Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein Azungumza na Wazee wa CCM wa Wilaya ya Kusini Unguja.


MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameiunga mkono kauli ya Wazee wa CCM wa Wilaya ya Kusini Unguja ya kuwa Wilaya hiyo itaendelea kuwa ngome ya CCM.
Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Skuli ya Kizimkazi Mkunguni, Wilaya ya Kusini Unguja, Mkoa wa Kusini Unguja wakati alipofanya mazungumzo na Wazee wa Wilaya ya hiyo.
Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza kuwa Wilaya ya Kusini Unguja ina historia kubwa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) hivyo, anaamini kuwa Wilaya hiyo ina uwezekano mkubwa wa kuendelea kuwa ngome ya chama hicho.
Alieleza kuwa ushindi wa CCM katika chaguzi zake zote ni jambo ambalo halina mbadala kwani hilo ni agizo la Katiba ya Chama hicho kutokana na malengo iliyojiwekea.
Alisema kuwa malengo ya CCM yako wazi kwamba chama hicho kimeundwa kwa lengo la kushinda uchaguzi Mkuu na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Tanzania Bara na Zanzibar.
Aidha, aliwataka viongozi wote wale ambao wako madarakani na wale wasiokuwepo madarakani bado wana nafasi ya kukipigania Chama Cha Mapinduzi (CCM) kama wanavyofanya Wazee na Mabaraza yao pamoja na Jumuiya za Chama hicho.
Aliwataka viongozi na wanachama wa CCM kufanya kazi na wazee sambamba na kuwasaidia ili waendelee kukiimarisha chama.
Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza haja kwa wazee kuwaeleza vijana juu ya heshima ya wazee na vipi wazee wanatakiwa kuenziwa na kutunzwa sambamba na kupewa heshima yao kutokana na mambo makubwa waliyoyafanya.
Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini na inazijali juhudi za wazee walizozichukua hadi kupelekea kupatikana uhuru wa Tanganyika na uhuru wa Zanzibar kupitia vyama vya ASP na TANU.
Katika hotuba yake aliyoitoa mbele ya wazee hao wa CCM pamoja na viongozi wengine wakuu wa chama hicho Rais Dk. Shein alisema kuwa wazee ndio walioijenga Zanzibar na kuleta ukombozi na hatimae kuwakomboa wanyonge.
Makamu Mwenyekiti huyo alieleza kuwa ipo haja ya kupokea mawazo ya wazee  sambamba na kuwaheshimu na kuwalinda wazee kwani kuna kila sababu ya kufanya hivyo hasa ikizingatiwa historia ya wazee katika kupigania uhuru wa nchi hii.
Rais Dk. Shein alipongeza kwa mapokezi makubwa aliyoyapata katika Wilaya hiyo na kuipongeza risala iliyotolewa ambayo imetoa pongezi kwake na kwa Serikali pamoja na wananchi kwa kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa vitendo.
Makamu mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza umuhimu wa wazee umo kwenye Katiba na Ilani ya CCM kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aliongeza kuwa wakati huu uliopo ndio wakati mzuri wa kushikamana na kuwa kitu kimoja sambamba na kuongeza nguvu katika kukiimarisha na kukiendeleza Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Alisisitiza kuwa ushindi kwa CCM ni lazima ili Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 yaendelee kulindwa yadumishwe na yaendelezwe sambamba na  kudumishwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulioasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Sheikh Abeid Amani Karume.
Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alieleza kuwa utamaduni wa Rais Dk. Shein wa kukutana na wazee ameuanza muda mrefu na kusisitiza haja kwa viongozi wengine wa chama kuiga utamaduni na utaratibu huo.
Naibu Mabodi alieleza kuwa mbali ya juhudi alizozichukua katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo nchini pia, amefanya juhudi katika kukiimarisha chama kwa kujenga Matawi, kuimarisha Mashina pamoja na Ofisi za chama.
Nao Wazee wa CCM Wilaya ya Kusini Unguja walieleza kuwa wanaamini kuwa ujio wa Rais Dk. Shein katika Wilaya hiyo watapata baraka, nasaha, busara pamoja na hekima zake za kuijenga CCM hususan kwa kipindi hichi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.
Aidha, walieleza jinsi wanavyoridhika na utekekelezaji wa Rais Dk. Shein wa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa vitendo pamoja na ahadi zake alizozitamka kipinndi cha Kampeni zilizopita kuzitimiza.
Wazee hao walimpongeza kwa mengi aliyoyafanya ndani ya Zanzibar kwani yapo ambayo yamewagusa moja kwa moja ikiwa ni pamoja na malipo ya Pencheji Jamii ya TZS 20,000 ambapo walianza wazee 1,421 mnamo mwaka 2016 na hivi sasa wapo wazee 1,348 ambao wote wanapata Pencheni hiyo.
Pia, wazee hao walitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kwa jitihada na huruma zake kubwa aliyowaonesha wazee kwa kuwaongeza kima cha chini cha penscheni ya wastaafu.
Walieleza kuwa uungwana wa uchapakazi wa  Rais Dk. Shein uliotukuka  wao wazee wanauona zaidi pale alipolisimamia kidete suala la upatikanaji wa maji safi na salama katika Wilaya yao na kutolea mfano wa kutatua tatizo la maji Makunduchi eneo la Mnywambiji.
Aidha, ahadi aliyoitoa Shehia ya Mtende ameitimiza kabla ya muda wake aliouahidi kufika sambamba na kero ya muda mrefu Shehia ya Michamvi nayo ameshaipatia muarobaini wake na sasa kazi ya kuzika mabomba inaendelea kutokea katika visima vya Ras el Khaimah Bwejuu kuelekea Michamvi.
Walieleza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatarajia kugharamia zaidi ya Bilioni 1.8 katika mradi huo.
Pia, wazee hao walieleza kuridhika na juhudi anazozichukua na Serikali anayoiongoza katika suala zima la kipaumbele cha elimu kwa Zanzibar nzima, kuanzia ujenzi wa skuli za ghorofa, mipango imara ya kuendesha elimu, ufaulu wa wanafunzi umeongezeka na utoro wa skuli umepungua.
Sambamba na hayo, wazee hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuwajengea Chuo Cha Amali killichopo Kisongoni Makunduchi na Skuli Sekondari ya kisasa iliyopo Kibuteni, kuwepo kwa majengo hayo wanaamini itatoa viongozi bora wa hapo baadae.
Kwa upande wa sekta ya afya wazee hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuifanya Wilaya yao ya Kusini kuwa na huduma za kisasa na zinazokwenda na wakati  kwa kuipandisha hadhi hospitali yao ya Makunduchi kuwa Hospiyali ya Wilaya.
Walieleza kwamba kiufanya hivyo kunasaidia kwa kiasi kikubwa sana baadhi ya huduma ambazo walilazimika kwenda katika hospitali ya rufaa na sasa zimesogea Hospitalini hapo.
“Tunashukuru sana wazee wako kwa hakika  wewe ni mja mwema unaejali wazee wako bila ya ubaguzi wa rangi, kabila wala itikadi ya siasa tunasema ahsante sana”, walieleza wazee hao kwenye taarifa yao hiyo.
Sambamba na hayo, wazee hao walimuaahidi Rais Dk. Shein kuwa Wilaya yao ya Kusini itaendelea kubaki kuwa ngome ya CCM.
Wazee hao pia, walishukuru  sana  kwa kuansihwa utaratibu mpya wa kuwakumbuka na kuwaombea dua Waasisi na viongozi mbalaimmbali ambao wamelitumikia Taifa hili kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara.  
Nae Mwenyeviti  wa CCM Wilaya ya Kusini Unguja Abdulaziz Hamad Ibrahim alipongeza ukusanyaji wa mapato na ukuaji wa uchumi jinsi ulivyoimarika hapa Zanzibar hatua ambayo imepelekea kuimarika kwa huduma mbali mbali za maendeleo ikiwa ni pamoja na ununuaji meli mpya ya mafuta na meli ya abiria.
Alimpongeza Makamo huyo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Rais Dk. Shein pamoja na Mwenyekiti wa CCM Taifa Dk. John Pombe Magufuli kwa hatua walizochukuwa katika kuhakikisha ada kwa wanachama wa CCM inahifadhiwa katika akauti maalum hatua ambayo imepelekea kupatikana fedha nyingi.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.