Habari za Punde

Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu katika michezo


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Pemba                                                    10.09.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amekagua matengenezo makubwa ya kuwekwa mpira wa kukimbilia (Tatan) katika uwanja wa Gombani Pemba na kupongeza hatua iliyofikiwa ambayo itazidi kuimarisha sekta ya michezo hapa nchini.


Dk. Shein alifika kiwanjani hapo akiwa ameongozana na viongozi mbali mbali wa Serikali akiwa na mwenyeji wake Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Rashid Ali Juma ambaye alimpa maelezo ya kina juu ya maendeleo ya matengenezo hayo makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Katika ukaguzi wake huo, Dk. Shein  alisema kuwa kukamilika kwa uwekaji huo wa Tatan katika uwanja huo wa Gombani Pemba kutauwezesha mchezo wa riadha kufanyika kwa ustadi mkubwa zaidi sambamba na kuufanya uwanja huo uwe umekamilika kimichezo hatua ambayo itaendeleza kuibua vipaji vya mchezo huo hapa nchini.

Alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na juhudi za kuimarisha na kuongeza miundombinu ya michezo katika maeneo yote yaliotengwa maalum kwa michezo katika visiwa vya Unguja na Pemba ili kuirejesha Zanzibar katika asili yake kwenye anga ya michezo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi wa Wizara hiyo kuhakikisha eneo lote lililozunguka uwanja huo linakuwa salama na halivamiwi kwa ujenzi usio rasmi.

Nae Waziri wa Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Rashid Ali Juma  alimueleza Dk. Shein maendeleo yaliofikiwa katika matengenezo ya tatan katika uwanja huo wa Gombani pamoja na hatua nyengine zinazoendelea kuchukuliwa ili uwanja huo uzidi kuvutia kimataifa.

Aidha, Waziri Juma alieleza kuwa hatua iliyofikiwa katika matengenezo hayo ni nzuri na kumuhakikishia Dk. Shein kuwa juhudi zaidi zinaendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha baadhi ya maeneo ya uwanja huo yanafanyiwa ukarabati awamu kwa awamu yakiwemo maeneo ya majukwa ili uzidi kuimarika na kuvuti zaidi.

Matengenezo ya uwekaji wa tatan hizo  yalioanza mwaka 2013 yalifanyika kwa awamu tatu ambapo awamu ya kwanza na ya pili ilifanywa na Kampuni ya Nowe Investment kutoka Dar-es-Salaam na awamu ya pili ya uwekaji wa tatan ilifanywa na Kampuni ya Guangzhou Jrace Athletic kutoka China.

Tatan hiyo iliyozungushwa katika kiwanja hicho mbali ya kuwekwa katika sehemu maalum kwa kukimbilia pia imeongezwa kwa baadhi ya maeneo katika kiwanja hicho ambayo yatawezesha baadhi ya michezo kuweza kuchezwa katika kiwanja hicho ukiwemo mchezo wa vinyoya na michezo mengineyo.

Hata hivyo, uwanja huo wa Gombani tayari umeshawekewa nyasi za bandia ambazo tayari zimeshaanza kutumika kwa kuchezewa mashindano mbali mbali ya mpira wa miguu yanayofanyika kisiwani Pemba.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.