Habari za Punde

Warsha ya siku 3 ya kujadili utungaji wa Mtaala wa Epistemolojia ya Kiislamu


Na Abdulla Ali Maelezo-Zanzibar                                 17/04/2015

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi na Utumishi wa Umma Zanzibar Mhe. Haroun Ali Suleiman amesema ipo haja kwa wasomi wa kiislamu kuchukua juhudi za makusudi katika kuunga mkono harakati za uanzishwaji wa Mtaala wa Epistemolojia ya Kiislamu kwani ndio mfumo pekee utakaowawezesha vijana hao kwenda sambamba na mabadiliko yanayoendelea kutokea kila siku Duniani.

 

Ameyasema hayo wakati akifungua Warsha ya siku 3 ya kujadili utungaji wa Mtaala wa Epistemolojia ya Kiislamu wa masomo ya Vyuo Vikuu uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Kumbumbu ya Abdurahman Al-Sumait kilichopo Chukwani, Zanzibar.

 

Amesema Dini ya Kiislamu ni neema kutoka Allah ambayo hutofautisha moja kwa moja kati ya binadamu na viumbe vyengine, hivyo ni wajibu wa kila muislamu kuthibitisha hilo kwa kuelewa Nyanja zote za uislamu zilizofungamana na Quran na Sunna ambavyo ndio misingi mikuu ya Epistemolojia ya Kiislamu.

 

Waziri Haroun amesisitiza kuwa katika kuendeleza vilivyo mtaala utakaojikita katika misingi ya Epistemolojia ya Kiislamu ipo haja kwa waislamu wenyewe kujifunza na kuelewa kiundani zaidi mafunzo ya Quran na Sunna za Mtume (S.A.W) kwani kuna utofauti mkubwa kati ya Epistemolojia ya Kiislamu na Epistemolojia nyengine ambazo hujumuisha mafundisho ya vitabu vitakatifu pamoja na mawazo ya watu lakini uislamu unatoa elimu zaidi ya hiyo.

 

Ametanabahisha kuwa kwa sasa vyuo vingi ulimwenguni hata katika Nchi za Kiislamu vimetawaliwa na mtaala usio wa kiislamu jambo ambalo hupelekea kuzalisha wataalamu ambao wanakuwa kimatiriali zaidi na wasio na hofu juu ya kumuogopa Mungu na wanaofanya mambo kwa kuangalia matashi yao binafsi.

 

Nae Makamo Mkuu wa Chuo cha Kumbumbu ya Abdurahman Al-Sumait Prof. Hamed Rashid Hikmany amesema Warsha hiyo ina lengo la kujadili mambo tofauti yakiwemo; hatua za mchakato wa kuoanisha, hatua za kutunga mtaala unaozingatia maeneo makuu ya kujifunza yakiwemo ufahamu, stadi za mazoezi, namna ya kutatua matatizo na stadi za sayansi, mawasiliano, uongozi, stadi za pamoja, menejimenti ya taarifa stadi na majukumu ya kijamii pamoja na taaluma na kanuni na stratejia za uhakiki.

 

Amesema zaidi ya wataalamu 40 wakiwemo wa Vyuo Vikuu, Maprofesa na Watafiti kutokea Vyuo Vikuu 9 vya Nchi za Afrika mashariki na Chuo Kikuu 1 cha Malaysia wamekutana Zanzibar kwa ajili ya Warsha hiyo ya siku 3 ambayo imeanza tarehe 17-19 Aprili, 2015 kwa ajili ya kutunga Mtaala wa masomo ya vyuo vikuu unaoendana na mabadiliko mbali mbali ya dunia yanayojitokeza hivi sasa.

 

Prof. Hikmany amefahamisha kuwa Warsha hiyo imeandaliwa na Taasisi ya Kimataifa ya Fikra ya Kiislamu inayoitwa International Institute of Islamic Thought (IIIT) yenye makao makuu yake nchini Malaysia kwa kushirikiana na Chuo chake, vikiwemo vyuo vikuu tofauti vinavyoshiriki ambavyo ni; Chuo Kikuu cha Waislamu Morogoro (Tanzania), Chuo Kikuu cha Umma (Kenya), Chuo Kikuu cha Moi (Kenya), Chuo Kikuu cha Zanzibar, Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Uganda, Chuo Kikuu cha Musa Bin Bique (Msumbiji), Mradi wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Sudan ya Kusini na Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Malaysia.  

 

 

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.