Habari za Punde

Serikali Imejizatiti Katika Kilimo Cha Kitaalam Kuendeleza Kwa Vitendo Mapinduzi ya Kilimo Bora Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akifungua Maonesho ya Siku ya Chakula Duniani katika viwanja vya Chamanangwe Wilaya ya Wete Pemba, kulia Waziri wa Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi Zanzibar.Mhe. Mmanga Mjengo Mjawiri.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema serikali imejidhatiti kuendeleza kwa vitendo Mapinduzi ya Kilimo kwa kuwapa taaluma ya kilimo bora wakulima, wafugaji na wavuvi, pamoja na kuendeleza huduma za ugani.

Dk. Shein amesema hayo katika ufunguzi wa Maonesho ya siku ya chakula Duniani, yaliofanyika katika viwanja vya Chamanangwe, Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Alisema katika kutekeleza azma hiyo, Serikali itaendelea kutowa huduma za matrekta na pembejeo mbali mbali za kilimo, kwa kutoa ruzuku ya asilimia 75 kama ilivyoahidi .

Alisema Serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri ya kibiasharaili kuwawezesha wafanyabiashara kuingiza na kuuza zana, vifaa na pembejeo za kisasa kwa wakulima kwa urahisi.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja ya wakulima kulima kwa kuzingatia matumizi ya mbinu za kisasa za kilimo pamoja na kufuata maelekezo ya wataalamu.

Alitaka kuwepo matumizi bora ya pembejeo za kilimo, mbolea pamoja na kuwataka wakulima kuondokana na kilimo cha mazowea, akibainisha hatua hiyo italiwezeshaTaifa kuongeza mavuno ya mazao ya chakula na biashara na kutoa uhakika wa chakula na lishe bora.

Rais Dk. Shein aliitaka Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kuhakikisha inakuwa na mipango na mikakati madhubuti katika kuwaelimisha, kuwahamasisha na kuwasaidia wananchi ili kuwa na mwamko wa kutumia teknoljia bora za kilimo katika mazao mbalimbali.

“Maarifa watakayopata wananchi kupitia maonyesho haya yatawasidia  kupata mbinu mpya za kuongeza uzalishaji katika kilimo na kuongeza tija”, alisema.

Aidha, alisema kupitia maonyesho hayo, wananchi watapata fursa ya kuzijua taasisi mbalimbali zinazotoa mikopo kwa wakulima, wavuvi na wafugaji pamoja na wajasiriamali na hatimae  kuweza kusaidiwa.

Alisema wananchi wataweza kujifunza na kuitumia elimu watakayoipata ili kuongeza uzalishaji katika shughuli za kilimo, uvuvi na ufugaji na hivyo kukuza uchumi pamoja na kujiongezea kipato cha kujikimu.

Akigusia changamoto za ajira zinazowakabili vijana, Dk. Shein  aliisistiza umuhimu wakutembelea maonesho hayo ili kuona fursa za kujiajiri zilizopo.

Alisema serikali itaendelea na juhudi za kuwasaidia vijana kupata mitaji ya kuendesha shughuli zao kupitia mfuko maalum ulioanzisha hivi karibuni pamoja na Mfuko wa Khalifa Fund wenye gharama ya  Dola za Kimarekani Milioni 10.

Sambamba na hilo, Dk. Shein alisema katika kipindi cha miaka mitano serikali imetenga Dola Milioni 10 (sawa na shilingi Bilioni 46) kwa lengo hilo hilo la kuwawezesha vijana kujiajiri na kupunguza kutegemea ajira kutoka serikalini.

Katika hatua nyengine, Dk.Shein alisema Serikali imeanzisha taasisi ya utafiti wa kilimo, mifugo na uvuvi ili kuziwezesha shughuli hizo kufanyika kisasa zaidi pamoja na kubaini changamoto zilizopo, hatua iliyokwenda sambamba na kukiunganisha Chuo cha Kilimo Kizimbani na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Alitowa wito kwa vijana wenye sifa za kujiunga  na masomo ya utaalamu wa kilimo, mifugo na uvuvi kujiunga na na masomo hayo ili Taifa lipate wataalamu inaowahitaji.

“Naiagiza Wizara ya Kilimo, maliasili. Mifugo na Uvuvi iendelee kuwaajiri vijana waliokwisha maliza masomo yao ya kitaalamu wakumbushwe kazi zao sio kukaaa ofisini, bali wawafuate wakulima huko waliko, kwani ndio namna bora ya kuwatumikia”, alisema.

Akigusia uendelezaji wa kilimo cha mpunga, Dk. Shein alisema kuna mafanikio ya kuongezeka kwa mavuno yalioanza kupatikana na kusema hivi sasa Serikali imejielekeza katika mradi mkubwa wa ujenzi wamiundombinu ya uwagiliaji maji kupitia mkopo wa Dola Milioni 50 kutoka Benki ya Exim ya Jamuhuri ya Korea.

Alisema mradi huo utatekelezwa katika mabonde matano yanayolimwa mpunga, ikiwemo Cheju, Kilombero, Bumbwisudi, Mkwararani na Mlemele, hatua itkayopanuwa wigo wakilimo cha mpunga wa umwagiliaji kutoka ekari 810 hivi sasa na kufikia ekari 2,397.

Alisema kutokana naongezeko hilo, kuna matarajio makubwa ya kuongezeka kwa mavuno ya mpunga nchini kutoka wastani watani 31,000 za mchele hadi kufikia tani 70,365, hivyo kupunguza matumizi ya fedha za kigeni katika kuagiza bidhaa hiyo.

“Takwimu zinaonyesha Zanzibar kwa mwaka tunatumia wastani wa shilingi Bilioni 40.5 kununua mchele peke yake, kiwango hiki kitapungua kwakiasi kikubwa na hatimaeckuondoka kabisa”, alisema.

Aidha, aliwataka Wakuu wa Wilaya kote nchini  kuongeza kasi ya mashirkkiano na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, sambamba na kusimamaia ipasavyo maendeleo ya kilimo katika Wilaya zao.

Alieleza kuwa mafanikio haliofikiwa na kuongezeka uzalishaji katika sekta ya kilimo, kunatowa matumaini makubwa katika miaka michache ijayo Zanzibar itajitosheleza kwa chakula,  kuwa na lishe bora na usalama wa chakula.

Alisema lishe borana usalama wa chakula ni muhimu katika kuleta ustawi wa jamii na hasa watoto wenye mahitaji maalum pamoja na wagonjwa.

Dk. Shein aliipongeza Wizara ya kilimo, Maliasili,Mifugo na Uvuvi pamoja na Wizara ya Elimu na mafunzo ya Amali kwa kuendeleza mpango wa kutoe elimu ya lishe bora kupitia maskulini, akibainisha kuwa ni uamuzi waserikali katika kuimarisha afya za watoto pamoja na kukabiliana na utapiamlo.

“Natoa wito kwa wananchi kuzingatia haja ya kula chakula chenye lishe bora kitakachosaidia kuimarisha afya zetu, tuone umuhimu wa kula vyakula vya asili vinavypapatikana kwawingi hapa nchini,ikiwemo matunda na mboga mboga ili tupate lishe bora”, alisema.

Mapema, Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Mmanga Mjengo Mjawiri, alisema muelekeo wasekta ya kilimo ni kuongeza uzalishaji na usarifu wa mazao ili kuongeza tija kama ilivyoainishwa katika MKUZA pamoja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya  2015-2020.

Aliipongeza serikali kwa juhudi za kutoa kipaumbele katika sekta ya kilimo, ili kuona uzalishaji wachakula onaongezeka na kuleta tija kwa jamii.

Alisema uamuzi wa Serikali wa kuanzisha Idara ya uhakiki wa chakula pamoja an ghala la Akiba la chakula ni muhimu , kwani pamoja na mambo mengine utapunguza mfumko wa bei na kuondokana na hatari ya kuibuka kwa njaa.

Alisema Wizara hiyo kwamashirikiano na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali  imejidhatiti kuendelea kutoa elimu kwa wananchi katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi juu ya lishe bora pamoja na  matumizi endelevu ya rasilimali zilizopo, sambamba na kuwataka wananchi, hususan vijana kutumia maonesho hayo kupata ujuzi.

Nae, Katibu Mkuu, Wizara ya Kilimo. Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Maryam Juma Abdalla alisema maonyesho hayo ni ya pili kufanyika katika eneo hilo la Chamanangwe, yakiwa na lengo la kuhamisha wananchi na wadau kutekeleza sera za kuimarisha kilimo nchini.

Alisema sekta ya kilimo imekuwa na mchango mkubwa katika kukuza uchumi na mandeleo ya Taifa na kubainisha katika mwaka uliopita wa 2018, sekta hiyo ilichangia wastani wa asilimia 21.3 ya pato la Taifa.

Alisema maonesho ya mwaka huu yameshirikisha wadau 207 kutoka taasisi za serikali na binafsi, wafanyabiashara pamoja na watoa huduma kutoka serikalini na sekta binafsi.

Maryam aliyapongeza mashirika ya ndani na yale ya Kimataifa kwa kuiunga mkono Serikali katika juhudi zake za kuimarisha kilimo pamoja na kufanikisha vyema maonesho hayo.

Katika hiyo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein  alikabidhi zawadi kwa vikundi mbali mbali vilivyofanya vizuri pamoja na kutembelea mabanda ya maonesho kuona uzalishaji wa bidhaa mbali mbali.


Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.