Habari za Punde

Jamii Imetakiwa Kuwa Karibu na Watoto Wenye Mazingira Magumu.

Na Mwashungi Tahir     Maelezo      22-112019.
Jamii imetakiwa kuwathamini watoto wenye mahitaji maalum kwa kuwasaidia katika kuwapatia misaada mbali mbali ili waweze kujikwamua kimaisha .
Hayo ameyasema  Katibu wa kamati maalum ya NEC ya Idara  maalum ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar.Bi.Catherine Peter  Nao  huko Kituo cha Upendo (Viziwi) kilioko Mwanakwerekwe wakati alipokuwa akikabidhi vifaa vilivyotolewa na Mwakilishi wa viti maalum kupitia watu wenye  ulemavu Mwantatu Mbaraka  Khamis kwa walimu wa kituo hicho.
Amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar  ikiwa katika Utekelezaji wa Ilani imeweka sehemu maalum ya watu wenye mahitaji maalum kwa kutambua umuhimu wa watu hao na kuweka kipaumbele kwa kuwapatia mahitaji yao  ili wapate faraja ya kuthaminiwa.
Pia amewaomba wazazi na walezi kushirikiana na walimu wanaowafundisha watoto hao walio katika mazingira hayo kwa kuwa nao karibu kwani sote ni walemavu watarajiwa.
Hivyo amewataka wawe na subira na kuwapa malezi yaliyo mazuri watoto hao kwa kuwa nao karibu na kuepuka kufanyiwa vitendo vya udhalilishaji ambavyo huwaathiri kisaikolojia.
”Hivi sasa kadhia ya udhalilishaji imelikumba Taifa hasa watoto wenye ulemavu tuwe karibu nao ili tuweze kuwalinda na vitendo hivi, “ alisema Catherine..
Vile vile amewataka wazazi na walezi  kutoa michango ya watoto hao kwa walimu ili waweze kukidhi mahitaji  yanayotakiwa kituo hapo ikiwemo sabuni  chakula na mahitaji maalum mengine wanayohitajika kwa  walimu hao wanajitolea kuwafundisha na  kuwatunza .
Hata hivyo ameiomba Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kukitembelea  kituo hicho ili kujua changamoto zinazowakabili na kuona vipi wataweza kuwasaidia.
Nae Mwakilishi wa vitu maalum vya watu wenye ulemavu Mwantatu Mbaraka Khamis  akikabidhi  vifaa katika  kituo hicho  amesema  lengo la kutoa vifaa hivyo ni kuunga mkono baada ya kuona wanapatiwa mafunzo ya kujiendeleza katika kituo hicho .
Amewapongeza walimu wa kituo hicho kwa juhudi kubwa wanayoifanya ya kuwahudumia watoto hao  katika mambo mengi ikiwemo kufuma , kushona na pia kutengeza madomet na vitu vyengine kadha na kuweza kujipatia fedha za kujikimu kimaisha.
Kwa upande wa msoma risala Msaidizi  Mkuu wa kituo hicho cha Upendo Sada Hamadi Ali amesema kituo kinatoa mafunzo mbali mbali yakiwemo  ya lugha za alama kwa watoto wadogo wa maandalizi na wa skuli za misingi za Serikali ikiwemo kazi za amali kwa vijana viziwi .    
Pia wanatoa mafunzo ya uzoefu wa tabia za watoto viziwi na wanafunzi wakubwa kufundishwa  lugha za alama ili waweze kupatiwa fursa ya ajira kwa kutumia lugha hiyo katika sehemu za kazi.
Amesema mafanikio waliyoyapata  watoto kujua kuelewa lugha za alama, kituo kutambulika katika  sehemu mbali mbali,  pamoja  na mashirikiano na viongozi wa jimbo hilo .
Kwa upande wa changamoto amesema wanakabiliwa na ukosefu wa mashirikiano na baadhi ya wazazi, ulipaji wa ada, kukosa sehemu ya kuuzia bidhaa zao na ukosefu wa mtaji wa kuendeleza bidhaa hizo .
Jumla ya sh Millioni Moja zimetumika kwa kununuliwa  vifaa hivyo ikiwemo sare za skuli , mabuku, vitamba vya kufumia mashuka , charahani ya kushonea na ya kufumia .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.