Habari za Punde

Majumuisho ya Ziara ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein Mkoa wa Kaskazini Pemba.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Pemba                                                                                                                24.08.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein, ameutaka uongozi wa Mkoa wa Kaskazii Pemba, Wilaya ya Micheweni na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi zishirikiane katika kuhakikisha soko la Tumbe linaanza kutumika ndani ya miezi miwili.

Dk. Shein aliyasema hayo katika hotuba yake ya majumuisho aliyoitoa baada ya kumaliza ziara yake ya siku mbili katika Mkoa wa Kaskazini Pemba, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), huko Mchangamdogo.

Dk. Shein alisema kuwa iwapo itashindikana basi wapeleke Serikalini mapendekezo juu ya matumizi mbadala ya soko hilo kwa hapo baadae.

Soko hilo limejengwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Mradi wa MACEMP na kuzinduliwa na Rais Dk. Shein mnamo mwaka 2015 na kutoa huduma kwa kipindi cha miezi miwili tu na baadae kusita kutumia hadi hivi leo.

Kusita kwa soko hilo kunatokana na mivutano iliyopo kati ya wananchi na taasisi zinazosimamia soko hilo.

Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi pia, imetakiwa kufanya uwamuzi wa haraka sana wa kuwaajiri na kuwapeleka Pemba vijana wanaomaliza masomo yao katika Chuo cha Kilimo Kizimbani, ili kutatua tatizo uhaba la bibi shamba na bwana shamba.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba na Mkuu wa Wilaya ya Wete na Micheweni wapite katika skuli kwa kushirikiana na Wakaguzi wa Elimu wa Wizara ya Elimu ili kuwachukulia hatua za kinidhamu walimu watoro.

Dk. Shein pia, aliipongeza Wizara ya Afya kwa kujenga benki ya damu katika Mkoa wa Kaskazini Pemba na kutoa agizo kwa Wizara kuwa makini katika suala hilo nyeti sana katika kuanishwa na kuiendesha benki hiyo ya damu iwapo haitajiandaa vizuri na kuwa waangalifu na waadilifu lengo hilo halitofanikiwa.

Wizara ya Afya pia, ilitakiwa kununua mashine ‘ultrasound’ kwa ajili ya matumizi ya huduma za wajawazito kwenye kituo cha Junguni na vituo vyengine vitano vitakavyojengwa katika maeneo mengine ya Unguja na Pemba.

Kwa upande wa jukumu la wanaCCM, Dk. Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar amewataka wanaCCM kudumisha umoja na mshikamano, kuandaa utaratibu mzuri wa kusimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020 pamoja na kuyatumia matawi kwa ajili ya kuimarisha chama.

Katika hotuba yake hiyo, Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Mkoa huo kwa juhudi unazoendelea kuchukua katika kuimarisha hali ya usalama katika Mkoa huo ili kuwawezesha wananchi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii kwa amani na utulivu.

Dk.Shein aliitaka Ofisi ya Mkoa, Wilaya ya Wete pamoja na Wizara ya Ardhi, Maji Nishati na Mazingira kushirikiana katika kufanya maandalizi madhubuti ya kufanikisha uzinduzi wa umeme kwenye Kisiwa cha Fundo huku akiipingeza Wizara hiyo kupitia ZECO kwa kuupeleka umeme kisiwani humo.

Ofisi ya Mkoa na Kamisheni ya Ardhi nayo ilitakiwa kuendeleza mikakati ya kukabiliana na matatizo ya ardhi ikiwa I pamoja na kushughulikia suala la uvamizi katika eneo la skuli ya Chimba.

Kwa upande wa Sekta ya Michezo, Dk. Shein aliutaka uongozi wa Mkoa na Wilaya ya Micheweni kushirikiana na Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo katika utekelezaji wa uwanja wa michezo Micheweni kwa haraka iwezekanavyo.

Aidha, Dk. Shein alitoa agizo na kutaka Mkuu wa Mkoa huopamoja na RPC wa Mmkka huo wa Kaskazini kuwa wahusika wote wa tukio la tarehe 21 Agosti mwaka huu kuhusiana na dawa za kulevya watafutwe na kupelekwa katika vyombo vya sheria na kutaka ndani ya wiki mbili jambo hilo likamilike.

Pia, aliutaka Mkoa kupitia Baraza la Mji la Wete na Halmashauri ya Wilaya ya Miheweni wasimamie usafi na sheria za mipango miji katika kuyaimarisha mazingira ya miji

Kwa upande wa zao la karafuu, Dk. Shein alisisistiza haja ya kuendeleza jitihaza za kukabiliana na magendo ya karafuu na Serikali itafanya kila linalowezekana katika kupambana na watu wanaoendesha hujuma dhidi ya zao la karafuu.

Aidha, alilitaka Shirika la ZSTC kuwa makini katika kulishughulikia zao la karafuu katika uchumaji, ununuzi, uuzaji nje ya nchi huku likihakikisha kuwa wakulima wa karafuu hawapati usumbufu.  


 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.