Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti waBaraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein.Azungumza na Mtawala wa Ras Al-Khaimah Sheikh. Saud Bin Saqr Al Qasimi leo.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amekutana na Mtawala wa Ras-Al-Khaimah Mtukufu Sheikh Saud Bin Saqr Al Qasimi na kufanya nae mazungumzo yaliolenga kuendeleza uhusiano na ushirikiano hasa katika sekta ya elimu.

Mazungumzo hayo yaliofanyika katika makaazi ya Sheikh Saud  Bin Saqr Al Qasimi mjini Ras-Al-Khaimah, ambapo kiongozi huyo wa Ras- al Khaimah  alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa yuko tayari kuisaidia Zanzibar katika kuimarisha sekta ya elimu.

Sheikh Saud Bin Saqr Al Qasimi alieleza kuwa Ras-al Khaimah imepiga hatua nzuri katika kuimarisha sekta ya elimu hasa elimu ya juu hivyo, ipo tayari kutoa fursa kwa walimu wa Zanzibar kwenda nchini humo kujifunza katika vyuo vikuu vilivyopo.

Aliongeza kuwa hatua hiyo itasaidia zaidi kutoa nafasi kwa walimu wengi waliopo Zanzibar kupata mafunzo ambayo watawasaidia na walimu wengine sambamba na kuongeza ufaulu kwa wanafunzi hasa wale wanaosoma elimu juu.

Alieleza kuwa programu hiyo ya kutoa mafunzo na kuwajengea uwezo walimu kutoka Zanzibar itakuwa ya kila mwaka na itadhaminiwa na Serikali ya Ras Al Khaimah.

Aidha, kiongozi huyo alieleza kuwa programu hiyo itajikita zaidi katika masomo ya Sayansi hali ambayo itasaidia kuendeleza masomo hayo sambamba na kuimarisha sekta ya elimu hasa katika karne hii iliyopo.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao walieleza kuwa Zanzibar na Ras-al. Khaimah zina mambo mengi yanayofanana kwa hivyo kuna haja kubwa ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo.

Pamoja na hayo, kiongozi huyo wa Ras Al Khaimah alimueleza Rais Dk. Shein azma ya nchi yake kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo za kiuchumi na kijamii.

Alieleza kuwa nchi yake inathamani uhusiano na ushirikiano huo uliopo na kuahidi kuwa itaendelea kuweka mikakati madhubuti katika kuhakikisha mashirikianao katika sekta za maendeleo yanadumishwa baina ya pande mbili hizo.

Kiongozi huyo wa Ras Al Khaimah alizipongeza juhudi za Rais Dk. Shein na kuahidi kuziunga mkono kwani anaona jinsi anavyofuatilia kwa karibu uimarishaji wa sekta za maendeleo kwa manufaa ya Zanzibar na watu wake.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, katika maelezo yake, alitoa shukrani kwa kiongozi huyo kutokana na juhudi zake za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na kumpongeza kwa azma yake hiyo ya kuiunga mkono sekta ya elimu Zanzibar.

Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka kwa ndugu zao wa Ras Al Khaimah na iko tayari kupanua wigo wa maendeleo kutoka nchini humo kwani inatambua mafanikio yaliopatikana kutokana na mikakati iliyowekwa katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya elimu.

Pamoja na hayo, viongozi hao kwa pamoja walizungumzia hatua zaidi zinazohitajika katika kuimarisha ushirikiano kati ya Zanzibar na Ras Al Khaimah katika sekta za maendeleo ikiwa ni pamoja na kupanga mipango madhubuti katika malengo yaliokusudiwa ya hapo baadae.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Sheikh Al Qasimi na kueleza kuwa programu hiyo ambayo amekusudia kuiunga mkono itasaidia kuimarisha juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inazoendelea kuzichukua katika kukuza sekta hiyo.

Aidha, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imepiga hatua katika kuimarisha elimu ya msingi na Sekondari hivyo hatua hiyo ya Serikali ya Ras Al Khaimah itasaidia kuimarisha elimu ya juu sambamba na kuongeza idadi ya wataalamu katika fani mbali mbali.
  Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.