RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyiameeleza azma ya Zanzibar kukuza na kuimarisha
uhusiano kati yake na Morocco hasa katika sekta ya utalii.
Dk. Hussein aliyasema hayo leo katika mazungumzo kati yake na Balozi wa
Ufalme wa Morocco katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Abdelilah Benryane,
mazungumzo yaliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.
Katika mazungumzo hayo, Dk. Hussein alisema kwamba kutokana na Morocco
kupata mafanikio makubwa katika sekta ya utalii, ni vyema Zanzibar ikapanua
wigo kutoka nchi hiyo.
Alisema kuwa kwa vile Zanzibar inategemea sana sekta ya utalii katika
uchumi wake itakuwa vyema kuwepo kwa mashirikiano ya pamoja kati ya pande mbili
hizo ili Zanzibar ipate mafanikio kama yale iliyoyapata Morocco katika sekta
hiyo.
Dk. Hussein alirejesha salamu za pongezi zilizotoka kwa kiongozi wa Morocco
kupitia Balozi huyo Mfalme Mohammed VI, zilizomtakia kazi njema na mafanikio
katika uongozi wake mpya wa Urais wa Zanzibar huku akiahidi kuzidisha
ushirikiano wake kwa nchi hiyo.
Aidha, Dk. Hussein alimueleza kiongozi huyo juhudi zitakazochukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kuimarisha
sekta ya utalii na kusisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano ya pamoja katika
sekta hiyo hasa ikizingatiwa kwamba Morocco ni miongoni mwa nchi za Bara la
Afrika iliyopiga hatua kubwa katika sekta ya utalii.
Pamoja na hayo, Dk. Hussein alimueleza Balozi huyo umuhimu wa
kushirikiana katika sekta nyenginezo za maendeleo hasa ikizingatiwa kwamba
Zanzibar ina kiu kubwa ya maendeleo hivi sasa.
Sambamba na hayo, Dk. Hussein alitumia fursa hiyo kuwakaribisha
wawekezaji wa Morocco kuja kuekeza Zanzibar katika sekta mbali mbali za
maendeleo.
Nae Balozi wa Morocco katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Abdelilah
Benryane,alianza kwa kumfikishia salamu za pongeza Rais Dk. Hussein Mwinyi
kutoka kwa Mfalme wa Morocco Mohammed VI, kufuatia ushindi wa kishindo wa Urais
wa Zanzibar.
Balozi huyo alimueleza Rais Dk. Hussein kwamba Morocco inajivunia
uhusiano na ushirikiano mwema uliopo kati yake na Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Balozi Abdelilah Benryane,
alisema kuwa Morocco iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika sekta ya
utalii, pamoja na sekta nyengine zote muhimu huku akieleza azma ya nchi yake ya
kutoa nafasi za masomo katika kada mbali mbali kwa wanafunzi wa elimu ya juu wa
Zanzibar ikiwa ni pamoja na nafasi za masomo ya elimu ya dini.
Balozi huyo pia, alieleza utayari wa nchi yake katika mashirikiano
kupitia mafunzo ya masuala ya kitalii kupitia chuo chake ambacho kina mahusiano
na nchi kadhaa za Ulaya na nyenginezo duniani
Aidha, alieleza haja ya kuwepo mashirikiano ya kubadilishana uzoefu na
utaalamu kwa wanafunzi wa Zanzibar na wale wa nchi yake kutokana na nchi hiyo
kuwa na vyuo vingi vinavyotoa mafunzo kadhaa.
Akizungumzia juu ya sekta ya utalii, alisema kuwa nchi yake imepiga
hatua kubwa katika sekta hiyo na kupokea wageni wengi hasa katika program ijulikanayo
‘Azur Blue’ iliyoanzishwa na kiongozi wa nchi hiyo Mfalme Momamed VI.
Hivyo, alieleza kuwa nchi yake itakuza uhusiano na Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo hasa ikizingatiwa kuwa nchini mwake kuna miundombinu mingi ya kuimarisha sekta hiyo vikiwemo vyuo vya mafunzo ya kitalii.
No comments:
Post a Comment