Habari za Punde

CCTV Kamera Kutumika Kuwabana Madereva Wazembe.


SERIKALI ya  Mapinduzi ya Zanzibar  inakusudia kuanzisha mfumo wa kielektroniki ili kuvitambua  vyombo vya  moto vinavyotembea barabarani kwa lengo la                    kuvifuatilia  na kubaini  madereva wanaokiuka sheria.                                                   
Akiwasilisha Ripoti ya utekelezaji wa Maagizo ya Kamati ya Ardhi na Mawasiliano ya Baraza la Wawakilishi ya Mwaka 2019/2020 kwa Wizara ya Ujenzi, Mawasilino na Usafirishaji, Waziri wa Wizara hiyo Dkt. Sira Ubwa Mamboya  amesema,  katika kutekeleza suala hilo serikali imeanza kutumia mfumo wa Kamera za CCTV zilizowekwa kwa matumizi ya mji salama ili kubaini makosa  ya usalama barabarani.
Aidha amesema Idara ya Usafiri na Leseni inazipitia Kanuni  mbali mbali za usalama barabarani na kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi  katika kuwachukulia hatua za kisheria  madereva wote watakaobainika kufanya makosa ya barabarani  kwa lengo la kuwadhibiti na kunusuru maisha ya wananchi na mali zao.
Wakati huo huo Mheshimiwa Dkt Sira amesema, Serikali inaandaa utaratibu  wa  faini  za  papo  kwa papo ili kuharakisha hukumu na adhabu kwa madereva  wazembe na wanaokwenda kinyume na  sheria za usalama Barabarani.
“Serikali inaandaa utaratibu wa kuwatoza faini watakaobainika kufanya makosa ya barabarani kwa njia za kielektroniki ili kukusanya fedha hizo hapo hapo (barabarani) au kupitia  kupitia Benki kwa kila atakaebainika kufanya makosa” Alifafanua mhe Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano na Usafirishaji.
Mheshimiwa Waziri amefahamisha kwamba  rasimu ya Kanuni hizo za adhabu ya papo kwa papo  imekamilika na kwa sasa ipo wizarani kwa mapitio.
Akichangia hoja hiyo mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Jimbo la Magomeni Mhe Rashid Makame Shamsi ameishauri  Wizara hiyo kuwashirikisha wadau wote wakati wa utungaji wa Kanuni hizo ili kuondosha malalamiko wakati wa utekelezaji wake.
 Imetolewa na :
Divisheni ya Itifaki na Uhusiano
Baraza la Wawakilishi, Zanzibar.
Jumatano, Aprili  15, 2020

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.