Habari za Punde

Timu 4 Zilizopanga Matokeo 11-1, 7-1 Central Wilaya ya Mjini Zapigwa Faini na Kufutwa Katika Mashindano , Viongozi wa Timu Hizo Wote Wafungiwa Mwaka Mmoja.

Na: Abubakar Khatib “Kisandu”, Zanzibar.
Kamati ya Soka la Vijana Wilaya ya Mjini imezipiga faini ya jumla ya shilingi laki tatu na kuziondosha katika Mashindano timu za FC Muembe beni, Real Kids, Schalke 04 na King Boys baada ya kukutwa na hatia ya upangaji wa matokeo katika mechi zao za mwisho za hatua ya 4 bora zilizopigwa Jumapili iliyopita ya July 23, 2017.

Katika michezo hiyo miwili iliyovikutanisha vilabu hivyo vinne, michezo ambayo ilikuwa inatafuta Bingwa wa Daraja hilo la Central ambapo timu ya Schalke 04 ilishinda mabao 11-1 dhidi ya King Boys wakati mchezo mwengine FC Muembe beni iliwafunga Real Kids 7-1 ndipo hapo baada ya kumalizika michezo hiyo viongozi wa Mashindano hayo wakashindwa kutoa zawadi na kupelekea jana kutoa maamuzi hayo baada ya kamati kujiridhisha.

Khamis Machano ambae ni mwenyekiti wa kamati hiyo amesema wametoa maamuzi hayo kwakuwa wamejiridhisha kwamba timu hizo zimepanga matokeo na kuamua kuzifuta na kuzipiga faini ya shilingi laki tatu.
“Kamati tumekaa na kuamua kuwapiga faini ya shilingi laki tatu kwa kila timu kati ya hizo nne mana kuna kila sababu ya kuwa wamepanga matokeo, baada ya kupitia ripoti za makamisaa zinaeleza kuwa michezo hiyo ina viashiria vya upangaji wa matokeo, kwa mujibu wa kanuni zetu kifungu nambari 25 kinatuamuru kuzifuta timu zote na kuzipiga faini ya shilingi laki tatu kutokana na kitendo hicho”.
Wakati huo huo Kamati hiyo imewafungia mwaka mmoja kutojihusisha na soka viongozi wote wa timu hizo nne ambao walikaa kwenye Mabenchi kwenye michezo hiyo.
“Viongozi wote waliyokaa kwenye Mabenchi kwenye michezo hiyo tumewafungia mwaka mmoja kutojihusisha na soka”. Alisema Machano.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.