Habari za Punde

TAMWA - Zanzibar Yakabidhi Vifaranga Vya Kuku Kwa Familia Zilizopata Kadhia ya Udhalilishaji wa Watoto wao na Wanawake Unguja.

Mmoja wa Mwanafamilia Ndg.Saidi Dude (kulia) akipokea miongoni mwa vifaranga vya kuku kutoka kwa afisa masoko wa Tamwa - Zanzibar Ndg.Muhidini Ramadhan, vifaranga hivyo vimetolewa kwa lengo la kuwasaidia baadhi ya familia ambazo watoto wao wamekutwa na matukio mbali mbali ya udhalilishaji ili waweze kujikwambua kiuchumi.

Na.Mohammed Khamis - TAMWA-Zanzibar.

Chama cha Waandishi wa habari wanawake Tamwa-Zanzibar kwa lengo la kuhakikisha kesi za udhalilishaji kwa wanawake na watoto zinatolewa ushahidi Mahakamani kimeamua kuwasaidia wazazi na walezi wa watoto waliokumbwa na kadhia hiyo, kwa kuwakabidhi msaada wa vifaranga vya kuku ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Hayo yamebainishwa na Afisa wa sheria kutoka TAMWA -Zanzibar Ndg.Ulfat Abdi katika zoezi maalumu la utowaji wa vifaranga vya kuku kwa familia 15 kutoka shehia tofauti za Unguja.

Alisema kwa kipindi kirefu kumekuwepo na baadhi ya wazazi au walezi kushindwa kufika Mahakamani kutoa ushahidi wakati mwengine sababu kubwa ikitajwa kukosa nauli.

Alieleza kuwa kwa mazingira hayo Tamwa-Zanzibar wameona ipo haja kuzisaidia familia hizo kuwapa vifaranga hivyo ambavyo anaamini wakivitunza vyema wataweza kuzalisha kuku wengine na hatimae kuwa chanzo cha kujingizia kipato.

Pamoja na hayo afisa huyo alisema jamii inapaswa kufahamu kuwa suala la kutoa ushahidi katika kesi za udhalilishaji linapaswa kuzingatiwa na kuona umuhimu wake na kwamba bila ya ushahidi kesi hukosa nguvu na hatimae mshtakiwa anaweza kuachiwa huru.

‘’Leo tunawapa vifaranga hivi ambayo kila kimoja kimegharimu shilingi elfu tano tukiamini kwamba utakua mwanzo mzuri kwenu wa kutunza kuku hawa na kuwa sehemu ya utatuzi wa changamoto zenu’’aliongezea.

Miongoni mwa wanufaika hao awali walisema si kama hawapendi kujitokeza Mahakamani kutoa ushahidi lakini wakati mwengine wamekua wakijikuta hawahudhurii kwa kukosa kwao nauli ya kuwafikisha huko hivyo kesi zao hulazimika kuondoshwa Mahakamani.

Kwa masharti ya kutotajwa jina mmoja miongoni mwa mzazi ambae mtoto wake alifanyiwa udhalilishaji ikiwemo kubakwa alisema ni mara chache sana alizowahi  kuhudhuria wito wa polisi kwa kukosa nauli hivyo kupelekea kesi ya mtoto wake kusuasua.

Aliseka kama si msaada wa majirani angeshindwa kuhudhuria kabisa kwenye kesi hio na anaamini isingeweza kwenda Mahakamani.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Chama cha waandishi wa habari wanawake Tamwa-Zanzibar Dkt,Mzuri Issa aliwatala wale wote walionufaika na mradi huo kuhakikisha wanawatunza ili waweze kuonezeka zaidi hatimae waweze kuwasaidia wengine.

Aidha Mzuri alisema anaamini kuku hao iwapo wahusika watawatunza vyema baada ya muda mchache wataweza kuzalisha wengine zaidi na kuwa chanzo kikubwa cha kujingizia kipato.

Zaidi ya vifaranga vya kuku mia tatu vimekusudiwa kugawiwa kwa baadhi ya familia tofauti Unguja na Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.