Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk.Ali Mohamed Shein, Azungumza na Ujumbe wa Jumuiya ya Wafanyabiasha Wenye Viwanda ya Sharjah Ikulu leo.7/12/2018.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Wenye Viwanda ya Sharjah ambae pia ni Mwenyekiti wa Kampuni ya Al Rawabi Bw. Abdallah Sultan Owais akiwa na Naibu Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Sheikh Majid Faisal Khalid Al Qasemi, walipofika Ikulu Zanzibar leo kwa mazungumzo.


RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameikaribisha Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda ya Sharjah kuzichangamkia fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda ya Sharjah ambae pia, ni Mwenyekiti wa Kampuni ya Al Rawabi Abdallah Sultan Owais akiwa pamoja na baadhi ya viongozi wa Jumuiya hiyo.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Mamlaka ya Uwekezaji, Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) tayari imeweka mazingira mazuri ya kuwekeza hapa nchini na kusisitiza kuwa milango ya uwekezaji ya Zanzibar iko wazi.

Rais Dk. Shein aliueleza uongozi huo wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda wa Sharjah kuwa Zanzibar ina fursa nyingi za kuwekeza katika sekta mbali mbali hapa nchini ikiwemo sekta ya utalii, viwanda, ufugaji na nyenginezo ambazo Jumuiya hiyo ina uzoefu.

Mbali ya kuitaka Jumuiya hiyo kuja kuekeza Zanzibar, Rais Dk. Shein pia alisisitiza haja ya kuwepo mashirikiano na uhusiano na Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda ya Zanzibar huku akisisitiza kuwa Zanzibar iko tayari kufanya kazi na Jumuiya hiyo.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuwepo kwa mashirikiano ya pamoja kati ya Jumuiya hizo mbili kutaisaidia kwa kiasi kikubwa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda ya Zanzibar kupanua wigo na kupata uzoefu kutoka kwa wenzao wa Sharjah.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya ufugaji na kusisitiza azma na malengo iliyoweka ikiwa ni pamoja na kujifunza kutoka kwa Kampuni ya Al Rawabi ya Sharjah ambayo tayari imeshapata mafanikio makubwa.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kupongeza mafanikio yaliofikiwa na Kampuni hiyo ya nchini Sharjah ambayo aliitembelea mnamo mwezi Januari mwaka huu wakati alipokuwa katika ziara yake katika nchini za Jumuiya ya Falme za Kiarabu (UAE).
Alisisitiza kuwa Kampuni ya Alrawabi yenye shamba kubwa la ng’ombe wa maziwa ambayo pia, ina viwanda vya vinywaji vya matunda pamoja na bidhaa nyengine zinazotokana na maziwa ya ng’ombe imeweza kupata mafanikio makubwa na ipo haja kwa Zanzibar kupanua wigo kutoka kwa Kampuni hiyo.

Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kuendelea kusisitiza haja ya Kampuni ya ndege ya Al Arabia ya Sharjah kufanya safari zake Zanzibar kwa azma ya kuongeza huduma za usafiri hasa kwa watalii pamoja na wananchi na wafanyabishara wa pande mbili hizo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa shukurani na pongezi kwa Sheikh Mohammed bin Rashid Al Makhtoum  Makamo wa Rais na Waziri Mkuu wa Nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), kwa juhudi alizozichukua za kuhakikisha Kampuni ya ndege ya Fly Dubai inaleta ndege kubwa tena ya kisasa hapa Zanzibar.

Dk. Shein alisema kuwa amepokea kwa furaha taarifa hiyo kutoka kwa Mwenyekiti huyo kwani jambo hilo lina umuhimu wa pekee katika kuimarisha huduma za usafiri wa ndege kati ya Dubai na Zanzibar sambamba na kuimarisha usafiri kwa watalii kati ya pende mbili hizo.

Nae, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda ya Sharjah ambae pia, ni Mwenyekiti wa Kampuni ya Al Rawabi Abdallah Sultan Owais ameeleza kuvutiwa kwake na mazingira ya Zanzibar na kumuahidi Rais Dk. Shein kuwa Jumuiya hiyo itahakikisha inaimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo.

Katika maelezo yake, kiongozi huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Jumuiya yake imevutiwa kuja kuwekeza Zanzibar hasa kutokana na mazingira mazuri sambamba na vivutio kadhaa ambavyo vimekwua vikiwavutia hasa watalii.

Aliongeza kuwa ujio wa watalii wengi ambao ameushuhudia yeye mwenyewe ni ushahidi wa pekee kuwa Zanzibar inajiuza kiutalii hatua ambayo inapokelewa vyema na watalii wa kila pembe ya duniani na kupelekea kumimininika kwa wingi kuja kuitembelea Zanzibar.

Pamoja na hayo, kiongozi huyo ameeleza azma ya kukuza uhusiano na ushirikiano kati yake na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara husika ya ufugaji kwa lengo la kuangalia fursa ya kuja kuekeza katika sekta hiyo ya ufugaji.

Pia, kiongozi huyo alimueleza Rais Dk. Shein hatua ya Kampuni ya Fly Dubai ya kuleta ndege kubwa ya kisasa ambayo itafanya safari zake kati ya Zanzibar na Dubai ambayo tayari imeshaanza kazi.

Mwenyekiti huyo wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda ya Sharjah alimpa Salamu Rais Dk. Shein zinazotoka kwa kiongozi wa Sharjkah Dk. Sheikh Sultan Mohammed Al Qasimi ambaye katika salamu hizo alieleza azma yake ya kuendelea kushirikiana na Zanzibar.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.