Habari za Punde

WAZIRI KAIRUKI ATIKISA WILAYA 6 ZA MKOA WA PWANI, AWAHAKIKISHIA WAWEKEZAJI MAZINGIRA MAZURI YA UWEKEZAJI.

Mshauri mwelekezi wa Shamba la Utunge Bw. Uwesu Msumi akimuonesha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) Mhe. Angellah Kairuki eneo la shamba hilo lenye ukubwa wa hekari 300 wanalotumia kulima mpunga, vitunguu na mahindi pamoja na ufugaji wa samaki lililopo Wilaya ya Rufiji Mkoa wa Pwani alipolitembelea kukagua eneo hilo.
Na.Mwandishi  Wetu.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Uwekezaji nchini Mhe. Angellah Kairuki amewahakikishia wafanyabiashara na Wawekezaji kuwa Serikali itaendelea kuwawekea mazingira mazuri ya Uwekezaji nchini.
Pia, Amesema Serikali imejipanga kuboresha mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara na wawekezaji ili kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa kuwekeza katika sekta mbalimbali zenye tija katika kuliingizia pato taifa.
Ameyasema hayo hivi karibu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku 6 katika Wilaya 6 za mkoa wa Pwani ikiwemo; Bagamoyo, Kibaha, Kisarawe, Mkuranga, Mafia na Rufiji pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze.
Akieleza lengo la ziara hiyo Mhe.Kairuki amesema mkoa wa Pwani ni miongoni mwa mikoa yenye uwekezaji mkubwa katika sekta mbalimbali; Uvuvi, kilimo na ufugaji na amefanya  ziara hiyo ili kujionea mazingira  pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili Wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.
Akitoa majumuisho ya ziara hiyo Mhe. Kairuki amezitaja changamoto zilizojitokeza katika maeneo mengi aliyotembelea kuwa ni ukosefu wa maji ya kutosha, ubovu wa barabara, ucheleweshwaji wa vibali vya kazi, kukosa umeme wa uhakika na utitiri wa tozo.
Mbali ya changamoto hizo, Mhe. Kairuki ametaja vikwazo vingine kuwa ni kutotengwa kwa maeneo ya uwekezaji, Taasisi wezeshi kutokuwa karibu na wawekezaji, ukosefu wa mitaji ya uhakika na utoaji wa adhabu zisizo za lazima.
Ameongeza kuwa uelewa mdogo wa wawekezaji katika kujiunga na Kituo cha Uwekezaji Nchini (TIC) ni moja ya  changamoto na kuwataka  wawekezaji kwa hiari yao waone umuhimu wa kujiandikisha katika kituo hicho ili kutumia fursa zinazopatikana.
“Wawekezaji tunawakaribisha TIC ili mjue fursa ziliopo nchini zaidi na kuona namna mnavyoweza kunufaika na kituo hiki,”alisisitiza Waziri Kairuki.
Ameongoza kuwa, ipo haja ya kila Halmashauri kuendelea kutenga maeneo ya uwekezaji ili kutoa fursa zaidi kwa watu kuwekeza na kuhakikisha miundombinu muhimu inakuwepo.
“Natoa rai kwa kila Halmashauri kuhakikisha kila kijiji kinatenga walau heka 20 za maeneo ya uwekezaji na kuwasilisha taarifa zao TIC” alisema Waziri.
Aidha, Waziri Kairuki amewataka wawekezaji kuzingatia sheria na taratibu za uwekezaji nchini ili waweze kunufaika na mitaji yao waliyowekeza.
“Endeleeni kuwekeza pasipo kuvunja sheria na kanuni zilizopo ikiwa ni kulipa kodi au kulipa vibali mbalimbali mfanye hivyo tena kwa wakati ili isitokee mmewekeza kwa mitaji mikubwa halafu ikawa kwa hasara,”alisisitiza Waziri Kairuki
Aliwahakikishia wawekezaji kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano, inatambua mchango wao na imedhamiria kuhakikisha inaboresha miundombinu muhimu ikiwemo uwepo wa nishati ya umeme ya uhakika, barabara bora, upatikanaji wa maji safi, kuboresha mifumo ya mawasilino na upatikanaji wa huduma bora za mamlaka zinazosimamia masuala yanayohusu uwekezaji nchini.
AWALI
Waziri Kairuki alifanya ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Pwani kwa siku 6 na kuzitembelea  Wilaya 6 ambapo jumla ya viwanda 22 alivifikia ikiwemo; Kiwanda cha KEDS, EUROPLASTIC, Samaki investment, KAMAL LTD, Hiill Packaging Company, Tan Choice, Global Packaging Ltd, Hester Bioscience Africa ltd, Chilambo Investment, Sabai Cash nut Processing, SHAFA Investment, Everwell Cable, Ice Drop ltd, Lodhia Group ltd, Waja Mabati na Waja General, Abajuko Enterprises, Tanpesca na kiwanda cha maziwa cha Mather Dairies. Aidha alipata fursa ya kutembelea mashamba ya uwekezaji mbalimbali pamoja na Shamba la Utunge, Sah janand, shamba la Utamaduni, Kigomani na shamba la kuku la AKM.
Wawekezaji wa maeneo hayo walipata fursa za kueleza changamoto wanazokabiliana nazo pamoja na mapendekezo kwa Serikali ya namna bora ya kuendelea kuwa na ushirikiano ili kufikia dhamira ya Serikali ya kuwa na Tanzania ya Viwanda.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.