MWENYEKITI
wa ushirika ‘’Nia njema’ wa wasioona uliopo Mtambile Mkoani Pemba, Ali Hemed
Khalifa, akimuuzia moja kati ya wateja wao Shemsia Khamis Zubeir, zulia lililotengenezwa
kwa usumba, ambapo zulia moja ni shilingi 15,000/= (picha na mpiga picha wetu, Pemba)
MWENYEKITI
wa ushirika wa ‘Nia njema’ wa wasioona uliopo Mtambile Mkoani Pemba, Ali Hemed
Khalifa, akiwa na wanaushirika wenzake ambao wanajishughulisha na utengenezaji
wa mazulia na madometi yanayotokana na usumba, wakiwa katika kazi hiyo huko
Mtambile, ambapo Dometi moja huuzwa shilingi 18,000/= na zulia ni shilingi
15,000/= hadi shilingi 15,000/= (picha
na mpiga picha wetu, Pemba)
‘’SISI macho yetu ni vidole, na ndio vinavyotulisha siku zote...’’,
Ni
neno la mwanzo la Mwenyekiti wa ushirika huo wa wasioona wa ‘’Nia njema’’uliopo
Mtambile Mkoani Pemba, Ali Hemed Khalifa.
Nikiwa
na Mwenyekiti wa ushirika huo na wanachama wake wawili, sikupata picha kamili,
kuwaona wasioona wakitengeneza Madometi na Mazulia.
Macho
juu na wakati mwengine akielekeza kichwa na sehemu ya kiwili wili chake upande
mwengine, lakini mkono wao wenye vidole kumi, ndio macho ya kuzipanga kamba za
usumba.
Hapo
ni mazungumzo kwenda mbele, huku wao wakiendesha kazi zao za kushona bidhaa
hizo zinazotokana na usumba, na kisha mkono wao kwenda kinywani.
Jamani
Muungu haachi mjawe, aso hili ana lile, lakini nikasema hupati kile ukakosa mwendo,,,,,,,niliyasema
haya kwenye moyo wangu huku machozi ya furaha yakimwagika.
Kalamu
yangu ya kuandikia makala hii, wakati mwengine nilikuwa nikiisahau, kutokana na
umahiri na ujuzi wa hali ya juu, uliokuwa ukifanywa na wanushirika huo.
Ali
Hemed Khalifa, ndie Mwenyekiti na
ndie muanzilishi wa ushirika huo wa wasioona, ambae yeye alionekana kuwa na
mengi yanayohusu ushirika wao pamoja na wasioona wanavyoweza kuleta mabadiliko.
Alinihadithia
kuwa ushirika wao, ambao haujapatapo ufadhili ulianza rasmi mwaka 2001, kwa
mafunzo ya awali yaliofanyika Unguja juu ya kutengeneza mazulia na madometi ya
usumba.
Ali
Hemed alienda huko kama yeye na kurudi ndioa akaona kumbe hakuna mlemavu
anaeshindwa na kijio chake kama atapata mafunzo kutokana na mazingira yake.
‘Kumbe
mlemvu kuwa omba omba si jambo la lazima kama wanavyofanya wengine, bali kama
atafundishwa na kuweza kuyatala mazingira yake anaweza kujiletea
maendeleo’’,alisema huku akiendelea na kazi ya kutengeneza dometi.
Baada
ya yeye kufanyaka kazi hiyo akiwa peke yake, ndipo alipoaanza safari ya kusaka
wasioona wenzake mmoja baada ya mwengine kwa kila eneo analoishi mwanachama wa
Jumuia ya Wasioona Zanzibar Wilaya ya Mkoani (ZANAB).
‘’Unamuona
huyo mwanachama wangu Mkasi, alikuwa hajawahi kutoka nje tokea azaliwe, na
nipofika kwa wazazi wake shughuli ilikuwepo maana walikuwa hawataki kumtoa’’, alisema.
Juhudi
kubwa ilifanyika, hadi mwanachama huyo kuweza kuingia kwenye ushirika huu, na
wazazi wake kuridhia ingawa kwa hapo awali ni kwa ushingo upande.
Mwaka
2004, kwa mujibu Mwenyekiti huyo alisema sasa ushirika huo ukatimia ukiwa na
wanachama sita wote wakiwa wasioona, ingawa baadhi yao wenye uoni hafifu na
wengine kiza kabisa.
‘’Sitaisahau
semina moja ya TASAF, ambayo hii ndio hasa iliotutoa sisi na ushirika huu,
kutambulika maana kama kawaida yangu niliyachukua Madomet na Mazulia na
yakanunuliwa huko’’,alifafanua.
Miaka
nenda, miaka rudi ushirika huo ambao ulikumbwa na changamoto kadhaa kuliko
faida, uliendelea kwa kuchangishana fedha, na kujinunulia malighafi ya usumba.
Mwaka
2010, hapo pia wanachama hao sita walichangishana fedha tena kila mmoja
shilingi 5,000/=, ingawa baadhi yao walikuwa wagumu kutoa wakidhani wanataka
kuibiwa.
‘’Wengine
walikuwa wangumu kutoa fedha, maana si unajua dunia imejaa wajanja na hata wao
walikuwa wagumu ,lakini baadae walikubali na kupata fedha za kununulia
malighafi’’, alisema huku akiendelea kutengeneza Dometi.
Mwenyekiti
huyo alizidi kunipa maajabu kuwa, katika ushirika wao, wanatengeneza mazulia na
madometi ya aina mbili kuu, ikiwa ni pamoja na madogo na makubwa.
Dometi
moja kutokana na nafasi yao baada ya kukamilisha vifaa vyote hulitengeneza kati
ya siku mbili hadi tatu, ambapo moja huliuza kati ya shilingi 18,000/= na
shilingi 15,000/=.
Mwenyekiti
huyo alilalamikia kutupwa na Serikali licha ya kuwepo kwa Idara maaluma ya watu
wenye ulemavu, wakiwemo wao wasioona katika kijiji hicho cha Mtambile.
‘’Tulikuwa
tukipigiwa kelele wee,,,, anzisheni vikundi ,,,,,,anzisheni sacos lakini tokea
siku tulioanzisha hadi leo, hatujapatiwa uafadhili wowote tupo tu kingu nguvu’nguvu’,alieleza
kwa masikitiko.
Pamoja
na uhaba wa mtaji, lakini kwa sasa tayari wanachama wote wa ushirika huo,
wameshapata uelewa wa kutengeneza madometi na mazulia ambapo pia hujipatia
fedha ndogo ndogo ya sabuni.
Mkasi,
vipi kuhusu hali ya kipato, ukilinganisha na wakati wote ulipokuwa umewekwa
ndani na wazazi,,,, nilimuuliza mwanachama huyo na kusema ‘’hamna hamna ndio
muliwamo.
Mkasi
ambae alikuwa amewekwa ndani kwa muda wa miaka zaidi ya 20, na wazazi hadi hapo
alipokwenda Mwenyekiti wake, kwa sasa anajisikia faraja.
‘’Mimi
nilijua kutokana na ulemavu wangu wa uoni, siwezi kufanya lolote, lakini kwa
sasa naweza kufanya makubwa, maana hata sabuni yangu hainipigi chenga’’,alisema
wakati akitengeneza zulia.
Mwanachama
huyo wa ushirika wa ‘Nia njema’ uliopo Mtambile, alitamka kuwa huu sio wakati
wa walemavu kuwekwa ndani, na badala yake watolewe nje ili wafanyekazi.
Baada
ya kufika ndani ya ushirika huo, pia ameweza kujiari mwenyewe, kwa kuanzisha
mpango wa kujishonea mikoba, makawa na mikeka jambo ambalo hapo awali
hakulitarajia.
‘’Kwa
kweli ushirika huu, umeniwezesha kuyatawala mazingira yangu, na hata kujidai
kwa kupata walau sabuni yangu, na hata kusaidia wenzangu, lakini nayo Serikali
ituone’’,alisema.
Nae
mwanachama Riziki Juma Omar, alisema kama iwapo ushirika wao utasaidiwa na
wafadhili unaweza kupiga hatua, na wasiiona katika ukanda huo wa Mtambile
kuondokana na utegemezi.
Kubwa
zaidi wanachama wa ushirika huo pomoja na kulilia mtaji, lakini pia wamepaza
sauti zao juu, kutaka kupatiwa mafunzo zaidi ya kazi yao hiyo ili waingie
katika soko la ushindani.
Mwenyekiti
wa ushiriki huo Ali Hemed Khalifa, alirudi tena na kusema suala la soko sio
tatizo kubwa sana, hasa baada ya ujio wa soko la Jumapili, lakini changamoto
kubwa kwa sasa ni malighafi.
‘Utaamini
kuwa baadhi ya siku inanibidi mimi nisafiri hadi Bumbwini au Kakazini Pemba,
kuyafuata makumbi au kamba, sasa angaalia safari hizo kisha uliuze shilingi
ngapi zulia ili upate faida’’,alisema.
‘’Soka
la jumapili lipo, lakini ugumu wetu kwa sasa ni upatikanaji wa malighafi
(makumbi), yamekuwa adimu na mali, sasa na hata ukiamua kununua kamba ni ghali
mno’’,alifafanua.
Ushirika
huo wa utengenezaji wa Madometi na Mazulia ya kamba za umba una malengo kadhaa,
ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya wanachama wasioona.
Hata
hivyo wanachama hao wametoa wito kwa wazazi na walezi, kuacha tabia ya
kuwafungia ndani watu wenye ulemavu, kwani wakiwezeshwa kwa mujibu mazingira
yao wanaweza kuleta mabadiliko.
Pia
wakaikumbusha Serikali kuhakikisha wanawatupia macho, ili uweze kujikongoja na
kufikia malengo yaliojipangia, ikiwa ni pamoja na kukuza pato lao.
Ushirika
huu ambao hadi sasa, haujafanya usajili rasmi, unajiendesha kwa nguvu za
wanachama na wamekuwa na utaribu wa kugawana shilingi 20,000/- baada ya kuuza
mazulia na fedha nyengine kununua maliaghafi.
Idara
ya watu wenye ulemavu, Umoja wa Watu wenye ulemavu na Jumuia ya wasioona
Zanzibar, hapa ndio pakuanzia kwa kuvipa mitaji vikundi kama hivi ili visonge mbele.
Thanks
ReplyDelete