Habari za Punde

ZJCBF yajitolea kuwapa vifaa waandishi, watangazaji Zanzibar

Na Haji Nassor, Pemba
TAASISI ya Kuwajengea Uwezo Waandishi wa Habari Zanzibar ‘ZJCBF’ ni asasi ya kiraia ya kitaaluma ya uandishi na utangazaji wa habari Zanzibar.

Kama zilivyo nyengine, nayo taasisi hii iliyoanzishwa kwa mujibu wa kifungu cha 20, cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na chini ya sheria namba 6 ya mwaka 1995, inayoruhusu kuanzishwa kwa asasi za kiraia Zanzibar.

Ni taasisi isiyolenga kupata faida binafsi, na imebuniwa na wanataaluma na wanamaarifa wa masuala ya uandishi na utangazaji wa habari visiwani humo .

Taasisi hii ilisajiliwa mapema Julai 13, mwaka 2014 na kupewa namba ya usajili 2292 na Mrajisi Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Hivyo kwa sasa Zanzibar kuna jumla ya tasisi 11, za kitaaluma katika masuala ya uandishi na utangazaji wa habari, ambazo zimesajiliwa kama asasi za kiraia.

Kwa mfano lipo Baraza la Habari Tanzania MCT- Zanzibar, ipo pia ‘Zanzibar Editors Forum ‘ZEF’, Chama cha waandishi wa Habari wanawake Tanzania TAMWA- Zanzibar, Klabu ya waandishi wa Habari Zanzibar ZPC, Klabu ya wanahabari Pemba, ‘PPC’, Jumuia ya waandishi wa Habari za Maendeleo WAHAMAZA.

Taasisi hii ya Kuwajengea Uwezo waandishi wa habari na watangazaji wa habari, kama vile imekuja na kitu kipya ambacho, waandishi wa habari wenyewe kimewafurahisha.

Kwa mujibu wa Mkurungenzi wa ZJCBF, Juma Khamis Juma aliwathibitishia waandishi hao kwenye mkutano uliofanana kama wa uzinduzi, uliofanyika mjini Unguja, kwamba watapatiwa vifaa.
Wakati akieleza hayo, waandishi waliohudhuria kwenye hafla hiyo, walikumbwa na mshangao wa furaha, juu ya malengo ya taasisi hiyo kwao.

Maana mtangaazaji Khadij Kombo Khamis wa ZBC redio Pemba, alionekana kama aliepatwa na kitetemishi cha kauli, juu ya taasisi hiyo kuwaahidi kuwapatia vifaa.

“Jamani mimi kama sijafahamu, Mkurugenzi unasema kwamba baada ya kupewa mafunzo, mnamalengo ya kutupatia na vifaa…?’’,alihoji mtangaazaji huyo.

Mtangaazaji Jazaa Kombo wa kituo cha redio cha Hits fm, alionekana kukazia nati neno la mtangaazaji mwenzake, kwamba, lazima kwenye hili ukweli uwepo.

Anasema sio sahihi kwa taasisi hiyo, kupanga mipango na mikakati madhubuti ya kuwaendeleza wanahabari kivifaa, kisha kuingia mitini.

“Maana zipo taasisi zinazofanana na ZJCBF, huahidi mambo mazuri kwa makundi husika, kisha kutetereka na ahadi kuwa hewa, sasa na hili lifanyike kweli’’,alifafanua.

Hapo Mwenyekiti Mtendaji wa taasisi hiyo Rajab Khamis Rajab, alilazimika kutuliza mizuka ya waandishi na kuwaahidi kuwa wameshajipanga.

Anasema hilo limo kwenye mipango na mikakati yao, ilikuhakikisha waandishi wa habari Zanzibar, bila ya kujali vyombo wanavyotoka wanapatiwa vifaa.

Taasisi inakusudia baada ya kuwapatia mafunzo, kuwakata kiu ya kuwapatia vitendea kazi kama vile vinasa sauti, kamera na hata kompyuta.

Wakati akifafanua hilo, mwandishi Salum Vuia Issa wa Idara ya Habari Maelezo, yeye alitaka atolewe tena hofu juu ya taasisi hiyo kuwapatia vifaa waandishi.

Vuia haamini sana kwenye nafsi yake, kutokana na Zanzibar kuanzishwa kwa jumuia kadhaa, zikiwa na katiba zenye malengo mazuri, kisha wakati wa utekelezaji mambo kwenda ndivyo sivyo.

“Mimi kwanza napongeza hatua ya kujipanga kutupatia vifaa, lakini lazima ukweli uwepo katika hili, ili kuepusha ahadi hewa kama wanavyofanya wengine’’,alitahadharisha.

Punde Mkurugenzi Mtendaji wa ZJCBF Juma Khamis Juma, alisimama wima, akawataka waandishi wawaamini na kuwapa msaada wa ushirikiano, ili taasisi hiyo ipate mafanikio.

“Hii ni taasisi nyengine na ya kupigiwa mfano, ni tofauti na hizo nyangine, sasa kama tukishirikiana basi malengo ya taasisi yenu yatafikiwa’’,alifafanua.

Alisisitiza kila kitu kina simama kikiwa na miguu, na kwamba kwa taasisi yao, miguu yake ni wanachama ambao ni waandishi wa habari, watangaazaji na hata wamiliki wa mitandao ya kijamii.
Awali taasisi hii inakusudia kuwajengea uwezo waandishi wa habari, kwa njia ya mafunzo kwa kujumuisha midia chapishi (magazeti na vitabu), midia-tangazi (redio na runinga) na midia-mtandao (kurasa za tovuti na blogu).

Hili la kuwawezesha waandishi wa habari kwenye taasisi hii, limeshatajwa litakuwa la kwanza, kisha ndio wakabidhiwe vifaa kwa ajili ya kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Wapo waandishi wa habari na watangazaji Zanzibar, ambao wameonekana kusubiri kwa hamu matunda ya taasisi hiyo, na hasa suala la kusaidiwa vifaa.

Maana mwandishi na mtangaazaji wa redio Jamii Micheweni Pemba Time Khamis Mwinyi, anaona kukosekana kwa vitendea kazi, wakati mwengine hurejesha nyuma kazi zao.

Anasema kwenye redio yao mashine za vinasa sauti na komputa huwa ni shida unapohitaji kwa ajili ya kufanyia kazi, sasa anaamini ZJCBF kama ikiwapatia watakuwa imara.

Kubwa aliuukumbusha uongozi wa taasisi hiyo, wakati wa ugawaji, wasije wakasauiliwa waandishi walioko kisiwa cha Pemba, na kuishia Unguja pekee.

Kauli kama hiyo, ilielezwa na mtangaazaji Said Suleiman wa redio Adhana fm, akisema hasa ukosefu wa vitendea kazi ndio changamoto inayokabili, sasa lazima usawa uwepo.

“Mimi naona mafunzo huwa tunapata kila baada ya muda, lakini suala la vifaa ndio shida kubwa kwetu, sasa taasisi kama imeshajipanga na hilo twaikaribisha’’,alifafanua.

Mwandishi mkongwe Mussa Haji Foum anaeandikia shirika la habari la X-inhua la China, anasema suala la vifaa vya kazi kwa waandishi wa nchi nyengine sio changamoto tena.

“Sasa na sisi Zanzibar kwa muda mrefu, tunalilia hili la ukosefu wa vitendea kazi, sasa kama ZJCBF imedhamiria hilo, naipongeza mikono miwili’’,alifafafanua.

Ameona ni aibu kwa waandishi wa habari kunasa sauti au kupiga picha kwa kutumia simu za mkononi, jambo ambalo halileti taswira nzuri.

Ndio hilo ambalo Mwenyekiti mtendaji Rajab Khamis Rajab, alidakiza na kusema taasisi yao haiji kwa mfumo wa zima moto kama baadhi ya wengine wanavyofikiria.

“Unajua sisi leo ndio kama tunazindua taasisi hii baada ya kupata ufadhili kupitia Mfuko wa wanawake Tanzania ‘WFT’, lakini tumejipanga na tumedhamiria kweli’’,alijigamba.

Anachoomba kwa wanahabari wa Zanzibar ni kuiunga mkono taasisi hiyo na kushiriki katika vikao kadhaa pale watakapowaita, ili kujenga umoja kwa kweli.

Aliwatoa hofu waandishi hao wa habari kuwa, kutokana na wafadhili ambao wamashawadokeza juu ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo, hana shaka.

Vifaa kama vinasa sauti, kamera na hata kompyuta aliahidi kuwa vitapatikana bila ya shaka yoyote, kwa waandishi, wamiliki wa mitando ya kijamii na watangaazaji.

Wakati taasisi hii ya kuwajengea uwezo waandishi na watangaazaji habari Zanzibar, ZJCBF ikijiwekea mikakati ya kuwapatia vifaa waandishi na watangaazaji, imeanza kukabiliwa na changamoto kadhaa.

Moja na kubwa ni ukosfu wa rasilimali watu, ingawa Mkurugenzi mtendaji Juma Khamis Juma, anasema hilo karibu litakaa sawa kwa kuajiri.

Maana kipindi cha mwaka mmoja ujao kutoka sasa, itaajiri wafanyakazi watatu, wawili wakiwa wanawake, sambamba na kupanga bajeti yao, ambayo itatatua baadhi ya changamoto.
Taasisi hii mpya pia, kwa sasa haijakuwa na ofisi yake rasmi, ingawa inakusudia kupangisha jengo eneo la karibu na Posta mkuu mjini Zanzibar.

Mei 18, mwaka huu, taasisi hiii baada ya kukutana na waandishi wa habari zaidi ya 35 kutoka kisiwa cha Unguja na Pemba, kwenye ukumbi wa Umoja wa watu wenye ulemavu Unguja, imewahakikishia itakuwa bega kwa bega.

Ndio maana kwa kuanzia, tayari idadi hiyo ya waandishi wa habari na watangaazaji, wameshapewa elimu ya namna ya kuandika au kutengeneza vipindi juu ya wanawake.

Uongozi wa ZJCBF umetamka kuwa, sasa kazi ya kuwakomboa wanahabari, wamiliki wa mitandao na watangaazaji Zanzibar imefika, na kwao ni kuhakikisha wanaungwa mkono.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.