Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Elimu Zanzibar leo Ikulu.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                              25.10.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, ameupongeza uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kutekeleza vyema majukumu yake na kusisitiza kuwa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuwa na elimu bora.

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2016/2017, Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2017/2018 na Utekelezaji wake kwa  kipindi cha robo ya kwanza ya Julai hadi Septemba kwa mwaka 2017.

Dk. Shein, alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Wizara hiyo ya Elimu, pamoja na watendaji wake wote kwa kwenda sambamba na azma ya Serikali ya kuwa na elimu bora huku akisisitiza haja ya Kujituma katika majukumu yao yote.

Aidha, Dk. Shein aliueleza uongozi huo haja ya kufanya kazi kwa pamoja, kusaidiana na kushirikiana katika kutekeleza majukumu yao ili Wizara hiyo ienndelee kupata mafanikio makubwa zaidi na kuwasisitiza kuwa wasichelee kuchukua hatua pale inapobidi kufanya hivyo.

“Hapa mlipofika leo pazuri sana, hivyo jitahidini msirudi nyuma kwani mmefanya kazi kubwa na nzuri, hivyo ni lazima tukupongezeni, hongereni sana na sote tumeridhika”, aliongeza Dk. Shein.

Mapema akizungumzia suala la utafiti, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuwepo kwa tafiti katika Wizara kwani hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuibua mambo mbali mbali na hatimae kupata majibu na kueleza kuwa Wizara yoyote ya Serikali haiwezi kwenda bila ya utafiti.

Dk. Shein pia, alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa vuguvugu la mashindano ya riadha kwa wanafunzi katika kipindi cha sherehe za elimu bila malipo kwa lengo la kuibua vipaji.

Alieleza kuwa ni vyema kwa kila mwanafunzi akapata muda wa kucheza na kuweza kushindana na wanafunzi wenziwe katika skuli nyengine ili wawe wakakamavu na kusisitiza haja ya kila skuli kuwa na mwalimu maalum wa michezo kama ilivyokuwa hapo siku za nyuma.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya michezo ni vyema Wizara hiyo ikatilia mkazo sanaa, katika skuli na hata katika Vyuo Vikuu kwani sanaa ni sehemu ya kuimarisha utamaduni, hatua ambayo pia, huchangia kupata wasanii mahiri.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alitoa pongezi kwa Wizara hiyo na kusisitiza haja ya kuimarishwa kwa Maktaba za Skuli pamoja na kulielezea suala zima la ukaguzi wa skuli na kutaka walimu wakuu wawe wakaguzi wa kwanza katika kuwasimamia walimu wanaowaongoza katika skuli zao.

Waziri wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali,  Riziki Pembe Juma alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa jinsi alivyokuwa karibu sana na Wizara hiyo kwa kuwapa miongozo na maelekezo ambayo yamechangia kwa kiasi kikubwa katika kuendeleza sekta ya elimu.

Alieleza kuwa jumla ya wanafunzi 2,655 wakiwemo 372 wapya na 2,283 wanaoendelea na elimu ya juu wamepatiwa mkopo kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya juu ya Zanzibar ambapo jumla ya TZS Bilioni 2,630 zimelipwa. Aidha, Bodi imefanikiwa kukusanya jumla ya TZS milioni 480, kutoka kwa wadaiwa waliohitimu.

Hata hivyo, Waziri huyo wa Elimu alieleza kuwa katika mwaka wa afedha  2017/ 2018, Wizara inaendelea na malengo ya kupanua upatikanahji wa huduma za elimu na kuimarisha ubora wa elimu inayotolewa  kwa kuimarisha elimu ya Maandalizi ikiwa ni pamoja na kujenga skuli ya Maandalizi huko Mbuyu maji, Matemwe Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Pia, kuimarisha Elimu ya Msingi kwa kujenga skuli mbili katika maeneo ya Kwarara an Fuoni-Pangawe, kuwajengea uwezo walimu katika kutathmini maendeleo ya watoto katika kusoma, kuandika na kuhesabu, kununua vitabu vya kujifunza kusoma na kutoa huduma ya chakula kwa skuli 10 za Unguja na Pemba.

Lengo jengine ni kuimarisha elimu ya Sekondari kwa kujenga skuli mbili Mwanakwerekwe na Wingwi, madarasa 48 na maktaba katika skuli 23 za Unguja na Pemba, kukamilisha ujenzi wa vituo viwili vya Mafunzo ya Amali vya Daya kwa Pemba na Makunduchi kwa Unguja na kukamilisha ujenzi wa majengo ya Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Karume na Taasisi ya Maendeleo ya Utalii ya Maruhubi na kujenga viwanja 11 vya michezo katika skuli 11.

Aidha, Waziri huyo alieleza changamoto katika sekta hiyo ya elimu ikiwa ni pamoja na kasi ya ongezeko la wanafunzi wanaoandikishwa katika skuli za msingi na sekondari hasa katika skuli za Mkoa wa Mjini Magharibi haiowani na ongezeko la miundombinu ya skuli na matokeo yake idadi ya wanafunzi kwa darasa inaongezeka, hali inayoathiri ubora wa elimu.

Uongozi wa Wizara hiyo pia, ulieleza hatua walizozichukua katika kupita maskulini na kuangalia usomeshaji na mahudhurio ya walimu madarasani sambamba na kuchukua juhudi za kuwashajihisha walimu kufanya kazi kwa ufanisi huku ukielezea jinsi ulivyofanya ukaguzi wa kushtukiza ambao umeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa.

Pia, katika maelezo yao uongozi wa Wizara hiyo walieleza changamoto iliyopo hivi sasa ya uhaba wa walimu uliopo ambayo pia, huchangiwa na tabia ya baadhi ya walimu kuhama hama kwa visingizo mbali mbali na baadhi ya wengine kukataa kushomesha katika skuli za vijiji na hata katika skuli za Pemba.

Ungozi huo pia, ulieleza haja ya kuwepo kwa Maktaba za Wilaya kwa ajili ya kuwafikishia watoto huduma hiyo kwani matumizi ya Maktaba Kuu iliyopo mjini kwa hivi sasa idadi ya watumiaji wake ni ndogo hali ambayo inatokana na masafa na umbali ya watoto wanakoishi pamoja na wazazi wengi kutowashajiisha watoto wao kutumia Maktaba.

Sambamba na hayo, uongozi huo ulieleza azma yake ya kuimarisha miundombinu ya elimu ikiwa ni pamoja na kukamilisha madarasa 200 yaliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi Unguja na Pemba pamoja na juhudi wanazoendelea nazo katika ukusanyaji wa fedha za madawati.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.