Habari
hii imeandikwa na Hassan Hamad, OMKR na waandishi wetu
No comments:
Post a Comment