Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Aongoza Hitma ya Dr. Badria Abubakar Gurnah Masjid Mahamur Upanga Jiji Dar es Salaam.



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein  ameongoza hitma ya kumuombea Dk. Badriya Abubakar Gurnal mke wa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Sadala (Mabodi) iliyofanyika katika msikiti  Maamur Upanga jijini Dar-es-Salaam.

Katika hitma hiyo, iliyohitimishwa na Sheikh Zain Sharif na dua yake kutolewa na Sheikh Ayoub Ali Seif wote wa msikiti Maamur, viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali walihudhuria pamoja na wana familia wakiwemo ndugu, jamaa na marafiki.

Baada ya hitma hiyo, akitoa neno la shukurani kwa niaba ya familia mjomba wa Marehemu alitoa shukurani kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein kwa ushiriki wake na kuungana pamoja na wanafamilia hao katika kisomo hicho.

Aidha, alitoa shukurani kwa wote waliohudhuria hitma hiyo na kutumia fursa hiyo kumuelezea Marehemu jinsi alvyokuwa mtu mwema, mwenye hikma na hulka aliyekuwa akifuata maadili ya Kiislamu sambamba na maadili ya kazi yake ya Udaktari.

Mapema Alhaj Dk. Shein akiwa na Mama Mwanamwema Shein walifika nyumbani kwao Marehemu Mikocheni jijini Dar-es-Salaam kwa ajili ya kutoa mkono wa pole kwa ndugu, jamaa watoto pamoja na mume wa Marehemu Dk. Badriya.

Akiwa nyumbani kwao Marehemu Rais Dk. Shein na Mama Mwanamwema Shein walitia saini kitabu cha Maombolezi kufuatia kifo cha Marehemu Badriya Gurnal.

Baada ya tukio hilo Rais Dk. Shein pamoja na Mama Mwanamwema Shein walitoa mkono wao wa pole huku Rais Dk. Shein akiwaomba wana familia wakiwemo ndugu, jamaa, watoto pamoja na mume wa marehemu kuwa na moyo wa subira katika kipindi hichi kigumu cha msiba.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alieleza jinsi alivyomfahamu Dk. Badriya katika maisha yake yote pamoja na utendaji wake wa kazi uliotukuka tokea Rais Dk. Shein akiwa Naibu Waziri wa Wizara ya Afya ambapo pia, aliwaomba wanafamilia kuzidi kuendelea kumuombea dua Marehemu.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi ambaye pia ni Mume wa Marehemu alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa kuwa karibu na familia hiyo tokea uhai wa marehemu, ugonjwa wake pamoja na hatua yake hiyo ya kwenda kuwafariji kwa kwuapa pole.

Dk. Mabodi alimshukuru Rais Dk. Shein kwa msaada wake mkubwa kwa familia hiyo na jinsi alivyokuwa karibu na Marehemu katika kipindi chake chote katika uhai wake na katika utendaji wake wa kazi.

Mara baada ya kutoa mkono wa pole kwa ndugu, jamaa, watoto na mume wa Marehemu Mama Mwanamwema Shein aliungana pamoja na akina mama wengine wakiwemo wakiwemo wanafamilia pamoja na viongozi mbali mbali katika hitma ya wanawake ya kumuombea Marehemu Badriya.

Hitma hyo iliyoongozwa na Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan ilifanyika nyumbani kwao Marehemu Badriya Mikocheni jijini Dar-es-Salaam.

Maziko ya Marehemu Dk. Badriya Abubakar Gurnal mke wa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar yalifanyika Juni 23, 2019 huko katika makaburi ya Kisutu jijini Dar-es-Salaam.

Marehemu Dk. Badriya alikuwa mfanyakazi wa Benki kuu ya Tanzania (BOT) ambaye alifariki Jumaamosi Juni 22 2019 katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, alikokuwa amelazwa akipatiwa matibabu baada ya kuugua kwa muda mfupi.

Marehemu Badriya Abubakar Gurnal ameacha mume na watoto watatu, Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahali pema peponi, Amin.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.