Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Ajumuika na Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Katika Futari Aliowaandalia Ikulu Ndogo Micheweni Kisiwani Pemba.Tae


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk Ali Mohamed Shein, akijumuika na Wananchi wa Mkoa wa Kaskazi Pembe katika Futari Maalum aliyowaandalia katika Viwanja vya Ikulu Ndogo Micheweni Pemba kushoto Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi na kulia Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Mhe. Omar Khamis Othman. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein amefutari pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba na kuwataka kuendeleza ibada na kufanya mambo ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu.

Hafla hiyo ya futari iliandaliwa na Dk. Shein kwa ajili ya wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba ilifanyika katika Ikulu ndogo Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa dini, vyama vya siasa, Serikali pamoja na wananchi wa Mkoa huo.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Rais, Mkuu wa Mkoa huo Omar Khamis Othman alieleza kuwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni kipindi cha kufanya ibada sambamba na kufanya mambo Mwenyezi Mungu ameamrisha ili kupata rehma za Ramadhani.

Alieleza kuwa wananchi na waumini wote wa Dini ya Kiislamu wanapaswa kufanya vitendo vyema hasa ikizingatiwa Zanzibar ni nchi yenye amani na utulivu mkubwa.

Alisistiza kuwa maendeleo makubwa yaliopatikana hapa Zanzibar yametokana na amani, utulivu na upendo sambamba na juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein.

Aliongeza kuwa kukutana kwao katika hafla hiyo kumetokana na amani, utulivu na upendo mkubwa uliopo hapa nchini na kusisitiza haja ya kuendeleza hata baada ya kumalizika kwa mwezi wa Ramadhani ili Zanzibar iendelee kupata neema.

Aidha, aliwasisitiza wananchi kuendelea kuzitumia vyema mvua za masika kwa kuimarisha na kuendeleza sekta ya kilimo kwani ndio uti wa mgongo wa taifa hili.

Alieleza kuwa mvua zinazoendelea ni vyema wakulima wakazidisha juhudi kwa kupanda miti ya kudumu ili waweze kufaidika wao pamoja na vizazi vijavyo huku akisisitiza haja ya kuimarisha kilimo cha mpunga kwani ndio chakula kinachopendwa zaidi hapa nchini.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuridhishwa na juhudi kubwa zinazochukuliwa na wakulima katika kuimarisha sekta ya kilimo hapa nchini na kueleza kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono ili mafanikio zaidi yaweze kupatikana.

Alhaj Dk. Shein aliwatakia Ramadhani njema wananchi wa Mkoa huo na kuwataka kumaliza salama funga yao ya mwezi mtukufu wa Ramadhan ili hatimae kusherehekea vyema Sikukuu ya Idd el Fitri kwa salama na amani.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein aliwashukuru wananchi wote waliohudhuria katika futari hiyo aliyowaandalia na kupongeza jinsi walivyoonesha upendo mkubwa kwake kwa kukubali muwaliko wake huo.

Mkuu wa Mkoa huo pia, litumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa niaba ya wananchi wa mkoa huo na kutoa pongezi zake kwa Alhaj Dk. Shein kwa kufutari pamoja na wananchi wa Mkoa huo katika eneo hilo la Micheweni na kueleza jinsi wananchi hao walivyofurahi kuona jinsi Rais wao alivyokuwa karibu nao.

Aidha, wananchi hao walitumia fursa hiyo kumuombea dua Rais Dk. Shein kwa ukarimu na upendo wake mkubwa aliyowaonesha pamoja na ukarimu anaoendelea kuwaonesha wananchi wote wa Zanzibar katika kipindi hichi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na katika kipindi chote cha uongozi wake.

Nae Ustadh Omar Hamad alitumia fursa hiyo kusoma dua na kumuomba Mwenyezi Mungu aendelee kuleta neema na baraka katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.

Wakati huohuo, nae Mama Mwanamwema Shein kwa upande wake aliungana pamoja na viongozi wanawake wa kitaifa wa Mkoa huo pamoja na wananchi katika futari hiyo maalum aliyoianda Rais Dk. Shein.

Leo Alhaj Dk. Shein anatarajiwa kuungana pamoja katika futari maalum aliyowaandalia wananchi wa kijiji cha Mkanyageni Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.