Habari za Punde


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameongoza mazishi ya Marehemu Ali Ferej Tamim huko katika Makaburi ya Mwanakwerekwe mjini Unguja  na kuungana na ndugu, jamaa,marafiki pamoja na wanamichezo mbali mbali walioshiriki mazishi hayo.

Marehemu Ali Fereji Tamim ambaye aliwahi kuwa kiongozi wa Chama Cha Soka cha Zanzibar (ZFA) kwa zaidi ya miaka 20 na kukiongoza chama hicho katika nyadhifa mbali mbali ikiwemo Urais wa Chama hicho.

Aidha, Marehemu Ali Ferej Tamim ambaye ni mmoja wa wanamichezo waliotoa mchango mkubwa katika mpira wa miguu hususan Zanzibar pia, aliwahi kushika wadhifa wa kuwa Makamo wa Rais wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) kwa muda mrefu.

Sambamba na hayo, Marehemu Ali Ferej Tamim alichukua juhudi kubwa katika uongozi wake katika kuhakikisha Zanzibar inapatiwa uwanachama wa Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) pamoja na kuhakikisha ligi kuu ya Zanzibar inapata udhamini na kuvipa nafasi vilabu vidogo vidogo.

Ali Ferej Tamim amefariki dunia leo alfajiri katika hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja mjini Zanzibar baada ya kusumbuliwa na maradhi kwa muda mrefu ambapo Marehemu Ali Ferej ameacha kizuka mmoja na watoto wawili.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.