Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Ardhi,Maji Nyumba na Nishati Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein,  ameupongeza uongozi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati kwa kutekeleza vyema majukumu yao na kuutaka kuandaa ziara maalum za kazi kwa ajili ya kwenda kuwasikiliza wananchi changamoto zinazowakabili.

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2017/2018, na Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2018/2019.

Dk. Shein alisema kuwa kwa vile Wizara hiyo imeyagusa maisha ya wananchi ni vyema kwa uongozi huo kwenda kuwasikiliza ili kutambua changamoto zinazowakabili na kuweza kuzipatia ufumbuzi kwani bila ya kufanya hivyo inawapelekea wananchi kuanza kulalamika kupitia vyombo vya habari jambo ambalo si busara.

Aliongeza kuwa kumsikiliza mwananchi ni sifa moja wapo ya kiongozi hivyo ni vyema  kwenda kwa wananchi kuwasikiliza hasa ikizingatiwa kuwa Wizara hiyo imewagusa wananchi kwa kiasi kikubwa kutokana na huduma zake inazozitoa ikiwemo maji, ardhi, nishati, nyumba na mambo mengineyo.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwakumbusha viongozi hao umuhimu wa Kamati ya Uongozi wa Wizara hiyo ambayo inaendeshwa kwa mujibu wa sheria zilizowekwa na kuwasisitiza wajumbe wa Kamati hiyo kuhudhuria vikao husika ambavyo vina umuhimu mkubwa katika kuiongoza Wizara hiyo.

Rais Dk. Shein alieleza umuhimu wa kuzingatia na kufuata sheria na taratibu zinazoongoza Wizara hiyo huku akisisitiza haja ya kuwaelemisha wananchi juu ya mambo mbali mbali ya Wizara hiyo ambayo wanapaswa wananchi kuyajua zikiwemo sheria za Wizara hiyo.


Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji Mpango Kazi huo iliyofanywa na Wizara hiyo huku akisisitiza haja kwa kila taasisi ya Wizara hiyo kutoa huduma zake ipasavyo hasa kutokana na Wizara hiyo kugusa maisha ya wananchi.

Nae Waziri wa Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Salama Aboud Talib alieleza kuwa  tayari Wizara hiyo imekamilisha Sera ya Ardhi ambayo kukamilika kwakwe kutaiwezesha Zanzibar kuimarisha utawala na maendeleo endelevu ya ardhi na usimamizi wa maliasili zilizomo katika ardhi hiyo kwa ajili ya maendeleo hapa nchini.

Waziri Salama alieleza kuwa lengo kuu la Sera hiyo ni kukuza uchumi na kuimarisha thamani ya ardhi pamoja na kuendeleza usimamizi wa matumizi bora ya ardhi.

Aidha, Waziri huyo alieleza kuwa Wizara kupitia Mamlaka ya Maji (ZAWA) imeendelea kusimamia shughuli za program za uhuishaji na upanuzi  wa shughuli za maji Mijini na usambazaji wa maji vijijini.

Aliongeza kuwa katika utekelezaji wa programu hiyo Mradi wa uchimbaji wa visima na usambazaji wa maji unaofadhiliwa na Jamhuri ya Watu wa China umefanikiwa kukamilisha ujenzi wa matangi matano ya maji katika maeneo ya Kisongoni, Chaani na Donge Mkoa wa Kaskazini Unguja na Kiboje, na Miwani kwa Mkoa wa Kusini Unguja.

Pia, Waziri huyo alieleza kuwa mradi huo umekamilisha kazi ya uchimbaji wa visima 11 katika maeneo hayo na ulazaji wa mabomba kwa masafa ya kilomita 20.17  kwa maeneo ya mradi, pamoja na kupelekwa kwa umeme, fidia na tayari umeshakabidhiwa Wizara.

Alieleza kuwa katika juhudi za kuimarisha mazingira bora ya utekelezaji wa kazi tayari Wizara kupitia ZURA  imeanza  kutekeleza shughuli za ujenzi wa jingo la Ofisi hapo Maisara ambalo linatarajiwa kukamilika mnamo mwaka wka fedha 2019/2020.

Sambamba na hayo, Waziri huyo alieleza kuwa Wizara kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia (ZPRA) imeendelea na zoezi la kukuza uelewa kwa jaimii juu ya masuala ya Mafuta na Gesi Asilia Unguja na Pemba kwa kuendesha Semina, Mikutano, Makongamano pamoja na kurusha hewani vipindi vya redio na televisheni.

Nao viongozi wa Wizara hiyo walimpongeza Rais Dk. Shein kwa maelekezo yake anayoyatoa kwao hatua ambayo inawarahisishia kutenda kazi zao huku wakimuhakikishia kuwa wanaendelea kutekeleza vyema kazi zao ili kuweza kutoa huduma bora kwa wananchi wote wa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.