Habari za Punde

SMZ yafanikiwa kudhibiti uvujaji wa mapato


NA Himid Choko, BLW

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema imefanikiwa kupata mafanikio makubwa  baada ya kuimarisha mifumo ya usimamizi wa mapato na matumizi yake.

Akiwasilisha Ripoti ya Utekelezaji wa Maagizo ya Kamati ya Kuchunguza na kudhibiti Hesabu za Serikali na Mashirika (PAC) ya Mwaka 2019/2020, Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa  Balozi Mohammed Ramia Abdiwawa  amesema  miongoni mwa hatua  zilizopelekea mafanikio hayo ni pamoja na  kudhibiti uvujaji wa mapato kutokana na kuimarisha mifumo yake ya ukusanyaji kwa kutumia njia za kibenki na mitandao ya simu za mikononi.

Balozi Ramia amezitaja njia nyengine zilizopelekea mafanikio hayo ni kufanya utambuzi wa walipa kodi kwa kutumia mfumo wa kielektroniki pamoja na kufuatilia kwa karibu malimbikizo ya madeni kwa wenye madeni ya kodi.

Aidha Balozi Ramia ameliarifu Baraza la Wawakilishi kuwa Serikali hivi sasa iko katika hatua za mwisho za kufanikisha utumiaji wa risiti za kielektroniki  kwa ajili ya ukusanyaji wa mapato.

Kwa upande wa matumizi ya Serikali, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amesema Serikali inaendelea kutoa mafunzo kwa watendaji wa ngazi tofauti  juu ya uwepo wa Sheria mpya ya zinazohusiana na matumizi ya fedha za umma ili kulinda fedha zake na hatimae zitumike vizuri na kwa tija zaidi.

Aidha amesema serikali pia inaendelea kufanya ukaguzi wa ndani wa mifumo yake ya malipo na kufuatilia taarifa wa wakaguzi hao.

Akitoa maoni ya Kamati ya Kuchunguza  na Kudhibiti  Hesabu za serikali na Mashirika, Makamo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mheshimiwa Shaibu Said Ali amevishauri vyombo vya uchunguzi ikiwemo Mamlaka ya kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi kuchunguza kwa kina madai ya malipo ya  Kampuni  ya Hassan & Sons  yanayokihusisha  Chuo Cha Mafunzo  ambapo kwa mujibu wa Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali ya Mwaka 2016/2017 hati ya malipo, maelezo pamoja na vielelezo vya malipo hayo havikupatikana wakati wa ukaguzi huo.

Amesema malipo hayo yanatokana na deni la mkopo wa pikipiki na vespa ambazo Kampuni hiyo iliikopesha chuo cha Mafunzo.

Mwisho.
Himid Choko, BLW
Alkhamis , April 16, 2020

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.