Habari za Punde

Umoja na Mshikamono Ndio Njia Pekee ya Kujiletela Maendeleo.- Mama Mwanamwema Shein.

MKE wa Rais wa  Zanzibar Mama Mwanamwema Shein ameeleza kuwa umoja na mshikamano ndio njia pekee ya kujiletea maendeleo endelevu katika jamii.

Mama Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Ikulu Ndogo Migombani wakati alipofanya mazungumzo na viongozi wanaounda Umoja wa wake wa Viongozi kwa upande wa Zanzibar, wakiwemo wake wa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Wabunge pamoja na viongozi wa Viti Maalum wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Katika maelezo yake, Mama Shein akiwa ndie mlezi wa Umoja wa Wake wa Viongozi, aliwakaribisha wake wa viongozi wa Majimbo yote ya Unguja katika Umoja huo na kueleza kuwa mafanikio makubwa yamepatikana ndani ya Umoja huo kutokana na mashirikiano makubwa yaliopo.

Alisema kuwa  mashirikiano ya pamoja yanahitajika katika kuwaepelekea maendeleo wananchi na kusisitiza kuwa ushiriki wao una nguvu kubwa katika kuwasaidia wananchi, kuisaidia nchi yao sambamba na kukiimarisha Chama chao cha CCM.

Nae Mama Asha Balozi, Mke wa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambaye pia, ni Mwenyekiti wa Umoja huo aliwaeleza wake hao wa viongozi pamoja na viongozi wengine waliohudhuria mkutano huo umuhimu  na malengo ya Umoja huo katika kuisaidia jamii kwa kushirikiana na Serikali iliyopo madarakani chini ya uongozi wa CCM.

Mama Asha alieleza kuwa uongozi wa Chama sio ajira bali ni jukumu katika kuwatumikia wananchi ikiwa ni pamoja na kuwasaidia katika kuzitatua changamoto wanazozikabili sambamba na kushirikiana nao katika shughuli zote za maendeleo.

Nao wake hao wa viongozi wakiwemo viongozi wa Viti Maalum walitoa pongezi zao kwa Mama Mwanamwema Shein kwa kubuni wazo lake hilo ambalo limeweza kutoa mchango mkubwa katika kuisaidia jamii katika maeneo mbali mbali Unguja na Pemba pamoja na kuendelea kukipa ushindi chama cha CCM huku wakiahidi kuendelea kumuunga mkono.

Wakati huo huo, Mama Shein amepokea fedha taslim kiasi cha Shilingi milioni kumi za Kitanzania, zilizotolewa kwa lengo la kuuimarisha Umoja huo ili uzidi kuimarika na kuwasaidia wananchi katika Majimbo yao, fedha hizo ni ahadi iliyotolea na Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mohammed Raza na wenzake hivi Karibuni huko katika Ukumbi wa Nyumba za Wazee Sebleni, wakati Mama Shein alipofanya mazungumzo na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa Unguja pamoja na viongozi wa Viti Maalum.

Mohamed Raza ametoa jumla ya Shilingi milioni nne kwa niaba ya familia yake, Amani Makungu ambaye aliwakilishwa na Mwakilishi wa Jimbo la Rahaleo Nassor Salim Aljazira, ambaye alikabidhi Shilingi milioni mbili na Taufiq Salim Turky ambaye ametoa Shilingi milioni mbili kwa niaba ya familia yake.

Hassan Mohammed Raza nae alikabidhi Shilingi milioni mbili kwa niaba ya familia ya Mfanyabiashara maarufu Naushad Mohammed, ambao wote kwa pamoja waliahidi kuendelea kuunga mkono Umoja huo kwa kuthamini majukumu yake katika kuisaidia jamii pamoja na kuiendeleza CCM ili iendelee kutekeleza vyema Ilani yake ya Uchaguzi.

Aidha, Mama Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi na shukurani kubwa kwa wapenda maendeleo hao ambao aliwahakikishia kuwa fedha hizo zitatumika vizuri ili kufikia malengo yaliokusudiwa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.