Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Awapongeza Wanafunzi Waliofanya Vizuri Mitihani Yao na Kutowa Skolashifi 30 Kwa Wanafunzi Hao Kwa Masomu Tafauti Waliofaulu.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, akiwahutubia Wanafunzi wa Kidatu cha Sita na Kidatu cha Nne Zanzibar waliofanya vizuri mitihani yao ya Taifa kwa mwaka wa masomo 2017/2018, wakati wa hafla ya chakula maalum alichowaandaliwa kwa ajili ya kuwapongeza na kuwakabidhi zawadi, hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya Ikulu Zanzibar. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein  amewataka wanafunzi kuongeza kasi katika kusoma masomo ya Sayansi na Sanaa kwani bado Zanzibar inahitaji wataalamu wengi zaidi katika fani mbali mbali ili kwenda na mabadiliko ya karne ya 21.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hafla ya kuwapongeza na kuwazawadia wanafunzi wa Kidato cha Nne na cha Sita waliofanya vizuri katika mitihani ya Taifa na kula nao chakula cha mchana, hafla iliyofanyika katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd na viongozi wengine.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa kila nchi ina mahitaji ya wataalamu wa fani za Sayansi na Sanaa, wakiwemo madaktari, wahandisi, marubani, viongozi, wanasheria, wanazuoni, mashekhe na fani nyenginezo.

Aidha, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutangaza rasmi kuwa Serikali imetoa udhamini wa nafasi 30 kwa wanafunzi waliopata daraja la Kwanza kwenda kusoma vyuo vya ndani na nje ya Zanzibar huku akisisitiza kuwa Serikali anayoingoza haitosita kufanya hivyo katika uongozi wake.

Alisema kuwa Serikali inathamini sana juhudi za wanafunzi hao katika kutafuta elimu na ndio kila mwaka amekuwa akiongeza nafasi za udhamini kwa wanafunzi wanaopata daraja la kwanza.

“Nilianza na wanafunzi wa daraja la kwanza Kidato cha sita 10 baadae wanafunzi 15 na sasa Serikali imeongeza hadi wanafunzi 30 waliopata daraja la kwanza”, aliongeza Dk. Shein.

Alieleza kufurahishwa kwake na taarifa ya wanafunzi 126 wanawake 48 na wanaume 78 wa Kidato cha sita katika mwaka huu wa 2018 wamefaulu kwa kupata daraja la kwanza na wanafunzi wanawake 61 na wanaume 74 ambao ni jumla ya wanafunzi 135 walifanya mitihani ya Kidato cha Nne mwezi Novemba mwaka 2017 wamepata daraja la kwanza.

Aliwapongeza wanafunzi wanaume kwa kuweza kupata daraja la kwanza kwa wingi zaidi kuliko wanafunzi wanawake kutokana na mwaka jana kuwatia moyo na hamasa katika sherehe kama hizo huku akieleza kuwa anaamini kwamba mwakani wanawake wataendelea kushika nafasi yao ya kuongoza.

Aliwapongeza wanafunzi hao wote kwa kufanya vizuri katika masomo ya Sayansi, Biashara na Sanaa na kutoa pongezi maalum kwa mwanafunzi Biubwa Khamis Ussi na Fahad Rashid kwa kupata Daraja la Kwanza la kiwango cha point 3 kila mmoja na kuwemo katika orodha ya wanafunzi 10 bora katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, aliwapongeza wote waliopata daraja la kwanza kwa kuwa wameijengea sifa Zanzibar na kuwadhihirishia wananchi, wazazi na walimu wao kwamba katika mazingira yaliyoandaliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hivi sasa kupata daraja la kwanza kwenye mitihani ya Taifa inawezekana katika masomo ya Sanaa.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi maalum kwa Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohammed Mahmoud kwa kutoa zawadi ya Kompyuta 96 aina ya Laptop tarehe 04 Septemba mwaka 2018 katika viwanja vya Mnara wa kumbukumbu ya Mapinduzi Mwembe Kisonge kwa wanafunzi wa Kidato cha Sita wote waliopata daraja la kwanza katika Mkoa wake.

Alimpongeza kwa dhati Naibu Katibu Mkuu wa CCM Dk. Abdalla Juma Mabodi kwa kushirikiana na viongozi wengine wa CCM kwa kuwapongeza na kuwazawadia vijana waliofanya vizuri pamoja na kuipongeza Mikoa yote ya Pemba pamoja na Mkoa wa Kaskanini Unguja kwa kufanya hivyo.

Rais Dk. Shein aliipongeza Benki ya Watu wa Zanzibar kwa kuwazawadia vijana hao na kuahidi kuwa huo ni mwanzo tu wa safari ndefu ya kuwaandaa vijana ili wawe mabingwa wa fani mbali mbali na bila shaka juhudi hizo zitaendelezwa kwa nguvu na mashirikiano makubwa.

Alieleza kuwa mwakani sherehe kama hizo atazifanya kubwa zaidi na ziwe za aina yake wakati wa usiku ili vijana washereheke kwani ni kumbukumbu ya maisha yao huku akieleza kuwa juhudi hizo ni azma ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

”Sherehe hizi ni sehemu ya kazi…..na kama mnavyojua kuwa ukiona vyaelea ujue vimeundwa”, aliongeza Dk. Shein.

Kutokana na juhudi kubwa za kusoma za wanafunzi hao Rais Dk. Shein alimnukuu mwanasoka maarufu Duniani, Edson Arantes do Nascimento maarufu Pele pale aliposema 
“Mafanikio sio ajali ni kazi ngumu inayotaka jitihada za wakati wote kujifunza, kusoma, kujitolea na miongoni mwa yote hayo ni mapenzi kwa yale unayotaka kufanya ama kujifunza”.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, walimu, wazazi, walezi na wale wote walioshiriki katika kuwalea, kuwasomesha na kuwatayarisha wanafunzi hao hadi wakapata matokeo mazuri yanayofurahisha.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuandaa utaratibu wa kuwazawadia walimu waliofanya vizuri katika kuwasomesha na kuwaandaa wanafunzi katika mitihani yao ya Taifa hapo mwakani ili nao wazawadiwe katika siku kama hiyo.

Kwani alisema kuwa kufanya hivyo kutawapa ari, nguvu na hamasa walimu wengi zaidi kufanya vizuri katika ufundishaji na utayarishaji wa wanafunzi kwa ajili ya mitihani yao.

Pia, aliuagiza uongozi wa Wizara hiyo uandae utaratibu wa kuzizawadia skuli mpya zilizojengwa katika kipindi cha miaka mitano ya mwanzo ya uongozi wake kwani aliwashaagiza kufanywa hivyo wakati akitoa hotuba yake ya majumuisho ya ziara ya Mkoa wa Kusini Pemba Agosti 19 mwaka jana 2017.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa tamko alilolitoa Mwasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar Mzee Abeid Amani Karume la kutangaza elimu bure kwa wananchi wa Zanzibar bila ya ubaguzi ndio msingi wa mafanikio ya maendeleo yanayopatikana hapa Zanzibar.

Aliongeza kuwa kila Mzanzibari mwenye elimu hivi sasa kwa njia tafauti amefaidika na juhudi za Serikali za kutoa elimu bila ya Malipo. “haitofilisika Serikali kwa kutoa elimu bure na afya bure kwani ndio Sera ya Mapinduzi ya Zanzibar ambapo jambo la tatu ni ardhi ambayo yote ni mali ya Serikali”, alisema Dk. Shein.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuendeleza utamaduni wake huo na kumuahidi kuwa Wizara yake itaendelea kumuunga mkono na kuimarisha juhudi katika kuhakikisha sekta ya elimu inaimarika.

Waziri Pemba alimpongeza Rais kwa kuipa kipaumbele sekta ya elimu na sekta ya afya ambazo zote kwa pamoja zinaenda sambamba katika kuleta matokeo mazuri ya mitihani ya wanafunzi ikiwa ni pamoja na kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Alitumia fursa hiyo kuwasisitiza vijana hao kuwa wazalendo kwa nchi yao na kusisitiza kuwa Wizara yake inaendelea kupata nafasi kadhaa za masomo ndani na nje ya nchi.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Dk. Idrisa Muslim Hija alisema kuwa wanafunzi wa Kidato cha Nne jumla ya wanafunzi 11,402 walifaulu kwa madaraja mbali mbali na jumla ya wanafunzi 142 wamefaulu kwa kiwango cha Daraja la Kwanza na kati ya wanafunzi 1,777 wa Kidato cha Sita wanafunzi 126 wamefaulu kwa kiwango cha daraja la Kwanza.

Katibu Mkuu huyo alitoa pongezi kwa jitihada za Rais Dk. Shein pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuiendeleza sekta ya elimu juhudi ambazo zimeiwezesha Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kupeleka vitabu na vifaa vya maabara katika skuli zote zenye Kidato cha Tano na Sita kwa masomo yote.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.