Habari za Punde

Mama Mwanamwema Shein, Awataka Viongozi wa UWT na Kimama Kushirikiana na Serikali Yao Kujiletea Maendeleo.

Na Rajan Mkasaba.
MKE wa Rais wa  Zanzibar Mama Mwanamwema Shein amewataka akinamama pamoja na viongozi na wanachama wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT), kushirikiana na Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na taasisi husika katika vita dhidi ya ukatili na udhalilishaji wa watoto na wanawake.

Mama Shein aliyasema hayo leo kwa nyakati tofauti wakati akizungumza na akinamama, viongozi na wanachama wa (UWT) wa Wilaya ya Dimani na Wilaya ya Mfenesini Kichama kwa lengo la kuwasalimia na kuwashukuru kwa kuendelea kuiunga mkono CCM, ikiwa ni muendelezo wa ziara zake kwa mikoa yote ya Zanzibar.

Katika maelezo yake Mama Shein alisema kuwa inasikitisha sana kuona kuwa miongoni mwa jamii wapo watu ambao wanajitoa mishipa ya ufahamu na kuwadhalilisha watoto kwa kuwafanyia vitendo viovu.

Aliwataka viongozi hao pamoja na akinamama kusimama imara na kupiga vita kwa nguvu zao zote vitendo vya aina hiyo na kuwataka kuungana katika kuvikomesha kwa vile ni kinyume cha ubinaadamu, kinyumme cha mafundisho ya Mwenyezi Mungu na pia, ni vitendo vinavyoiabisha jamii ya Kizanzibari.

Hivyo, Mama Shein aliwasisitiza viongozi hao,akinamama na wanajumuiya ya UWT kwa kila mmoja awe askari kwa kuwaripoti, wanaohusika katika vyombo vya sheria, ili wachukuliwe hatua zinazostahiki.

Mama Shein alieleza kuwa jitihada za Serikali katika kuleta maendeleo, haziwezi kufanikiwa iwapo hali ya amani, umoja na mshikamano vitaondoka.

Alisema kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika hotuba zake amekuwa akikumbusha umuhimu wa kuitunza amani iliyopo na kuitaka jamii kuijiepusha na vitendo vyote vinavyoweza kuharibu amani na utulivu wa nchi.

Hivyo, Mama Shein kwa upande wake alisisitiza umuhimu wa kuiendeleza amani, na kuwaaasa vijana kutojiingiza katika vitendo vinavyoweza kuharibu amani.

Akitoa nasaha zake juu ya matumizi ya mitandao ya kijamii, Mama Shein alisema kuwa ni lazima akinamama na viongozi wa (UWT) kuwa makini katika matumizi ya mitandao ya kijamii hasa kwa watoto na vijana kwani ni dhahiri kwamba, baadhi ya vijana hawaitumii vyema mitandao hiyo na kupelekea kuporomoka kwa maadili na kuathiri utamaduni wa Kizanzibari.


Katika ziara yake hiyo, Mama Shein aliwakabidhi kadi 80 kwa wanachama wapya waliojiunga na Jumuiya hiyo ya (UWT) kwa Wilaya ya Dimani na Mfenesini.

Nae Mama Asha Balozi, Mke wa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar  alieleza kusikitishwa kwake na vitendo vya ubakaji vilivyokithiri na kusisitiza kuwa nguvu za pamoja zinahitajika ikiwa ni pamoja na kushirikishwa jamii katika Kamati zilizoundwa kwa makususdi hayo.

Mama Asha alieleza haja ya kutiliwa nguvu na kauli mbiu iliopo hivi sasa isemayo “Mama mlinde mwanao na mwana wa mwenzio” na kusisitiza kuwa mtoto kamwe hawezi kulelewa na mzazi peke yake bali jamii nzima inayomzunguka inalo jukumu hilo.

Nae Mama Fatma Katume alitumia fursa hiyo kuwataka wanachama wa Jumuiya hiyo kujitokeza kwa wingi kwenda kuchukua fomu za kugombania nafasi mbali mbali za uongozi katika jumuiya hiyo wakati ukifika tena bila ya woga.

Nae Waziri wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wawake na Watoto Maudline Castico aliwaeleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kupambana na vitendo  hivyo na kusisitiza haja ya mashirikiano ya pamoja katika kupiga vita janga hilo.

Nao wanajuiya ya (UWT) walieleza kufarajika kwao na ziara hizo za Mama Shein na kumsifu kwa uungwana wake wa kwenda kuwasalimia na kuwashukuru kwa kuendelea kuiunga mkono CCM na kukipa ushindi wa kishindo katika uchaguzi uliopita na kuahidi kuwa ushindi wa chama hicho utakuwa endelevu katika chaguzi zote zijazo.

Aidha, kwa upande wao pia walieleza masikitiko yao kutokana na vitendo vya ubakaji.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.