Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na mwenyeji wake Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Uhuru Kenyatta, baada ya Uzinduzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi Endelevu wa Bahari,(Sustainable Blue Economy) uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kenyatta Nairobi Kenya leo.
Na. Suzan Kunambi Nairobi Kenya.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Mhe Dk.Ali Mohamed Shein, alisema kuwa Kenya na
Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla zina uhusiano wa
kihistoria na kindugu ambao ni lazima uimarishwe na uendelezwe kwa faida ya
pande zote mbili.
Dk. Shein aliyasema hayo wakati
akizungumza na Rais wa Kenya, Mheshimiwa
Uhuru Kenyatta katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Kenyatta mjini Nairobi
. Katika mazungumzo hayo,Dk. Shein alisisitiza
juu ya ushirikiano katika kuendeleza uchumi wa bahari
kuu baina Kenya na Zanzibar na Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kwa jumla.
Dk. Shein alisema kwamba watu wa Tanzania ni ndugu na wamoja kwa hivyo ni muhimu pande mbili hizo
kuzidisha ushirikiano huo uliopo
katika masuala mbali mbali ya kiuchumi
na kijamii.
Akizungumzia
suala la kuendeleza uchumi wa bahari
kuu, Dk. Shein alishauri kwamba ni
muhimu kuandaliwe programu ya pamoja ya kuimarisha uvuvi wa bahari kuu, hatua ambayo ni muhimu katika jitihada
zinazoendelea za kukuza ajira kwa vijana
na kuwa na matumizi bora ya
rasilimali za bahari.
Vile
vile, katika kufanikisha mikakati na mipango iliyopo ya kuimarisha
matumizi bora ya rasilimali za bahari,
mito na maziwa alisema kwamba ni vyema nchi hizo zikahakikisha kwamba sekta
binafsi zinashirikishwa kikamilifu.
Aidha,
Dk. Shein alipendekeza kwamba itakuwa ni
vyema kuanzisha utaratibu ambao utaziwezesha timu za viongozi na wataalamu kutoka pande mbili hizo kukutana
mara kwa mara, ikiwa ni hatua muhimu ya
kujadili mafanikio na changamoto mbali
mbali zinazojitokeza katika sekta hiyo. Aliongeza kusema kwamba hatua
hiyo ni muhimu katika kuimarisha uhusiano uliopo.
Kwa
upande wake, Rais wa Kenya, Mheshimiwa
Uhuru Kenyatta alimpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein na ujumbe aliofuatana nao kwa
kwa kukubali mwaliko wa kuhudhuria katika mkutano wa Kimataifa wa Uchumi
Endelevu wa bahari unaoendelea nchini
humo.
Rais Kenyatta alipongeza uamuzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa kuanzisha
safari za meli baina ya Zanzibar na Mombasa kwa ajili ya kuimarisha huduma za
usafiri, biashara na kuendeleza uhusiano wa kidugu na kihistoria uliopo baina ya wananchi wa pande mbili hizo.
Vile
vile, alishauri kwamba itakuwa ni vyema hivi sasa kuimarisha huduma za usafiri
kwa kuanzisha safari za ndege za moja kwa moja
baina ya Zanzibar na Mombasa, ili
kufanikisha utekelezaji wa mipango na
mikakati ya kuimarisha sekta ya utalii, hasa ikizingatiwa kwamba sekta hiyo ni
muhimu kwa uchumi wa pande zote mbili.
Alisema kwamba hivi sasa wapo watalii
wengi wanaotembelea Mombasa ambao wangependa kusafiri moja kwa moja kwenda Zanzibar lakini
hushindwa kufanya hivyo kutokana na kukosekana kwa usafiri wa aina hiyo.
Mheshimiwa
Uhuru Kenyatta, alihimiza haja ya kuimarsiha mikakati iliyopo ya kudhibiti
uvuvi haramu katika mwambao wa Afrika Mashariki, sambamba na kuimarisha hali ya usalama katika ukanda huo.
Katika kikao hicho viongozi hao walikubaliana ziwepo
ziara za mara kwa mara za viongozi wa ngazi mbali mbali la kuongeza maelewano
na kuhakikisha utekelezaji wa mambo wanayokubaliana .
No comments:
Post a Comment