Habari za Punde

Dk Khalid asisitiza umuhimu wa elimu ya dini

 Ni  Ustadh Idd Shekha Makame kwa  niaba ya Mwakilishi wa jimbo la Donge  Dkt. Khalid Salum Mohamed akitoa nasaha kwa washiriki wa mashindano ya kuhifadhi Quran huko Donge Kitaruni Unguja.

 i mwanafunzi Juma Kassim Choum akikabidhiwa zawadi ya msahafu baada ya kuhifadhi juzuu tano na kushinda kwa Alama 85.

Ustadh Idd Shekha Makame kwa  niaba ya Mwakilishi wa jimbo la Donge  Dkt. Khalid Salum Mohamed akikabidhi misahafu 140 kwa Amir wa jumuiya ya kuhifadhisha Quran Kanda ya Donge, Wakanda Haji Kombo.

Na Juma Farid, Zanzibar.

WAZAZI na walezi nchini wameshauriwa kuwahimiza watoto wao kusoma kwa bidii elimu ya dini ya kiislamu ili kuandaa  viongozi bora wa baadae watakaosimamia  kwa uadilifu misingi imara ya dini hiyo.

Rai hiyo imetolewa na Mwakilishi wa Jimbo la Donge, Dkt. Khalid Salum Mohamed wakati akizungumza katika mashindano ya kuhifadhi Quran yaliyoandaliwa na Jumuiya  ya kuhifadhisha Kanda ya Donge  yaliyofanyika Donge Kitaruni katika Madrasa ya Twalibina Wilaya ya Kaskazini “B” Unguja.

Alisema elimu ndio urithi wa kudumu na wenye manufaa kwa watoto wa jinsia zote kwani wanakuwa na misingi ya  maadili mema  na kuepuka mambo maovu.

Pia Dkt. Salum ambaye pia ni Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, aliwasihi wazazi, walimu na viongozi wa madrasa za Wilaya hiyo kukaa pamoja na kupanga mikakati ya kudumu ya kuthibiti tatizo la wanafunzi wa kiume wanaoacha mapema masomo ya kidini hiyo bila sababu za msingi.

Akizungumza kwa niaba ya Mwakilishi huyo, Ostadh Idd Shekha Makame alieleza kwamba waumini wa dini hiyo wanatakiwa kuwa wamoja na wenye kuamrishana mema na kukatazana mabaya wakati wote na sio katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani pekee.

“Elimu ndio nyenzo pekee ya kuleta maendeleo ya kudumu kwa mwanadamu yeyote na jamii yetu itapiga hatua za kimaendeleo kwa haraka kama vijana wetu tutakuwa tumewarithisha rasilimali hiyo.”, alisema Ostadh Shekha kwa niaba ya Dkt. Salum.

Hata hivyo  Ostadh Shekha alitoa wito kwa madrasa zilizoshiriki katika masindano hayo kwamba licha ya kutoa elimu ya dini wanatakiwa kuanzisha miradi ya maendeleo itakayozalisha kipato kitakachosaidia kutatua baadhi ya changamoto zinazowakabili.

Pamoja na hayo Dkt. Salum alitoa zawadi ya misahafu 140 na magunia manne ya Tende kwa vyuo vilivyoshiriki mashindano hayo.

Naye Katibu wa jumuiya hiyo, Haji Ali Makame alizitaja changamoto zinazowakabili katika jumuiya hiyo kuwa ni kushuka kwa kiwango cha uelewa wa masuala ya dini kutokana na kuwepo kwa tabia za baadhi ya waumini kuiga utamaduni za kigeni.

Mashindano hayo yameshirikisha wanafunzi 97 kutoka  vyuo vya Madrasa 10  za  Mkoa wa Kaskazini Unguja waliosoma quran kuanzia juzuu ya Pili hadi 17 ambapo washindi wa mashindano hayo wamepokea zawadi mbali mbali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.