Habari za Punde

Wananchi Waipongeza Hotuba ya Salamu za Eid El Fitry


WANANCHI wameipongeza hotuba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyotoa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari ikiwa ni salamu zake za sikukuu ya Idd El Fitr hivi karibuni.

Wananchi hao walieleza kufarajika na salamu hizo alizozitoa Rais Dk. Shein katika  hotuba yake hiyo na kusisitiza kuwa wamezipokea mikono miwili na watazifanyia kazi hasa wito alioutoa juu ya kuendeleza mafunzo ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Walieleza kuwa Rais Dk. Shein ameonesha kuwajali kwani licha ya kuwepo kwa janga  la COVID-19 lakini amefanya juhudi za makusudi za kuhakikisha anazifikisha salamu zake kwa wananchi wake anaowaongoza kupitia vyombo vya habari.

“Kwa jambo hili lazima tumpongeze Alhaj Dk. Shein kwa  kutupa salamu za Idd el Fitr wananchi wake kwa kweli tumefarajika sana hasa pale alipotutaka tuendeleze vazi la uchamungu, Allah atamlipa kwa hili”,alisema Nwagili mkaazi wa Ubago Cheche.

Wananchi hao waliongeza kuwa hatua zake hizo zimeonesha kuwa Rais Dk. Shein ni kiongozi anaewajali wananchi anaowaongoza pamoja na kuwa na kiu ya kutaka wananchi wake waishi kwa upendo, amani, utulivu na maelewano zaidi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao walimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa wataendelea kumuunga mkono yeye na Serikali anayoiongoza na wale wote ambao hawapendi maendeleo ya Zanzibar pamoja na kukebehi juhudi zinazochukuliwa  ni vyema wakapuzwa na badala yake wamemtaka Rais Dk. Shein endelee kuchapa kazi.

Walieleza kuwa tokea kuanza kwa maradhi yanayosababishwa na virusi vya Corona duniani na hadi kuingia visiwani Zanzibar, Rais Dk. Shein amekuwa mstari wa mbele katika kuwapa maelekezo mazuri wananchi wake pamoja na matumaini makubwa katika kupambana na janga hilo sambamba na kuwatoa hofu.

Wakiwa katika maeneo mbali mbali kwa nyakati tofauti wananchi hao wameipongeza hotuba ya Rais Dk. Shein na kumpongeza yeye mwenyewe binafsi kwa yale yote aliyoyasema katika hotuba hiyo ambayo wamesema wamepata matumaini makubwa hasa baada ya kusikia kuwa Serikali inakusudia kuregeza masharti iliyoyaweka.

Katika pongezi hizo pia, wananchi hao wameipongeza misimamo yao thabiti ya Rais Dk. Shein pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli ya kutozifunga nyumba za ibada kwa hofu ya ugonjwa wa COVID-19 ambapo waumini wameweza kufanya ibada zao vyema ikiwemo sala ya Idd el Fitr.

Kwa upande wake Sheikh Fadhil Suleiman Soraga aliisifu na kuipongeza hotuba ya Rais Dk. Shein na juhudi anazozichukua na kueleza kuwa hotuba hiyo imekusanya mambo yote muhimu na kusisitiza kuwa kitendo cha Rais kuwatakia heri ya Idd el Fitr wananchi wake ni kitendo cha kiungwana ambacho kinafaa kupongezwa.

Wananchi hao pia, walieleza azma yao ya kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha uchumi, kudhibiti mapato na kuzilinda rasilimali mbali mbali ikiwa ni njia moja  ya uaminifu na kufanya uadilifu.

“Hapa Rais Dk. Shein amepigilia msumari aliposema wananchi ni lazima tuepuke kufanya vitendo viovu kama vile vya uonevu na hujuma ambavyo vinaweza kutupeleka katika mustakabali mbaya ambayo yote hayo ni mafunzo ya saumu, nampongeza kwa kusisitiza hili katika hotuba yake”, alisema Khamis Ame mkaazi wa Donge Pwani.

Aisha Ahmada Ali mwalimu wa skuli ya Migombani alipongeza hotuba ya Rais Dk. Shein hasa pale aliposema kuwa Serikali kwa upande wake itahakikisha kwamba inaendelea kuwapatia wafanyakazi fursa za kujiendeleza kwa elimu na ujuzi zaidi ili kuwajengea uwezo.

Nae Mkufufunzi  kutoka Skuli ya Afya na Sayansi za Tiba kutoka (SUZA)  Mohammed Sharksy aliipongeza hotuba ya Rais Dk. Shein hasa shukurani alizozitoa kwa madaktari na wataalamu wa afya ambao tangu yalipoanza maradhi ya COVID-19 wamekuwa wakifanya juhudi kubwa za kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kuwapa huduma walioathirika au wale walioonesha dalili.

Nao baadhi ya wananchi mbali mbali Kisiwani Pemba wametoa pongezi zao kutokana na hotuba ya Idd el Fitr aliyoitoa Dk. Shein kupitia vyombo vya habari na kusema kwamba iliojaa hekima na busara kubwa ikiwa ni pamoja na kuendeleza hatua za kujikinga na maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19.

Wamesema hotuba hiyo imewaondoshea hofu wananchi wa Zanzibar juu ya janga hilo  na kueleza kuwa tamko la kuangalia uwezekano wa kupunguza masharti linaonesha jinsi anavyowajali wananchi wake.

Walieleza kuwa kila siku Dk, Shein, amekuwa akihimiza Wananchi kuchukuwa tahadhari juu ya maambukizo hayo kwani anaelewa athari za kuwepo kwa wagonjwa wengi nchini.

Hata hivyo, walisema ni wajibu wa kila mwananchi kuona umuhimu wa kuchukuwa tahadhari zilizoelezwa na Rais Shein katika kujikinga na maradhi hayo na sio kupuuza kwani mgonjwa mmoja anaweza kuwaambukiza watu wengi na kwa wakati mmoja.

Bwana Juma Salum kutoka Wete Pemba, alisema kiongozi mzuri ni yule anaewahimiza wafuasi wake kutenda mambo mema kwa maana hiyo kitendo cha Rais Dk. Shein, cha kuwataka wananchi kuendelea kufanya mema waliojifunza katika mwezi mtukufu wa Ramadhani ni kuonesha mapenzi kwa anaowaongoza.

“Ni wazi kwamba Rais wetu amekuwa mstari wa mbele kila mara katika kutuhimiza sisi wananchi wake kufanya mema na kitendo cha kutuhimiza tuendeleze mafunzo ya mwezi wa Ramadhani ni kuonesha uadilifu wake kwa sisi anaotuongoza,”alisema Juma.

Akizungumzia kwa namna Rais Shein, alivyosikitika kutokana na wananchi wake kufunga mwezi mtukufu wa Ramadhani huku wakiwa wamekabiliwa na mitihani ya janga la COVID-19 sambamba na mafuriko kutokana na mvua kubwa ilionyesha inaonesha wazi juu ya kiongozi huyu anavyowajali wananchi wake.

“Tumepokea salamu zake za pole alizozitowa katika hotuba yake hiyo na hii inatupa moyo kuwa Serikali inayoongozwa na Dk, Shein iko pamoja na wananchi wake kwa hali yoyote inayowatokea kwa kweli tunampongeza kwa kutufariji,”alieleza.

Nae Mohammed Khamis Ali, mkaazi wa Chake Chake alisema kuwa hotuba ya Rais Dk. Shein ilikuwa na kila aina ya ujumbe kwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania nzima kwani ilijaa nasaha ambazo hata kwenye dini ya Kiislamu zimo na hii inaonesha jinsi Dk. Shein alivyokuwa Mcha Mungu na alivyobobea katika elimu ya dini ya Kiislamu.  

“Mimi kwa  nafsi yangu nampongeza Dk, Shein kwa namna anavyoonesha kuguswa na mambo mbali mbali yanayowapata wananchi wake yakiwemo maradhi, mafuriko, ukosefu wa huduma muhimu kama maji safi na salama ” alieleza Mohammed Khamis.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.