Habari za Punde

Watumia mti kupimia uzito watoto

Na Fatina Mathias, Dodoma
WAKAZI wa kata ya Mnadani manispaa ya Dodoma, wamelazimika kutumia mti wa ofisi ya Ofisa Mtendaji kata hiyo, kama kliniki ya kuwapimia watoto uzito kutokana na  kukosekana zahanati.

Hayo yalibainishwa jana na Diwani wa kata hiyo,Steven Masangia,alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Alikiri wakazi hao kukabiliwa na changamoto hiyo na kufafanua kuwa tayari eneo la kujenga zahanati  limepatikana.

Alisema eneo hilo ni kubwa lenye uwezo wa kujengwa hata kituo kikubwa cha afya lakini bado fedha hazijapatikana kutekeleza mradi huo.

"Kata yangu haina zahanati,tunatumia pale ofisi ya kata kuna mti ambao mzani unatundikwa na watoto wanapimwa uzito," alisema.

Aliiomba serikali kuchangia ujenzi wa zahanati hiyo itakayogharimu  shilingi milioni 126 ili kwa sababu kina mama wanapata shida.

"Wananchi wangu wamejitahidi kuchangia kwa hali na mali mpaka sasa tumeweza kufikia hatua ya kumwaga jamvi chini, walileta fedha,kokoto,mchanga na vitu vingine mpaka tumefikia hatua hii,” alisema.

Aidha alisema halmashauri imekubali kuchangia shilingi milioni 20, lakini hata hivyo bado fedha zinazohitajia ni nyingi.


Akizungumzia maendeleo ya kata hiyo, Diwani huyo aliwaasa wananchi kutoiachia serikali ifanye kila kitu bali washiriki katika kuleta maendeleo yao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.