6/recent/ticker-posts

Mpango wa kuzisimamia kesi za jinai na kuzipa namba maalum wazidi kuibua kesi zaidi


Na ZUHURA JUMA, PEMBA

JESHI la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, limesema mpango wa kuzisimamia kesi za jinai na kuzipa namba maalum, (Investigation Register), uliokuwepo kisheria na mwaka 2016 kuutekeleza rasmi, umesaidia kugundua makosa 100 ya jinai.

Kabla ya Jeshi hilo kuanza kuutumia mpango huo ambao upo kisheria, kwa mwaka jana waligundua makosa 39 ya jinai, ambayo ndio pekee walioyapa namba za usajili wa kosa husika ‘IR number’.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Kamanda wa Polisi mkoani humo Haji Khamis Haji, alisema awali Jeshi hilo lilishindwa kutekeleza mpango huo, kutokana na kuhofia uwingi wa majalada kwa kesi ambazo tayari jamii wameshazifanyia sulhu.

Alisema kuanzia mwaka 2016, rasmi Jeshi hilo limeamua kila kesi itayofikisha kwao, kwanza ni kuipa namba maalumu na kuwa nayo kwenye kumbu kumbu za kipolisi, kwa ajili ya shughuli nyengine.

 “Kesi yoyote inayokuja kuanzaia sasa tunaipa namba ‘IR number’ hata kama mwishowe haina na kesi ya kujibu ndani yake, mwaka jana ilikuwa mpaka tujiridhishe kuwa kuna ushahidi katika kesi husika, ndio tuipe namba, kwani wananchi huwa na tabia ya kusuluhishana na kupelekea kuwepo mrundikanao wa majalada”, alisema Kamanda huyo.

Kamanda huyo alieleza kuwa, sababu nyengine iliopelekea kuongezeka kwa matukio hayo, ni kutokana na mwaka huu kuwepo na harakati za kupita uchaguzi, ambapo matukio mengi ya uhalifu hujitokeza.

Alisema kuwa, makosa ya jinai ya mwaka 2015 ni kesi za kubaka tisa (9), kunajisi tano (5), uvunjaji  kwa dhamira ya kutenda kosa 10, wizi wa mifugo tatu (3), bangi sita (6) na madawa ya kulevya nne (4).

“Kati ya kesi zilizopelekwa mahakamani ni 17, zilizopata hatia 17, zinazoendelea mahakamani tatu (3), zilizo chini ya upelelezi tano (5) na zilizofungwa 14”, alisema Kamanda

Kamanda Haji alieleza kuwa, mwaka huu kumeripotiwa kesi za kubaka 23, uvunjaji kwa dhamiara ya kutenda kosa 47, wizi wa mifugo mbili (2), kupatikana na bangi 15, kupatikana na madawa ya kulevya 12 na kesi ya mauwaji moja (1).

Kati ya kesi hizo, zilizopelekwa mahakamani ni 55, upelelezi 26, zilopata hatia 38, zinazoendelea mahakamani 17 na zilizofungwa 19.

“Kesi ambazo zimefungwa ni kutokana na ushahidi haukuweza kulinganisha na kosa, hivyo ni vyema kwa wananchi kuwa mstari wa mbele kutoa ushahidi, kwani bila ya ushahidi hakuna hatia”, alieleza Kamanda huyo.

Alisema kuwa, ili kesi kupata nguvu na kuweza kupunguza wimbi la matukio ya kihalifu katika jamii, wanajamii hawanabudi kutoa ushahidi wa kutosha  na kuwataka wasichoke kwani hiyo ni haki yao ya msingi.

Haji aliwataka wananchi kushirikiana na Jeshi hilo kwa kuyaripoti matukio yanayotokea katika maeneo yao, ili kuweza kufanikisha kupunguza ama kuondosha matukio ya kihalifu.

Kwa upande wa wananchi wa Mkoa huo walieleza kuwa, wamekuwa wakichukua juhudi za kuwakamata wahalifu na kuwafikisha kituo cha Polisi, ingawa huvunjika moyo wa kuendelea kutokana na wahalifu hao kuwaona wanaranda mitaani na kuzidisha uhalifu mara dufu.

“Wahalifu hata tukiwapeleka wanatolewa na wakija mitaani huzidisha uhalifu, hivyo tumechoka na kupelekea baadhi ya wananchi kujichukulia hatua mikononi mwao, kwani wanaona haki haitendeki”, walisema wananchi hao.

Wananchi hao waliliomba Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua za kisheria wahalifu, ili nao kuweza kupata nguvu ya kuyaripoti matukio hayo pale yanapotokea, jambo ambalo litaweza kuondosha matatizo katika jamii

Post a Comment

0 Comments