RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, ametuma salamu za
rambirambi kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na wafanyakazi wa IPP Media kufuatia
kifo cha Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP Dk. Reginald Abraham Mengi.
Kifo cha Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP
Dk. Reginald Abraham Mengi kilitokea alfajiri ya kuamkia Alhamis ya Mei 2, 2019
akiwa mjini Dubai Falme za Kiarabu (UAE).
Rais Dk. Shein alieleza kuwa amepokea kwa mshtuko
na huzuni kubwa taarifa ya kifo cha Dk. Mengi na kueleza kuwa yeye binafsi
pamoja na wananchi wote wa Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla wamejawa na
simanzi nzito kufuatia msiba huo mkubwa wa kitaifa.
“Kwa hakika msiba huu umetugusa Watanzania sote,
ni msiba wetu kwa sababu aliefariki ni ndugu yetu, mwenzetu, mfanyabiashara, mwekezaji
mzalendo na aliyekuwa akiwajali wanyonge wakiwemo wananchi wa rika zote pamoja
na watu wenye ulemavu, wanamichezo na wapenda mazingira”,ilieleza sehemu ya
salamu za rambirambi alizozituma Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa vile kifo ndio
mwisho wa uhai wa mwanaadamu alimuomba Mwenyezi Mungu aijaalie roho ya marehemu
Dk. Reginald Mengi alilaze mahala salama.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa
wananchi wa Zanzibar wanaungana na ndugu, jamaa, wafanyakazi wa IPP Media na
marafiki wa marehemu katika msiba huo mzito.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alimuomba
Mwenyezi Mungu awape Watanzania wote na wanafamilia nyoyo za subira katika
kipindi hiki kigumu cha msiba.
Katika salamu hizo za rambi rambi Rais Dk. Shein
alieleza kuwa hatomsahau Marehemu Dk. Reginald Abraham Mengi kwa juhudi zake
kubwa katika suala zima la uhifadhi wa mazingira ambaye aliweza kushirikiana
nae kwa kiasi kikubwa wakati Rais Dk.
Shein akiwa Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano na Dk. Mengi akiwa Mwenyekiti
wa Baraza la Taifa la Mazingira (NEMC).
Dk. Shein alieleza kuwa Marehemu Dk. Reginald Abraham
Mengi ambaye aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Biashara la Afrika Mashariki
(EABC) kuanzia mwaka 2008 hadi 2009 alihamasisha Maendeleo ya Kanda ya Jumuiya
ya Afrika Mashariki (EAC) kwa kuchangia ukuaji wa sekta binafsi kuendana na
soko la pamoja kwa nchi wanachama.
Marehemu Dk. Mengi pia, atakumbukwa kwa juhudi
zake kubwa katika kuiimarisha tasnia ya Habari katika nchi za Afrika Mashariki
ambapo vile vile aliweza kuanzisha tunzo za waandishi wa habari katika nchi za
(EAC) kwa ajili ya kuhamasisha ari ya uandishi wa kujenga uhusiano mwema wa (EAC).
Pia, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Marehemu Dk.
Mengi atakumbukwa kwa uzalendo wake wa kuipenda nchi yake pamoja na wananchi
wake hasa katika kuimarisha michezo ambapo hadi mauti yanamfika alikuwa Mlezi wa Timu ya Taifa ya Vijana U17
“Serengeti Boys”.
Dk. Reginald Abraham Mengi alizaliwa katika kijiji
cha Nkuu huko Machame, Kilimanjaro, Tanzania mnamo mwaka 1942 ambaye amefariki
alfajiri ya kuamkia Alhamis ya tarehe 2, Mei 2019 akiwa mjini Dubai Falme za
Kiarabu (UAE).
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment